15 – Khaythamah bin Sulaymaan ametukhabarisha: Ishaaq bin Sayyaar an-Nuswaybiy ametuhadithia: Abu Haatim na Ibraahiym bin Muhammad bin ´Amaarah wametuhadithia: Ahmad bin Yahyaa as-Suufiy ametuhadithia: Shujaa´ bin Makhlad ametuhadithia: Abu ´Aaswim ametuhadithia, kutoka kwa Sufyaan, kutoka kwa ´Ammaar ad-Duhniy, kutoka kwa Muslim al-Batwiyn, kutoka kwa Sa´iyd bin Jubayr, kutoka kwa Ibn ´Abbaas – Shujaa´ amesimulia kwamba alimuuliza Mtume (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam) kuhusiana maneno Yake (´Azza wa Jall):

وَسِعَ كُرْسِيُّهُ السَّمَاوَاتِ وَالْأَرْضَ 

”Kursiy Yake imeenea mbingu na ardhi.”

Akasema:

”Kursiy ni mahali pa kuweka Nyayo Zake mbili na ´Arshi hakuna awezaye kukisia ukubwa wake.”

Namna hii ndivo alivyopokea Shujaa´ bin Makhlad kutoka kwa Mtume (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam). Ishaaq bin Sayyaar ameisimulia kutoka kwa Abu ´Aaswim, kutoka kwa Ibn ´Abbaas kama masimulizi yake mwenyewe. Vivyo hivyo wameipokea marafiki zake na ath-Thawriy kutoka kwake. Vilevile imepokelewa kutoka kwa ´Ammaar ad-Duhniy kwa njia ya maneno ya Swahabah. Abu Bakr al-Hudhaliy na wengineo wameipokea kutoka kwa Sa´iyd bin Jubayr, ambaye amesema:

”Kursiy ni mahali pa kuweka Nyayo Zake mbili.”

Ja´far bin Abiyl-Mughiyrah ameipokea kutoka kwa Sa´iyd bin Jubayr, kutoka kwa Ibn ´Abbaas, ambaye amesema:

”Kursiy ni ujuzi Wake.”

Hakuna mwingine zaidi ya Ja´far aliyeisimulia. Isitoshe si mwenye nguvu katika kusimulia kutoka kwa Sa´iyd bin Jubayr.

16 – Tumekhabarishwa hayo na Ahmad bin Muhammad bin Ibraahiym, mtumwa wa Banuu Haashim aliyeachwa huru: Muhammad bin ´Abdil-Wahhaab ametuhadithia, kutoka kwa Ibn Abiy Tammaam: Aadam bin Abiy Iyaas ametuhadithia: Hushaym bin Mutwarrif ametuhadithia, kutoka kwa Ja´far bin Abiyl-Mughiyrah, kutoka kwa Sa´iyd bin Jubayr, kutoka kwa Ibn ´Abbaas, ambaye amesema kuhusu:

وَسِعَ كُرْسِيُّهُ السَّمَاوَاتِ وَالْأَرْضَ 

”Kursiy Yake imeenea mbingu na ardhi.”

”Ujuzi Wake.”

Hadiyth hii ni yenye kutambulika kutoka kwa Mutwarrif, kutoka kwa Ja´far bin Abiyl-Mughiyrah, ambaye amepwekeka katika kuisimulia.

Imepokelewa pia kuwa Abu Muusa al-Ash´ariy amesema:

”Kursiy ni mahali pa kuweka Nyayo mbili.”

17 – Tumekhabarishwa hayo na Ahmad bin Ibraahiym al-Baghdaadiy huko Makkah: Muhammad bin Yaziyd ametuhadithia: ´Aliy bin Muslim ametuhadithia: ´Abdus-Swamad bin ´Abdil-Waarith ametuhadithia: Muhammad bin Jahaadah ametuhadithia, kutoka kwa Salamah bin Kuhayl, kutoka kwa ´Amaarah bin ´Umayr, kutoka kwa Abu Muusa, ambaye amesema:

”Kursiy ni mahali pa kuweka Nyayo mbili na inatoa sauti kama sogi.”

Nahshal ameipokea kutoka kwa adh-Dhwahhaak, kutoka kwa Ibn ´Abbaas, ambaye amesema kuhusiana na maneno Yake (Ta´ala):

وَسِعَ كُرْسِيُّهُ السَّمَاوَاتِ وَالْأَرْضَ 

”Kursiy Yake imeenea mbingu na ardhi.”

”Ujuzi Wake.”

Masimulizi haya hayakuthibiti. adh-Dhwahhaak hakusikia chochote kutoka kwa Ibn ´Abbaas na Nahshal alikuwa mwenye kuachwa.

Miongoni mwa mambo yanayotilia nguvu tafsiri ya Ibn ´Abbaas na Abu Muusa juu ya Kursiy ni kwamba ar-Rabiy´ bin Anas amesimulia kwamba Maswahabah wa Mtume (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam) walisema kumwambia Mtume (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam):

”Ikiwa Kursiy imezizunguka mbingu na ardhi, vipi kuhusu ´Arshi?” Ndipo Allaah (´Azza wa Jall) akateremsha:

وَمَا قَدَرُوا اللَّهَ حَقَّ قَدْرِهِ 

”Hawakumkadiria Allaah inavyostahiki kukadiriwa!”

  • Muhusika: Imaam Muhammad bin Ishaaq bin Mandah (afk. 395)
  • Tarjama: Firqatunnajia.com
  • Marejeo: ar-Radd ´alaal-Jahmiyyah, uk. 44-46
  • Imechapishwa: 09/06/2026
  • Taaliki: ´Allaamah ´Aliy bin Naaswir al-Faqiyhiy