Haya ndio ambayo ametueleza Mtume (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam). Haya yanatuhimiza kushikamana barabara na yale aliyokuwemo Mtume (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam) na Maswahabah zake. Jengine tunachofaidika ni kuwa tusidanganyike na mapote na wingi wake na tukafikiria kuwa hawawezi kuwa katika upotofu kwa sababu ni wengi. Wapotofu ni wengi. Watu wa haki ni wachache. Hatudanganyiki na wingi. Bali ni lazima kwetu kuyaangalia yale waliyomo watu; yale ambayo ni haki, ijapo yanafanywa na mtu mmoja tu, au pengine hakuna yeyote anayeyafanya, tunatakiwa kuyafanyia kazi. Na yale ambayo ni upotofu basi tunayaacha, ijapo yanafanywa na watu wengi:

وَمَا أَكْثَرُ النَّاسِ وَلَوْ حَرَصْتَ بِمُؤْمِنِينَ

“Na wengi wa watu si wenye kuamini hata ukijitahidi vipi.”[1]

وَمَا وَجَدْنَا لِأَكْثَرِهِم مِّنْ عَهْدٍ ۖ وَإِن وَجَدْنَا أَكْثَرَهُمْ لَفَاسِقِينَ

”Hatukuwakuta wengi wao kuwa ni wakweli wa ahadi. Bali hakika Tumewakuta wengi wao ni mafasiki.”[2]

وَإِن تُطِعْ أَكْثَرَ مَن فِي الْأَرْضِ يُضِلُّوكَ عَن سَبِيلِ اللَّـهِ

“Ukiwatii wengi walioko ulimwenguni, basi watakupoteza na njia ya Allaah.”[3]

Kinachozingatiwa sio ule wingi. Aayah hizi ni dalili inayoonyesha kuwa wingi si wenye kuzingatiwa unapokuwa hauko juu ya haki. Aidha inafahamisha pia kwamba wachache hawatakiwi kuipa mgongo haki, ijapo ni kikosi kidogo cha watu au mmoja. Mtume (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam) ametueleza mipasuko itayokuwepo na akatueleza namna ya kuokoka na mifarakano hiyo, nayo ni:

“Ni lile litakalofuata mfano wa yale niliyomi mimi hii leo na Maswahabah zangu.”

Mahimizo haya yanahusu pia majina na sifa za Allaah na Tawhiyd. Yule anayeshikamana na yale aliyokuwemo Mtume (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam) na Maswahabah zake inapokuja katika majina na sifa za Allaah na Tawhiyd, basi huyo ni katika kundi Lililookoka. Na yule atakayejiunga na mapote yaliyopinda inapokuja katika majina na sifa za Allaah, basi ni katika mapote potofu.

Hadiyth hii ni katika miujiza ya Mtume (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam). Ameelezea juu ya jambo kabla ya kutokea kwake – na baadaye likatokea kweli. Lengo juu ya hilo ni kutahadharisha kujiunga na mapote haya wakati wa kuzuka kwake na pia mahimizo ya kuwa na msimamo juu ya haki, ijapo hakuna walioshikamana nayo isipokuwa tu wachache. Jengine ni kuwa Hadiyth inahimiza kuwa na subira. Kwa sababu ambaye ameshikamana na haki anaweza kuudhiwa, akapewa mtihani, akapigwa, akauliwa au akafungwa jela. Kwa ajili hiyo asubiri na asijiunge na wapotofu. Vinginevyo atakutana na misukosuko na shari.

[1] 12:103

[2] 7:102

[3] 6:116

  • Mhusika: Imaam Swaalih bin Fawzaan al-Fawzaan
  • Mfasiri: Firqatunnajia.com
  • Marejeo: at-Ta´liyqaat at-Tawdhwiyhiyyah ´alaa Muqaddimat-il-Fatwaa al-Hamawiyyah, uk. 165-167
  • Imechapishwa: 10/09/2024