40. Mapendezo ya kuoga kwa yule mwenye kumuosha maiti

31- Imependekezwa kwa yule mwenye kuosha aoge pia. Amesema (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam):

“Mwenye kumuosha maiti aoge na mwenye kumbeba atawadhe.”

Ameipokea Abu Daawuud (02/62-63), at-Tirmidhiy (02/132) na ameifanya kuwa nzuri. Vilevile ameipokea Ibn Hibbaan katika “as-Swahiyh” yake (751- al-Mawaarid), at-Twayaalisiy (2314) na Ahmad (280, 433, 454, 472). kwenye njia kutoka kwa Abu Hurayrah. Baadhi ya njia zake ni nzuri na zengine ni Swahiyh juu ya sharti za Muslim[1] – Ibn-ul-Qayyim katika “Tahdhiyb-us-Sunan” ametaja njia kumi na moja kutoka kwake kisha akasema:’

“Njia zote hizi zinafahamisha kuwa Hadiyth imehifadhiwa.”

Ibn-ul-Qattwaan ameisahihisha. Vivyo hivyo Ibn Hazm katika “al-Mahallaa” (01/250, 02/23-25) na al-Haafidhw katika “at-Talkhiysw” (02/134- muniyriyyah) ambapo akasema:

“Kama itakuwa na hali mbaya sana basi itakuwa nzuri (Hasan).”

Udhahiri wa maamrisho yanafidisha uwajibu. Lakini hatukuyasema kuwa ni wajibu kwa sababu ya Hadiyth mbili ambazo zimeishilia kwa Swahabah – lakini hata hivyo hukumu yake ni kurufaishwa kwa Mtume (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam):

Ya Kwanza: Kutoka kwa Ibn ´Abbaas ambaye amesema:

“Hamna ulazima wa kuoga wakati mtapomuosha maiti wenu. Kwani hakika maiti wenu sio najisi. Inakutosheni kuiosha mikono yenu.”

Ameipokea al-Haakim (01/386) na al-Bayhaqiy (03/398) kupitia kwa Ibn ´Abbaas ambaye amerufaisha kutoka kwa Mtume (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam).

al-Haakim amesema:

“Swahiyh juu ya sharti za al-Bukhaariy.” na adh-Dhahabiy akaafikiana naye. Hadiyth ni yenye cheni ya wapokezi, kama alivosema al-Haafidhw katika “at-Talkhiysw”. Kwa sababu ndani yake yumo ´Amr bin ´Amr ambaye kuna maneno dhidi yake. adh-Dhahabiy mwenyewe katika “al-Miyzaan”, baada ya kutaja maneno ya maimamu juu yake, amesema:

“Hadiyth ya Swaalih ni nzuri.”

Kisha nikayapa nguvu maoni ya sawa ni kwamba Hadiyth hiyo ni yenye kuishilia kwa Swahabah. Hayo nimeyahakiki katika “adh-Dhwa´iyfah” (6304).

Ya pili: Ibn ´Umar (Radhiya Allaahu ´anhumaa) amesema:

“Tulikuwa tukiwaosha maiti miongoni mwetu wako wenye kuoga na miongoni mwetu wengine hawaogi.”

Ameipokea ad-Daaraqutwniy (191), al-Khatwiyb katika “at-Tariykh” yake (05/424) kwa cheni ya wapokezi Swahiyh, kama alivosema al-Haafidhw. Imaam Ahmad ameashiria katika hilo. al-Khatwiyb amepokea kutoka kwake kwamba alimhimiza mtoto wake ´Abdullaah kuiandika Hadiyth hii.

[1] Nimeyabainisha hayo ubainifu wa kutosheleza katika kitabu changu ”ath-Thamara al-Mustatwaab” na ”Kitaab-ul-Ghusl”.

  • Mhusika: Imaam Muhammad Naaswir-ud-Diyn al-Albaaniy
  • Mfasiri: Firqatunnajia.com
  • Marejeo: Ahkaam-ul-Janaa-iz wa Bid´ahaa, uk. 71-72
  • Imechapishwa: 18/02/2020