23. Mtume (صلى الله عليه وسلم) ni mtu na anafikwa na yale yanayowafika watu wengine

Ahl-us-Sunnah wal-Jamaa´ah wanaamini kwamba Mtume (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam) ni mtu  na anafikwa na zile sifa zote za kiutu na za kimwili; analala, anakula, anakunywa, anapatwa na ugonjwa, anapatwa na maumivu, anahuzunika, anaridhia na anakasirika (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam). Vilevile anakufa kama wanavokufa watu wengine:

إِنَّكَ مَيِّتٌ وَإِنَّهُم مَّيِّتُونَ ثُمَّ إِنَّكُمْ يَوْمَ الْقِيَامَةِ عِندَ رَبِّكُمْ تَخْتَصِمُونَ

“Hakika wewe utakufa nao pia watakufa. Kisha hakika nyinyi siku ya Qiyaamah mtakhasimiana mbele ya Mola wenu.”[1]

وَمَا مُحَمَّدٌ إِلَّا رَسُولٌ قَدْ خَلَتْ مِن قَبْلِهِ الرُّسُلُ ۚ أَفَإِن مَّاتَ أَوْ قُتِلَ انقَلَبْتُمْ عَلَىٰ أَعْقَابِكُمْ ۚ وَمَن يَنقَلِبْ عَلَىٰ عَقِبَيْهِ فَلَن يَضُرَّ اللَّـهَ شَيْئًا

“Muhammad si chochote isipokuwa ni Mtume tu [na] wamekwishapita kabla yake Mitume [wengine]. Je, akifa au akiuawa mtageuka nyuma ya visigino vyenu? Atakayegeuka nyuma ya visigino vyake, basi hatomdhuru Allaah kitu chochote.”[2]

Hapana shaka yoyote kuwa Mtume (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam) amekufa kifo cha kimwili ambacho roho yake imetengana na mwili wake. Familia na Maswahabah zake walimfanyia yale wanayowafanyia watu wengine katika mambo ya kifo. Isipokuwa tu hawakumvua nguo zake (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam) wakati wa kumuosha. Jengine linalojulikana ni kwamba hawakumswalia swalah ya mkusanyiko. Watu walikuwa wakimswalia mmojammoja. Kwa sababu yeye (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam) ndiye kiongozi.

Mwenye kudai kwamba yeye (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam) yuko hai ndani ya kaburi lake uhai wa kimwili na si uhai wa ndani ya kaburi na kwamba anaswali, anafunga, anahiji na kwamba anayajua yale yanayosemwa na yanayofanywa na Ummah basi amezungumza maneno asiyokuwa na ujuzi nayo.

[1] 39:30-31

[2] 03:144

  • Mhusika: Imaam Muhammad bin Swaalih bin ´Uthaymiyn
  • Mfasiri: Firqatunnajia.com
  • Marejeo: Manhaj Ahl-is-Sunnah wal-Jamaa´ah fiy-´Aqiydah wal-´Amal, uk. 35
  • Imechapishwa: 20/08/2019