32. Namna ya kutaamiliana na anayekusalimia kipindi cha Khutbah

Swali 32: Ni ipi hukumu ikiwa imamu anatoa Khutbah ambapo mtu mwingine akakutolea salamu kwa kunyoosha mkono wake[1]?

Jibu: Mwashirie kwamba ni wakati wa Khutbah na uweke mkono wako juu ya mkono wake akikunyooshea pasi na kuzungumza. Mtume wa Allaah (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam) ameamrisha kunyamaza na akasema:

”Ukimwambia rafiki yako siku ya ijumaa nyamaza ilihali huku imamu yuko anatoa Khutbah, basi umefanya upuuzi.”[2]

Ameipokea al-Bukhaariy na Muslim.

Amefanya kule kuamrisha kwake mema wakati wa Khutbah ni upuuzi. Tusemeje maneno mengine?

Vilevile amesema (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam) katika Hadiyth Swahiyh:

“Yeyote atakayegusa changarawe basi amefanya upuuzi.”[3]

Muumini katika ijumaa anatakiwa kunyamaza, anyenyekee na atahadhari kucheza na changarawe au kitu kingine. Akisalimiwa na yeyote basi amwashirie kwa mkono wake na wala asizungumze. Akiweka mkono wake juu ya mkono wake pindi atapomnyooshea pasi na kuzungumza ni sawa kama tulivyotangulia kutaja. Baada ya kumalizika Khutbah amfunze kwamba kitendo hicho hakitakikani na kwamba kilichosuniwa kwake atapoingia na imamu anatoa Khutbah, basi aswali Rak´ah mbili ambazo ni za mamkuzi ya msikiti na wala asimsalimie yeyote mpaka Khutbah imalizike. Anapochemua amuhimidi Allaah ndani ya nafsi yake na wala asinyanyue sauti yake.

[1] Majmuu´-ul-Fataawaa (12/410-411).

[2] al-Bukhaariy (882) na Muslim (1404).

[3] Muslim (1419) na at-Tirmidhiy (458).

  • Mhusika: Imaam ´Abdul-´Aziyz bin ´Abdillaah bin Baaz
  • Mfasiri: Firqatunnajia.com
  • Marejeo: Ahkaam Swalaat-il-Jumu´ah wal-Jamaa´ah, uk. 71-72
  • Imechapishwa: 03/12/2021