Abu Ja´far at-Twahaawiy (Rahimahu Allaah) amesema:

35 – Madai yote ya unabii baada yake ni upotofu na kuchupa mipaka.

MAELEZO

Mtume (Swalla Allaahu ´alayhi wa salla) amewaeleza ummah wake hali ya kuwanasihi na kuwatahadharisha kwamba watakuja baada yake madajali wengi. Amesema katika baadhi yake:

”Wote watakuwa wakidai kuwa ni Manabii, lakini mimi ndiye Nabii wa mwisho. Hakuna Nabii mwingine baada yangu.”[1]

Miongoni mwa wongo hao ni Mirza Ghulaam Ahmad al-Qaadiyaaniy. Bwana huyu alijidai kuwa ni Nabii. Yuko na wafuasi India, Ujerumani, Uingereza na Marekani. Wanayo misikiti wanayowapotosha waislamu kwayo. Kipindi fulani walikuwepo wachache huko Syria, lakini Allaah  akawatokomeza kabisa. Wanazo I´tiqaad zingine mbali na kuamini kuwa kuna Nabii mwingine anayekuja baada ya Muhammad (Swalla Allaahu ´alayhi wa salla).

Mtangulizi wake ni Ibn ´Arabiy Suufiy. Wameandika maneno yake kutilia nguvu ´Aqiydah yao iliyotajwa. Licha ya kwamba Mashaykh wamethibitisha kuwa Qaadiyaaniyyah ni makafiri, hawakuweza kuwaraddi kwa sababu Qaadiyaaniyyah wanajengea hoja kwa maneno ya Ibn ´Arabiy. Hakuna nafasi wala muda wa kuzitaja ´Aqiydah zao kwa kina, lakini hapana shaka yoyote wao ni miongoni mwa wale aliowakusudia Mtume wa Allaah (Swalla Allaahu ´alayhi wa salla) pale aliposema:

”Mwishoni mwa zama watajitokeza madajli na waongo. Watasimulia mambo ambayo hamjapatapo kuyasikia nyinyi wala baba zenu. Jihadharini nao na tahadharisheni nao wasije kukupotosheni wala wasikufitinisheni.”[2]

[1] Muslim na wengineo. Tazama “as-Swahiyhah” (1683).

[2] at-Twahaawiy katika “Mushkil-ul-Aathaar” (4/104) na Muslim (1/9).

  • Mhusika: Imaam Muhammad Naaswir-ud-Diyn al-Albaaniy
  • Mfasiri: Firqatunnajia.com
  • Marejeo: al-´Aqiydah at-Twahaawiyyah – Sharh wa Ta´liyq, uk. 21-22
  • Imechapishwa: 16/09/2024