Shaykh-ul-Islaam Muhammad bin ´Abdil-Wahhaab (Rahimahu Allaah) amesema:

Mtume wa mwisho ni Muhammad (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam).

MAELEZO

Dalili ya hilo ni maneno Yake (Ta´ala):

مَّا كَانَ مُحَمَّدٌ أَبَا أَحَدٍ مِّن رِّجَالِكُمْ وَلَـٰكِن رَّسُولَ اللَّـهِ وَخَاتَمَ النَّبِيِّينَ

“Hakuwa Muhammad baba wa yeyote miongoni mwa wanaume wenu, lakini ni Mtume wa Allaah na ni mwisho wa Manabii.” (33:40)

Kwa hivyo hakuna Nabii atayekuja baada ya Muhammad (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam). Kukisemwa ya kwamba Mtume ´Iysaa bin Maryam (´alayhis-Swalaatu was-Salaam) atatumwa katika zama za mwisho, tunasema kuwa ni haki. Lakini hata hivyo hatotumwa kama Mtume muhuishaji. Atahukumu kwa mujibu wa Shari´ah ya Mtume Muhammad (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam). Jengine ni kuwa ni wajibu kwa ´Iysaa na Manabii wengine wote kumuamini Muhammad (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam), kumfuata na kumnusuru. Allaah (Ta´ala) amesema:

وَإِذْ أَخَذَ اللَّـهُ مِيثَاقَ النَّبِيِّينَ لَمَا آتَيْتُكُم مِّن كِتَابٍ وَحِكْمَةٍ ثُمَّ جَاءَكُمْ رَسُولٌ مُّصَدِّقٌ لِّمَا مَعَكُمْ لَتُؤْمِنُنَّ بِهِ وَلَتَنصُرُنَّهُ ۚ قَالَ أَأَقْرَرْتُمْ وَأَخَذْتُمْ عَلَىٰ ذَٰلِكُمْ إِصْرِي ۖ قَالُوا أَقْرَرْنَا ۚ قَالَ فَاشْهَدُوا وَأَنَا مَعَكُم مِّنَ الشَّاهِدِينَ

“Na pale Allaah alipochukua ahadi kwa Manabii: “Nikisha kupeni Kitabu na  hekima, kisha akakujieni Mtume mwenye kusadikisha mliyo nayo, ni juu yenu mumuamini na  mumnusuru.” Akasema: “Je, mmekiri nammekubali kushika agizo langu juu ya hayo?” Wakasema: “Tumekubali.” Akasema: “Basi shuhudieni na Mimi nipamoja nanyi katika kushuhudia. Watakaogeuka baada ya haya basi hao ndio mafusaki.” (03:81)

Mtume huyu mwenye kusadikisha ile haki waliyokuwamo alikuwa ni Muhammad (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam). Haya yamepokelewa katika Hadiyth Swahiyh kutoka kwa Swahabah mtukufu Ibn ´Abbaas (Radhiya Allaahu ´anh) na wengineo.

  • Mhusika: Imaam Muhammad bin Swaalih bin ´Uthaymiyn
  • Mfasiri: Firqatunnajia.com
  • Marejeo: Sharh Kashf-ish-Shubuhaat, uk. 17-20
  • Imechapishwa: 04/10/2023