´Aqiydah yetu ni ileile kama ya wanazuoni na maimamu ambao wamekuja baada ya Maswahabah na wanafunzi wa Maswahabah, wakiwemo maimamu wanne na wengine wote waliopita juu ya njia hii. Walikuwa wengi kabisa. Maimamu, waliohuisha dini na wanazuoni ni wengi katika ummah huu na himdi zote njema ni stahiki ya Allaah. Waislamu wameafikiana juu ya uongofu wa maimamu hawa, bi maana waliipatia haki na kwamba walikuwa na uelewa, elimu, matendo na ufuataji. Baadhi ya watu wako na elimu lakini hawana matendo. Wengine wako na matendo lakini hawana elimu. Maimamu hawa walikuwa wanajua na wanatenda.

Ni wajibu kusema yale yaliyosemwa na Allaah, Mtume Wake (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam) na Muhaajiruun, Answaar na wale waliowafuata kwa wema katika mambo yote ya dini, khaswa Aayah na Hadiyth zinazozungumzia sifa. Yule anayeenda kinyume na hayo ni katika wapotofu na wapindaji. Ni wajibu kwako kufuata mfumo wa Salaf katika mambo yote ya dini kwa jumla na khaswa katika majina na sifa za Allaah. Usipinde kutoka katika mfumo huo. Au ukajidai kuwa wewe unajua jambo ambalo Salaf hawakulijua au unafahamu jambo ambalo wao hawakufahamu. Kwa sababu baadhi ya watu husema mambo kutoka vichwani mwao na hayakusemwa na Salaf wala wanazuoni. Wanakuja na tafsiri na ijtihaad kutoka vichwani mwao katika Tawhiyd ambayo ni maudhui ambayo hazikubaliwi ijtihaad za watu. Tawhiyd ni kufuata na kuigiliza peke yake. Unatakiwa kusema yale yaliyosemwa na Salaf na ukomeke na yale waliyokomeka nayo Salaf. Kwa sababu wao walikuwa watambuzi na imara zaidi katika elimu kuliko wewe. Inakutosha wewe kuwafuata, kuijua ´Aqiydah yao na kuifuata. Ama kuja na tafsiri na ijtihaad yako ni upotofu na batili. Wako watu wanaojifanya ni wasomi wamezua I´tiqaad mpya juu ya sifa za Allaah na kujengea hoja kwa vitabu fulani na fulani. Mwanafunzi hatakiwi kuthibitisha kitu isipokuwa yale yaliyothibitishwa na Salaf kwa mujibu wa Qur-aan na Sunnah. Usiseme jambo ambalo halikusemwa na Salaf. Hili ndio jambo la wajibu katika maudhui haya na mengine yote. Unalazimika kuwafuata Salaf katika mambo yote ya elimu. Inakutosha kupita juu ya njia yao ili kuungana nao. Usipinde kutoka katika njia yao ili usije kuuacha msafara wao.

  • Mhusika: Imaam Swaalih bin Fawzaan al-Fawzaan
  • Mfasiri: Firqatunnajia.com
  • Marejeo: at-Ta´liyqaat at-Tawdhwiyhiyyah ´alaa Muqaddimat-il-Fatwaaa al-Hamawiyyah, uk. 36-37
  • Imechapishwa: 25/07/2024