Unasema kwenye barua yako:

“Walikuta maneno yake yanaashiria kuwa alikuwa ni mtu mwenye Ikhlaasw na mpwekeshaji.”

Kusema kuwa alikuwa na Ikhlaasw au hapana hili ni jambo analojijua Allaah peke yake. Ikhlaasw ni kitendo kilichojificha na hakuna akijuae isipokuwa Allaah pekee. Mtume (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam) amesema katika Hadiyth Swahiyh:

“Hakika kila kitendo kinategemea na nia na kila mtu atalipwa kwa kile alichonuia.”

Abu Muusaa amesimulia kwamba Mtume (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam) amesema:

“Yule mwenye kupigana ili neno la Allaah liwe juu, basi huyo ndiye anapigana katika njia ya Allaah.”

Ahmad amepokea kupitia Ibn Mas´uud ambaye ameeleza kuwa Mtume (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam) amesema:

“Allaah ndiye mwenye kujua zaidi ni nia ipi alokuwa nayo yule mwenye kuuliwa kati ya safu mbili.”

Vilevile umesema:

“… alikuwa mpwekeshaji.”

Huu ni ushuhuda na mapendekezo yako ambayo Allaah atakuja kukuuliza juu yake. Ilikuwa ni wajibu kwako kujifikiria kabla ya kuzungumza namna hiyo. Hivi kweli umetia mapendekezo haya mahali pake stahiki? Mimi sielewi kama wewe hutambui kuwa al-Bannaa alitumbukia kwenye shirki na kwamba alikuwa na anasa na washirikina na shirki zao na kuwachagua kuwa wanachama katika mfumo wake. Pamoja na yote hayo alikuwa akisema katika sherehe ya mazazi ya Mtume (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam):

“Mpenzi huyu (yaani Mtume) amedhuhuria pamoja na wapenzi wake na amemsamehe kila mmoja kwa yaliyopitika.”

Bi maana Mtume (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam) anahudhuria sherehe zao na kuwabariki na kuwasamehe madhambi yao. Ee Shaykh! Hii ni shirki au hapana? Mtu anayezungumza na kuimba hivi ni mpwekeshaji? Mtu mwenye kuahidi kiapo cha utiifu na usikivu kwa Hasswaafiyyah na Shaadhiliyyah anahesabika kuwa ni mpwekeshaji? Je, unajua kuwa Suufiyyah ni wapwekeshaji na wanalingania katika Tawhiyd au ni washirikina na wanalingania katika shirki na Bid´ah? Unajua kuwa Suufiyyah imejengwa juu ya shirki na imechanganyika na shirki na Bid´ah? Unajua kuwa Hasan al-Bannaa alikuwa akienda kila ijumaa kilomita 20 kwenye kaburi la kuhani wa Suufiyyah, kama ad-Dasuuqiy na Sanjar, na kilomita 20 kurudi? Mpwekeshaji hufanya hivo?

Ee Shaykh! Mche Allaah na tambua kuwa umeisononesha Tawhiyd yako na kuitukana shahaadah yako kwa kusema kuwa washirikina na watu wa Bid´ah ni wapwekeshaji. Tubu kwa Allaah na urejee Kwake kabla hujachelewa.

Mtu aliyekuwa akilingania katika Uislamu na akimpwekesha Allaah ilikuwa ni Shaykh Muhammad bin ´Abdil-Wahhaab (Rahimahu Allaah) na wale waliopita katika njia yake miongoni mwa wanachuoni na viongozi katika wakati wake na wakati wa Muhammad bin Su´uud mpaka hii leo.

Mtu aliyekuwa akilingania katika Uislamu na akimpwekesha Allaah ilikuwa ni Shaykh ´Abdullaah bin Muhammad al-Qar´aawiy aliyeeneza Tawhiyd kusini kwa msaada wa mfalme ´Abdul-´Aziyz.

Ee Shaykh! Ninakuuliza kwa jina la Allaah; lau muulizaji angelikuuliza juu ya mtu mwenye kwenda kuanzia tarehe moja Rabiy´-ul-Awwaal mpaka tarehe kumi na mbili na kuimba kwa nyimbo zilizo na yafuatayo:

“Mpenzi huyu (yaani Mtume) amehudhuria pamoja na wapenzi wake na amemsamehe kila mmoja kwa yaliyopitika.”

Ungelimhukumu kwa shirki au Tawhiyd[1]? Ungelijibu nini? Vipi ungelijibu lau ungeliulizwa juu ya mtu mwenye kutembea kilomita 20 kwa wiki ili kutembelea makaburi ya Suufiyyah na kimomita 20 kurudi? Je, ungelisema kuwa ni Sunniy au ni mtu wa Bid´ah? Je, ungelisema kuwa ni mpwekeshaji au ni mshirikina[2]?

Ee Shaykh! Mche Allaah na rejea katika usawa. Tubu kwa Allaah kwani hakika anaikubali Tawbah. Usiwapoteze watu, na khaswa wanafunzi, kwa kuwatetea watu wa Bid´ah.

[1] Sisemi kuwa Hasan al-Bannaa alikufa akiwa kafiri kwa vile sijui alivokufa. Hata hivyo ninasema kuwa haijuzu kumsifu kuwa ni Muwahhid – mtu mwenye kumwabudu Allaah pekee – wakati imepothibiti kuwa alitumbukia katika yale yaliyopokelewa kutoka kwa wafuasi na wanusuraji wake.

[2] Hapa ninahukumu maneno, au kitendo, yanayotoka kwa mtu huyu na ambayo yamethibitishwa kuwa ni shirki kubwa. Ama kuhusu mtu huyu kwa dhati yake, sionelei kuwa ni kafiri kutokana na shirki yake kwa vile sijui alikufa katika hali gani.

  • Mhusika: ´Allaamah Ahmad bin Yahyaa an-Najmiy
  • Mfasiri: Firqatunnajia.com
  • Marejeo: Radd-ul-Jawaab, uk. 23-27
  • Imechapishwa: 05/07/2020