Kuamini Vitabu maana yake ni kuamini ule uongofu na nuru iliyomo ndani yake na kwamba Allaah ameviteremsha kwa Mitume Wake ili kumwongoza mwanaadamu. Vikubwa katika Vitabu hivyo ni vile vitatu; Tarwaat, Injiyl na Qur-aan. Kikubwa katika hivyo vitatu ni Qur-aan tukufu. Nayo ndio miujiza mikubwa. Amesema (Ta´ala):

قُل لَّئِنِ اجْتَمَعَتِ الْإِنسُ وَالْجِنُّ عَلَىٰ أَن يَأْتُوا بِمِثْلِ هَـٰذَا الْقُرْآنِ لَا يَأْتُونَ بِمِثْلِهِ وَلَوْ كَانَ بَعْضُهُمْ لِبَعْضٍ ظَهِيرًا

“Sema: “Ikiwa watajumuika watu na majini ili walete mfano wa hii Qur-aan hawatoweza kuleta mfano wake, japokuwa watasaidiana wao kwa wao.””[1]

Ahl-us-Sunnah wal-Jamaa´ah wanaamini kuwa Qur-aan – ni mamoja herufi na maana yake – ni maneno ya Allaah yaliyoteremshwa na ambayo hayakuumbwa. Hili ni tofauti na wanavyosema Jahmiyyah na Mu´tazilah kwamba Qur-aan – herufi na maana yake vyote viwili – imeumbwa. Vivyo hivyo ni tofauti na wanavyosema Ashaa´irah na wenye kujifananisha nao ya kwamba maneno ya Allaah ni maana peke yake. Kuhusu herufi wanasema kuwa zimeumbwa. ´Aqiydah zote mbili ni batili. Amesema (Ta´ala):

وَإِنْ أَحَدٌ مِّنَ الْمُشْرِكِينَ اسْتَجَارَكَ فَأَجِرْهُ حَتَّىٰ يَسْمَعَ كَلَامَ اللَّـهِ

“Ikiwa mmoja wa washirikina akikuomba umlinde, basi mlinde mpaka asikie maneno ya Allaah.”[2]

يُرِيدُونَ أَن يُبَدِّلُوا كَلَامَ اللَّـهِ

“Wanataka kubadilisha maneno ya Allaah.”[3]

Ni maneno ya Allaah na si maneno ya mwengine.

[1] 17:88

[2] 09:06

[3] 48:15

  • Mhusika: Imaam Swaalih bin Fawzaan al-Fawzaan
  • Mfasiri: Firqatunnajia.com
  • Marejeo: Min Usuwl ´Aqiydah Ahl-is-Sunnah wal-Jamaa´ah, uk. 19-20
  • Imechapishwa: 12/05/2022