115. Allaah yuko juu ya mbingu na ujuzi Wake uko kila mahali

Maalik (93-179), imamu wa mji wa Kuhajiri.

129 – Ishaaq bin ´Iysaa at-Twabbaa´ amesimulia kuwa Maalik amesema:

”Kila ambapo tunajiwa na mtu ambaye ni bingwa wa mabishano kumshinda mwengine tutayaacha yale ambayo Jibriyl amemshushia Muhammad (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam) kwa sababu ya mabishano yake?”[1]

130 – ´Abdullaah bin Ahmad bin Hanbal amesimulia katika ”ar-Radd ´alaal-Jahmiyyah” amepokea kutoka kwa baba yake kutoka kwa ´Abdullaah bin Naafiy´, ambaye amesimulia kuwa Maalik bin Anas amesema:

”Allaah yuko juu ya mbingu na ujuzi Wake uko kila mahali. Hakuna chochote kinachojificha Kwake.”[2]

131 – al-Bayhaqiy amepokea kwa cheni ya wapokezi Swahiyh kutoka kwa Abur-Rabiy´, mtoto wa kaka yake na Rishdayn bin Sa´d, ambaye amesema: ”Nimemsikia ´Abdullaah bin Wahb akisema:

”Tulikuwa kwa Maalik bin Maalik wakati ambapo alikuja bwana mmoja na kusema: ”Ee Abu ´Abdillaah!

الرَّحْمَـٰنُ عَلَى الْعَرْشِ اسْتَوَىٰ

”Mwingi wa rehema amelingana juu ya ´Arshi.”

Amelingana vipi?” Maalik akainamisha kichwa chake mpaka kijasho kikamtoka. Halafu akasema: “Kulingana si kwamba ni kitu hakitambuliki[3]. Namna haijulikani. Kuamini hilo ni wajibu. Kuulizia hilo ni Bid´ah. Sikuoni vyengine zaidi ya kuwa ni mtu wa Bid´ah.” Baada ya hapo akaamrisha atolewe nje.”[4]

Haya yamethibiti kutoka kwa Maalik. Mfano wa hayo yamepokelewa kutoka kwa Rabiy´ah, mwalimu wa Maalik. Ahl-us-Sunnah wote wanasema hivo. Hatuelewi namna ya Kulingana, bali ni jambo tusilolijua. Hata hivyo kulingana kunatambulika na ni kama ambavyo kunalingana Naye, kama alivyoyaeleza hayo katika Kitabu Chake. Hatuingii kwa ndani, wala hatufukui. Wala hatupekui yale yanayopelekea hayo kwa njia ya kukanusha wala kuthibitisha. Bali tunanyamaza na tunasimama kama walivyosimama Salaf. Tunajua kuwa kama yangelifasiriwa basi Maswahabah na wanafunzi wao wangekimbilia kufanya hivo badala tu ya kuthibitisha, kuyapitisha na kuyanyamazia. Tunajua kwa yakini kabisa ya kwamba hakuna mfano wa Allaah inapokuja katika sifa Zake, kulingana Kwake wala kushuka Kwake. Allaah ametakasika kutokana na yale wanayoyasema madhalimu!

[1] Ibn ´Abdil-Barr amepokea mfano wake katika  “al-Jaamiy´” (2/95) na al-Harawiy katika “Dhamm-ul-Kalaam” (1/94/5) kupitia kwa at-Twabbaa´. Cheni ya wapokezi ni Swahiyh.

[2] Ameipokea na ´Abdullaah katika “as-Sunnah”, uk. 5, na pia Abu Daawuud katika “Masaail-ul-Imaam Ahmad”, uk. 263, al-Aajurriy, uk. 289, na al-Laalakaa’iy (1/92/2). Cheni yake ya wapokezi ni Swahiyh. Kwa mujibu wa al-Aajurriy Ahmad ameijengea kama hoja.

al-Kawthariy amesema katika dibaji ya ”al-Asmaa´ was-Swifaat:

”Yumo ´Abdullaah bin Naafiy´ al-Aswamm, mpokeaji wa masimulizi dhaifu na yanayogongana.”

Jambo hilo ni katika ghushi au hadaa yake. Hakuna yeyote katika maimamu wa kujeruhi ambaye amemjeruhi kwa namna hiyo. Bali wamesema kuwa yeye ndiye ambaye alikuwa ni mjuzi zaidi wa maoni na masimulizi ya Maalik. Tazama ”at-Tahdhiyb”. Aidha ni kosa kutambulika kwake kama al-Aswamm; alikuwa anatambulika kama as-Swaa-igh.

[3] Kwa maana kwamba inatambulika. Kwa ajili hiyo tunawaona pindi maimamu wanaponukuu masimulizi haya kutoka kwa Imaam Maalik, wanasema kwamba Kulingana kunatambulika, kama atakavyosema al-Qurtwubiy huko mbele ya kitabu. Kwa msemo mwingine kulingana kunajulikana inapokuja kilugha, kwa njia ya kwamba mtu anaweza kufasiri na kuifanyia tarjama kwenda katika lugha nyingine. Ni katika tafsiri ambazo wanazijua wale waliobobea katika elimu. Hata hivyo kuhusu namna ilivyo sifa hiyo na sifa zingine zote ni katika zile tafsiri ambazo hakuna wazijuazo isipokuwa Allaah pekee.

[4] ad-Daarimiy katika “ar-Radd ´alaal-Jahmiyyah”, uk. 33, na al-Laalakaa’iy (1/92/2). Mtunzi wa “Furqaan-ul-Qur-aan bayna Swifaat-il-Khaaliq wa Swifaat-il-Akwaan” amenukuu masimulizi kwa njia ya ”Kulingana kumetajwa”, uk. 16. Sijayapata wala kuyaona kwa mtindo huo kutoka kwa yeyote anayeaminika. Kwa ajili hiyo ndio maana ameikumbatia kihivo kwa sababu ya kutaka kuitakasa ´Aqiydah yake ya kukanusha maana ya kulingana na kwamba ni yenye kutambulika kwa Maalik.

  • Mhusika: Imaam Shams-ud-Diyn Muhammad bin Ahmad adh-Dhahabiy
  • Mfasiri: Firqatunnajia.com
  • Marejeo: al-´Uluww lil-´Aliy al-Ghaffaar, uk. 138-139
  • Imechapishwa: 17/07/2024
  • taaliki: Imaam Muhammad Naaswir-ud-Diyn al-Albaaniy