29. Vichinjwa vinavyochinjwa katika maombolezo ya al-Husayn

Kutoka kwa ´Abdul-´Azizy bin ´Abdillaah bin Baaz kwenda kwa ndugu muheshimiwa X – Allaah amuwafikishie kwa yale anayomridhia na amzidishie elimu na imani. Aamiyn.

Salaam ´alaykum wa Rahmatullaahi wa Barakaatuh

Amma ba´d:

Nimefikiwa na barua yenu tukufu – Allaah akuunganishe kwa kamba ya uongofu na uwafikishaji – na yale maswali mawili yanayotambulika iliokuwa imebeba:

Swali 01: Ni ipi hukumu ya mahuzuniko yanayofanywa na ki-Raafidhwah juu ya al-Husayn na yale yanayofanyika ndani yake katika kupiga makofi, kupiga mashavu, kupasua nguo na kujipigapiga ambako wakati mwingine kunafikia kujipiga kwa minyororo pamoja na kuwaomba uokozi na watu watukufu wa nyumbani kwa Mtume (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam)?

Jibu: Haya ni maovu yanayochukiza na Bid´ah inayokemewa. Ni lazima kuiacha. Haijuzu kushiriki ndani yake. Haijuzu kula katika kile chakula kinacholetwa. Mtume (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam) na Maswahabah zake (Radhiya Allaahu ´anhum), wakiwemo watu wa nyumbani kwake (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam), na wengineo hawakufanya hivo. Amesema (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam):

“Yeyote atakayezua kitendo kisichokuwa katika amri yetu atarudishiwa mwenyewe.”[1]

Kuna maafikiano juu ya usahihi wake.

Vilevile amesema (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam):

“Yeyote atakayefanya kitendo kisichoafikiana na amri yetu atarudishiwa mwenyewe.”[2]

Ameipokea Muslim katika “as-Swahiyh” yake na al-Bukhaariy ameipokea katika “as-Swahiyh” yake kwa cheni ya wapokezi pungufu kwa njia ya kukata.

Zipo Hadiyth nyingi zenye maana kama hii.

Kuhusu kuwataka uokozi wafu na watu wa nyumbani kwa Mtume (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam) ni shirki kubwa kwa maafikiano ya wanazuoni. Allaah (Subhaanah):

وَمَن يَدْعُ مَعَ اللَّـهِ إِلَـٰهًا آخَرَ لَا بُرْهَانَ لَهُ بِهِ فَإِنَّمَا حِسَابُهُ عِندَ رَبِّهِ ۚ إِنَّهُ لَا يُفْلِحُ الْكَافِرُونَ

“Yeyote yule anayeomba pamoja na Allaah mungu mwengine – hana ushahidi wa wazi juu ya hilo – basi hakika hesabu yake iko kwa Mola wake. Hakika hawafaulu makafiri.”[3]

وَأَنَّ الْمَسَاجِدَ لِلَّـهِ فَلَا تَدْعُوا مَعَ اللَّـهِ أَحَدًا

“Hakika misikiti yote ni ya Allaah, hivyo basi msiombe yeyote pamoja na Allaah.”[4]

وَمَنْ أَضَلُّ مِمَّن يَدْعُو مِن دُونِ اللَّـهِ مَن لَّا يَسْتَجِيبُ لَهُ إِلَىٰ يَوْمِ الْقِيَامَةِ وَهُمْ عَن دُعَائِهِمْ غَافِلُونَ وَإِذَا حُشِرَ النَّاسُ كَانُوا لَهُمْ أَعْدَاءً وَكَانُوا بِعِبَادَتِهِمْ كَافِرِينَ

“Ni nani aliyepotea zaidi kuliko yule anayemwomba badala ya Allaah, ambao hatowaitikia mpaka siku ya Qiyaamah nao hawatambui maombi yao. Na [Qiyaamah] watakapokusanywa watu [miungu ya uongo] watakuwa maadui wao na watakuwa kwa ‘ibaadah zao ni wenye kuzikanusha.”[5]

يُولِجُ اللَّيْلَ فِي النَّهَارِ وَيُولِجُ النَّهَارَ فِي اللَّيْلِ وَسَخَّرَ الشَّمْسَ وَالْقَمَرَ كُلٌّ يَجْرِي لِأَجَلٍ مُّسَمًّى ۚ ذَٰلِكُمُ اللَّـهُ رَبُّكُمْ لَهُ الْمُلْكُ ۚ وَالَّذِينَ تَدْعُونَ مِن دُونِهِ مَا يَمْلِكُونَ مِن قِطْمِيرٍ إِن تَدْعُوهُمْ لَا يَسْمَعُوا دُعَاءَكُمْ وَلَوْ سَمِعُوا مَا اسْتَجَابُوا لَكُمْ ۖ وَيَوْمَ الْقِيَامَةِ يَكْفُرُونَ بِشِرْكِكُمْ ۚ وَلَا يُنَبِّئُكَ مِثْلُ خَبِيرٍ

“Anauingiza usiku ndani ya mchana na anauingiza mchana ndani ya usiku na anaitisha jua na mwezi; kila kimoja kinakwenda hadi muda maalum uliokadiriwa. Huyo ndiye Allaah, Mola wenu, ufalme ni Wake pekee.  Wale mnaowaomba badala Yake hawamiliki hata kijiwavu cha kokwa ya tende. Mkiwaomba, hawasikii maombi yenu, na hata wakisikia, hawatakuitikieni na siku ya Qiyaamah watakanusha ushirikina wenu na wala hakuna atakayekujulisha vyema kama Mwenye khabari zote za ndani.”[6]

Zipo Aayah nyingi zenye maana kama hii.

Mtume (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam) amesema:

“Du´aa ndio ´ibaadah.”[7]

Wameipokea watunzi wa Sunan wanne kwa cheni ya wapokezi Swahiyh. Muslim amepokea katika “as-Swahiyh” yake kupitia kwa kiongozi wa waumini ´Aliy bin Abiy Twaalib (Radhiya Allaahu ´anh) ambaye amesimulia kuwa Mtume (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam) amesema:

“Allaah amlaania mwenye kumchinjia asiyekuwa Allaah.”[8]

Kwa hivyo ni lazima kwa Shiy´ah na wengine wote kumtakasia ´ibaadah Allaah pekee na wajihadhari na kumwomba uokozi mwengine asiyekuwa Allaah, kuwaomba waliokufa na viumbe visivyoonekana. Ni mamoja ni watu wa nyumbani kwa Mtume (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam) au wengineo. Sambamba na hilo ni lazima watahadhari kuomba viumbe visivyokuwa na uhai na kuvitaka uokozi katika masanamu, miti, nyota na vyenginevyo kutokana na zile dalili za zilizowekwa katika Shari´ah. Ahl-us-Sunnah wal-Jamaa´ah katika Maswahabah na wengineo wameafikiana juu ya hayo.

Swali 02: Ni ipi hukumu ya kichinjwa kinachochinjwa maeneo hayo katika mnasaba huu? Vivyo hivyo ni ipi hukumu ya vile vinywaji vinavyosambazwa mitaani kwa watu wa kawaida?

Jibu: Ni Bid´ah yenye kukemewa. Haijuzu kushiriki, kula katika vichinjwa hivi wala kula katika vinywaji hivi. Ikiwa mchinjaji amechinjwa kwa ajili ya asiyekuwa Allaah katika watu wa nyumbani kwa Mtume (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam) au wengineo ni shirki kubwa. Allaah (Subhaanah) amesema:

قُلْ إِنَّ صَلَاتِي وَنُسُكِي وَمَحْيَايَ وَمَمَاتِي لِلَّـهِ رَبِّ الْعَالَمِينَ لَا شَرِيكَ لَهُ ۖ وَبِذَٰلِكَ أُمِرْتُ وَأَنَا أَوَّلُ الْمُسْلِمِينَ

”Sema: “Hakika swalah yangu na kichinjwa changu na uhai wangu na kufa kwangu ni kwa ajili ya Allaah pekee, Mola wa walimwengu, hali ya kuwa hana mshirika; na kwa hayo ndio nimeamrishwa, nami ni muislamu wa kwanza.”[9]

إِنَّا أَعْطَيْنَاكَ الْكَوْثَرَ فَصَلِّ لِرَبِّكَ وَانْحَرْ

“Hakika Sisi tumekupa al-Kawthar. Basi swali na uchinje kwa ajili ya Mola wako.”[10]

Aayah na Hadiyth zilizo na maana kama hii ni nyingi.

Namwomba Allaah atuwafikishe sisi, nyinyi na ndugu zetu wengine wa Kiislamu katika yale yote anayoyapenda na kuyaridhia na atuepushe sisi na nyinyi na ndugu zetu wengine kutokamana na fitina zenye kupotosha. Kwani hakika Yeye yukaribu, Mwenye kuitikia.

as-Salaam ´alaykum wa Rahmatullaahi wa Barakaatuh.

[1] al-Bukhaariy (2697) na Muslim (1718).

[2] Muslim (1718).

[3] 23:117

[4] 72:18

[5] 46:05-06

[6] 35:13-14

[7] Ahmad (17919), Abu Daawuud (1479), at-Tirmidhiy (2969) na Ibn Maajah (3828).

[8] Muslim (1978).

[9] 06:162-163

[10] 108:01-02

  • Mhusika: Imaam ´Abdul-´Aziyz bin ´Abdillaah bin Baaz
  • Mfasiri: Firqatunnajia.com
  • Marejeo: at-Tahdhiyr min Fitnat-il-Qubuur, uk. 104-107
  • Imechapishwa: 13/07/2022