11. Taathira ya Qur-aan kwa wafanya ´ibaadah na waja wema

Watu wengi wema walisikia Aayah hii ikisomwa ambapo ikawaathiri kwa njia nyingi. Wako ambao walikufa kwa kupata mshtuko wa moyo. Wengine wakatubu na wakayaacha yale waliyomo. Nimetaja khabari zao katika kitabu “al-Istighnaa’ bil-Qur-aan”. Amesema (Ta’ala):

لَوْ أَنزَلْنَا هَـٰذَا الْقُرْآنَ عَلَىٰ جَبَلٍ لَّرَأَيْتَهُ خَاشِعًا مُّتَصَدِّعًا مِّنْ خَشْيَةِ اللَّـهِ

”Lau Tungeliiteremsha hii Qur-aan juu ya mlima, basi ungeliuona unanyenyekea ukipasukapasuka kutokana na khofu ya Allaah.”[1]

Abu ´Imraan al-Juuniy amesema:

”Naapa kwa Allaah! Mola wetu ametuwekea wazi ndani ya Qur-aan kwa namna ambayo angeliiwekea wazi milima basi angeliifuta na kuisawazisha.”

Maalik bin Diynaar (Rahimahu Allaah) alikuwa akisoma Aayah hii kisha anasema:

”Naweza kuwaapia ya kwamba hakuna mja yeyote ambaye ataamini Qur-aan hii isipokuwa moyo wake utapasuka.”

Imepokelewa kwamba al-Hasan (Rahimahu Allaah) amesema:

“Ee mwanadamu! Shaytwaan akijaribu kukushawishi utende dhambi, au ukijiambia kufanya hivyo, basi hapo fikiria juu ya yale ambayo Allaah amekubebesha kutoka katika Kitabu chake. Kama angeliibebesha milima imara, basi ingelinyenyekea na kupasuka. Je, humsikii akisema:

لَوْ أَنزَلْنَا هَـٰذَا الْقُرْآنَ عَلَىٰ جَبَلٍ لَّرَأَيْتَهُ خَاشِعًا مُّتَصَدِّعًا مِّنْ خَشْيَةِ اللَّـهِ

”Lau Tungeliiteremsha hii Qur-aan juu ya mlima, basi ungeliuona unanyenyekea ukipasukapasuka kutokana na khofu ya Allaah.”

Amekupigia mifano ili uweze kuitafakari, kuizingatia na matokeo yake ukomeke na kumuasi Allaah (‘Azza wa Jall). Wewe, ee mwanadamu, una haki zaidi ya kunyenyekea kutokana na utajo wa Allaah, yale aliyokubebesha katika Kitabu Chake na akakupa katika hekima. Kwa sababu mbele yako uko na hesabu na ima Pepo au Moto.

[1] 59:21

  • Muhusika: Imaam Zayn-ud-Diyn ´Abdur-Rahmaan bin Rajab al-Hanbaliy (afk. 795)
  • Tarjama: Firqatunnajia.com
  • Marejeo: al-Khushuu´ fiys-Swalaah, uk. 52-54
  • Imechapishwa: 24/11/2025