Allaah (Ta´ala) amesema:

إِنَّ الَّذِينَ يَتْلُونَ كِتَابَ اللَّـهِ وَأَقَامُوا الصَّلَاةَ وَأَنفَقُوا مِمَّا رَزَقْنَاهُمْ سِرًّا وَعَلَانِيَةً يَرْجُونَ تِجَارَةً لَّن تَبُورَ لِيُوَفِّيَهُمْ أُجُورَهُمْ وَيَزِيدَهُم مِّن فَضْلِهِ ۚ إِنَّهُ غَفُورٌ شَكُورٌ

“Hakika wale wanakisoma Kitabu cha Allaah na wakasimamisha swalah na wakatoa sehemu katika yale Tuliyowaruzuku – kwa siri na dhahiri – wanataraji biashara isiyoenda patupu ili [Allaah] awalipe ujira wao kikamilifu na awazidishie kutokana na fadhilah Zake. Hakika Yeye ni Mwingi wa kusamehe, Mwingi wa kupokea shukurani.”[1]

Tumesimuliwa kutoka kwa ´Uthmaan bin ´Affaan (Radhiya Allaahu ´anh) ambaye ameeleza ya kwamba Mtume wa Allaah (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam) amesema:

”Mbora wenu ni yule anayejifunza Qur-aan na akaifundisha.”[2]

Ameipokea Imaam Abu ´Abdillaah Muhammad bin Ismaa´iyl bin Ibraahiym al-Bukhaariy katika ”as-Swahiyh” yake, ambayo ndio sahihi zaidi ya vitabu baada ya Qur-aan.

´Aaishah (Radhiya Allaahu ´anhaa) amesimulia kwamba Mtume wa Allaah (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam) amesema:

”Yule anayesoma Qur-aan na yeye ni hodari nayo atakuwa pamoja na Malaika waandishi watukufu wema, na yule anayesoma Qur-aan huku anajikokota ndani yake na ni ngumu kwake, basi atapata ujira mara mbili.”[3]

Ameipokea al-Bukhaariy na Abul-Husayn Muslim bin al-Hajjaaj bin Muslim al-Qushayriy an-Naysaabuuriy katika ”as-Swahiyh” zao.

Abu Muusa al-Ash´ariy (Radhiya Allaahu ´anh) amesimulia kwamba Mtume wa Allaah (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam) amesema:

”Mfano wa muumini anayesoma Qur-aan ni kama limau kubwa; harufu yake ni nzuri na ladha yake ni nzuri. Mfano wa muumini asiyesoma Qur-aan ni kama tende; haina harufu lakini ladha yake ni nzuri tamu. Mfano wa mnafiki anayesoma Qur-aan ni kama mrihani; harufu yake ni nzuri lakini ladha yake ni chungu. Mfano wa mnafiki asiyesoma Qur-aan ni kama tango pori chungu; haina harufu na ladha yake ni chungu.”[4]

Ameipokea al-Bukhaariy na Muslim.

´Umar bin al-Khattwaab (Radhiya Allaahu ´anh) amesimulia ya kuwa Mtume (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam) amesema:

”Hakika Allaah (Ta´ala) huwainua watu kwa maneno haya na huwashusha wengine kwa hayo.”[5]

Ameipokea Muslim.

Abu Umaamah al-Baahiliy (Radhiya Allaahu ´anh) amesimulia ya kuwa amemsikia Mtume wa Allaah (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam) akisema:

”Isomeni Qur-aan, kwani itakuja siku ya Qiyaamah hali ya kuwa ni mwombezi kwa watu wake.”[6]

Ameipokea Muslim.

Ibn ´Umar (Radhiya Allaahu ´anhumaa) ameeleza kwamba Mtume (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam) amesema:

”Hakuna husuda isipokuwa katika mambo mawili: mtu ambaye Allaah amempa Qur-aan, naye anasimama nayo usiku na mchana, na mtu mwingine ambaye Allaah amempa mali, naye anaitumia usiku na mchana.”[7]

Ameipokea al-Bukhaariy na Muslim.

[1] 35:29-30

[2] al-Bukhaariy (5027-5028), Abu Daawuud (1452), at-Tirmidhiy (2907-2908) na Ibn Maajah (211-212).

[3] al-Bukhaariy (4937) na Muslim (798).

[4] al-Bukhaariy (5020, 5059 na 7560) na Muslim (797).

[5] Muslim (817).

[6] Muslim (804).

[7] al-Bukhaariy (5025 na 7529) na Muslim (815).

  • Muhusika: Imaam Yahyaa bin Sharaf an-Nawawiy (afk. 677)
  • Tarjama: Firqatunnajia.com
  • Marejeo: at-Tibyaan fiy Aadaabi Hamalat-il-Qur-aan, uk. 17-18
  • Imechapishwa: 17/08/2026