03. Kuomba du´aa katika theluthi ya mwisho ya usiku

33 – Abu Hurayrah (Radhiya Allaahu ´anh) amesimulia kwamba Mtume wa Allaah (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam) amesema:

”Mola wetu (Tabaarak wa Ta´ala) hushuka kila usiku katika mbingu ya chini ya dunia pale kunapobaki theluthi ya mwisho ya usiku na anasema mpaka kuingie alfajiri: “Nani anayeniomba Nimuitikie? Ni nani anayeniuliza Nimpe? Ni nani anayenitaka msamaha Nimsamehe?”[1]

Kuna maafikiano juu yake.

Imekuja katika upokezi wa Muslim:

“Allaah (Subhaanahu wa Ta´ala) hushuka kila usiku katika mbingu ya chini ya dunia pale kunapopita theluthi ya usiku ya kwanza na anasema: “Mimi ndiye Mfalme, Mimi ndiye Mfalme! “Nani anayeniomba Nimuitikie? Ni nani anayeniuliza Nimpe? Ni nani anayenitaka msamaha Nimsamehe?”

MAELEZO

Hadiyth hii ni miongoni mwa zile Hadiyth zilizopokelewa kwa mapokezi tele. Isitoshe ni Hadiyth tukufu inayothibitisha kushuka kwa Mungu.

Hadiyth inamthibitishia Mola kushuka ambako kunalingana na utukufu na ukubwa Wake. Anashuka anavotaka. Halinganishwi wala hafananishwi na ushukaji wa viumbe. Anashuka akiwa juu ya ´Arshi, kama inavyolingana na utukufu na ukubwa Wake.

Hadiyth inafahamisha ubora wa kuswali katika theluthi ya mwisho ya usiku kwa kuafikiana na wakati huu mbora na ndio wakati ambao inamalizika witr yake (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam).

Hadiyth pia inajulisha ubora wa kuomba du´aa mwishoni mwa usiku, kwani kuna matarajio makubwa ya kukubaliwa.

[1] al-Bukhaariy (1145) na Muslim (785).

  • Muhusika: ´Allaamah ´Abdul-´Aziyz bin ´Abdillaah ar-Raajihiy
  • Tarjama: Firqatunnajia.com
  • Marejeo: al-Ad´iyah wal-Adhkaar, uk. 36-37
  • Imechapishwa: 07/10/2025