Kuhusu kuamini makadirio ndani yake kunaingia kuamini mambo manne:

1 – Allaah (Subhaanah) ameyajua yaliyokuwepo, yatayokuwepo, amezijua hali za waja, amezijua riziki zao, muda wao wa kueshi, matendo yao na mengine katika mambo yao. Hakuna chochote katika hayo kinachojificha Kwake (Subhaanahu wa Ta´ala). Amesema (Subhaanah):

أَنَّ اللَّـهَ بِكُلِّ شَيْءٍ عَلِيمٌ

“Hakika Allaah juu ya kila kitu ni mjuzi.” (02:231)

لِتَعْلَمُوا أَنَّ اللَّـهَ عَلَىٰ كُلِّ شَيْءٍ قَدِيرٌ وَأَنَّ اللَّـهَ قَدْ أَحَاطَ بِكُلِّ شَيْءٍ عِلْمًا

“… ili mpate kujua kwamba Allaah juu ya kila kitu ni muweza na kwamba Allaah amekwishakizunguka kila kitu kwa ujuzi.” (65:12)

2 – Ameyaandika (Subhaanah) yale yote aliyoyakadiria na kuyapanga. Amesema (Subhaanah):

قَدْ عَلِمْنَا مَا تَنقُصُ الْأَرْضُ مِنْهُمْ ۖ وَعِندَنَا كِتَابٌ حَفِيظٌ

“Hakika Sisi tunajua kinachopunguzwa na ardhi kutokana nao [miili yao iliyokufa] na tunacho Kitabu kinachohifadhi.” (50:04)

وَكُلَّ شَيْءٍ أَحْصَيْنَاهُ فِي إِمَامٍ مُّبِينٍ

“Kila kitu Tumekirekodi barabara katika kitabu kinachobainisha.” (36:12)

أَلَمْ تَعْلَمْ أَنَّ اللَّـهَ يَعْلَمُ مَا فِي السَّمَاءِ وَالْأَرْضِ ۗ إِنَّ ذَٰلِكَ فِي كِتَابٍ ۚ إِنَّ ذَٰلِكَ عَلَى اللَّـهِ يَسِيرٌ

“Je, hujui kwamba Allaah anajua yale yote yaliyomo mbinguni na ardhini? Hakika hayo yamo katika Kitabu. Hakika hayo kwa Allaah ni mepesi.” (22:70)

3 – Kuamini matakwa Yake yenye kutendeka. Anayoyataka, hutokea, na asiyoyataka, hayatokei. Amesema (Subhaanah):

إِنَّ اللَّـهَ يَفْعَلُ مَا يَشَاءُ

“Hakika Allaah anafanya atakavyo.” (22:18)

إِنَّمَا أَمْرُهُ إِذَا أَرَادَ شَيْئًا أَن يَقُولَ لَهُ كُن فَيَكُونُ

“Hakika hapana vyengine amri Yake anapotaka chochote kile hukiambia: “Kuwa!” – nacho huwa.” (36:82)

وَمَا تَشَاءُونَ إِلَّا أَن يَشَاءَ اللَّـهُ ۚ إِنَّ اللَّـهَ كَانَ عَلِيمًا حَكِيمًا

“Hamtotaka chochote isipokuwa atake Allaah; hakika Allaah daima ni mjuzi, Mwenye hekima.” (76:30)

4 – Kuumba Kwake (Subhaanah) vile vyote vilivyopo. Hakuna muumbaji mwingine wala Mola asiyekuwa Yeye. Amesema (Subhaanah):

اللَّـهُ خَالِقُ كُلِّ شَيْءٍ ۖوَهُوَ عَلَىٰ كُلِّ شَيْءٍ وَكِيلٌ

“Allaah ni Muumbaji wa kila kitu Naye juu ya kila kitu ni mdhamini anayetegemewa.” (39:62)

يَا أَيُّهَا النَّاسُ اذْكُرُوا نِعْمَتَ اللَّـهِ عَلَيْكُمْ ۚ هَلْ مِنْ خَالِقٍ غَيْرُ اللَّـهِ يَرْزُقُكُم مِّنَ السَّمَاءِ وَالْأَرْضِ ۚ لَا إِلَـٰهَ إِلَّا هُوَ ۖفَأَنَّىٰ تُؤْفَكُونَ

“Enyi watu! Kumbukeni neema za Allaah juu yenu. Je, kuna muumbaji mwingine badala ya Allaah anayekuruzukuni kutoka mbinguni na kwenye ardhi? Hapana mungu wa haki isipokuwa Yeye, basi mbona mnageuzwa?” (35:03)

Kuamini makadirio kunajumuisha kuamini mambo haya manne kwa mujibu wa Ahl-us-Sunnah wal-Jamaa´ah. Hivyo ni tofauti na baadhi ya Ahl-ul-Bid´ah waliopinga baadhi ya mambo hayo.

  • Mhusika: Imaam ´Abdul-´Aziyz bin ´Abdillaah bin Baaz
  • Mfasiri: Firqatunnajia.com
  • Marejeo: al-´Aqiydah as-Swahiyhah wa maa yudhwaadduhaa, uk. 09-10
  • Imechapishwa: 30/05/2023