Swali linauliza namna hii:

“Ni ipi njia bora ya kufanya Da´wah?”

Mimi nawaambia wanawake:

وَقَرْنَ فِي بُيُوتِكُنَّ

“Kaeni majumbani mwenu.”[1]

Nyinyi hamna chochote kinachohusiana na Da´wah. Mimi napinga neno “Da´wah” kutumia kati ya vijana na kwamba wao ni ´walinganizi’. Ni kana kwamba Da´wah imekuwa ni mtindo wa leo. Kila mtu anayejua kitu katika elimu basi amekuwa ni mlinganizi. Jambo halikuishilia kwa wavulana limeenda mpaka kwa wasichana na wake walioko majumbani. Inatokea mara nyingi wanaacha kusimamia majukumu ya majumbani mwao, waume zao na watoto wao na kukiendea kitu ambacho sio wajibu kwao, nacho ni Da´wah.

Hapo kitambo niliulizwa swali na mwanamke mmoja aliyesikia kwenye kaseti yangu kutoka Kuwait nikisema kwamba haijuzu kwa mwanamke kutoka kwa ajili ya kufanya Da´wah. Na hapa hivi sasa kunaulizwa ni njia ipi bora ya kufanya Da´wah. Kimsingi ni kwamba mwanamke anatakiwa kukaa nyumbani kwake na haijuzu kwake kutoka nje isipokuwa kwa haja ambayo ni kubwa. Nilitaja jinsi Mtume (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam) alivosema:

“Hata hivyo majumba yao ni bora kwao.”

Majumba yao ni bora kwao kuliko kuswali kwao misikitini. Hivi sasa tunaona jambo lililoenea kati ya wanawake pindi wanapotoka nje kwa wingi kwa ajili ya kuswali katika mkusanyiko, sembuse swalah ya ijumaa:

“Hata hivyo majumba yao ni bora kwao.”

Isipokuwa kama kuna msikiti ambao kuna mwanamme mwanachuoni anayewafunza wahudhuriaji elimu ya dini. Katika hali hii ni sawa kwa mwanamke kutoka kwenda kuswali msikitini na kusikiliza elimu.

Ikiwa mwanamke atakaa nyumbani kwake na akasoma vitabu ambavo analetewa na ndugu zake wa kiume kisha akajiamulia siku moja kujiliwa na wanawake au yeye akaenda katika nyumba ya mmoja wao, hili ni bora yeye akatoka kwenda nyumbani kwa mmoja wao kuliko wote kutoka kumwendea yeye. Ama yeye kutoka na akasafiri (na pengine hata akasafiri pasi na Mahram ili kujihalalishia Da´wah yake) ni katika Bid´ah za kisasa. Sizungumzii wanawake peke yao. Nawazungumzia hata wanamme ambao wana hamasa ya kufanya Da´wah ilihali bado wakingali chipukizi katika mambo ya elimu.

[1] 33:33

  • Mhusika: Imaam Muhammad Naaswir-ud-Diyn al-Albaaniy
  • Mfasiri: Firqatunnajia.com
  • Marejeo: Fataawaa Juddah (25)
  • Imechapishwa: 05/07/2021