145. al-´Ayyaashiy upotoshaji wake wa tisa wa al-A´raaf

al-´Ayyaashiy amesema:

“Haaruun bin ´Ubayd amepokea kutoka kwa mmoja wao ambaye amesimulia: “Kuna kundi la watu kutoka Kuufah lililokuja kwa kiongozi wa waumini na kusema: “Ee kiongozi wa waumini! Nondo hizi zinauzwa katika masoko yetu.” Kiongozi wa waumini akatabasamu kisha akasema: “Inukeni nikuonyesheni maajabu. Msiseme juu ya wasii wenu isipokuwa tu kheri.” Wakainuka pamoja naye wakafika mpaka kwenye bahari. Akatema mate kwenye bahari na akatamka baadhi ya maneno. Tahamaki kukajitokeza nondo iliyokuwa imeinua kichwa na imefunua kinywa. Kiongozi wa waumini akaiambia: “Wewe ni nani? Ole wako wewe na watu wako.” Ikasema: “Sisi tunatoka katika kile kijiji kilicho kando na bahari ambacho Allaah amewazungumzia kwa kusema:

وَاسْأَلْهُمْ عَنِ الْقَرْيَةِ الَّتِي كَانَتْ حَاضِرَةَ الْبَحْرِ إِذْ يَعْدُونَ فِي السَّبْتِ إِذْ تَأْتِيهِمْ حِيتَانُهُمْ يَوْمَ سَبْتِهِمْ شُرَّعًا وَيَوْمَ لَا يَسْبِتُونَ ۙ لَا تَأْتِيهِمْ

“Waulize kuhusu mji ambao ulikuwa kando ya bahari walipovuka mipaka ya Sabt: walipowajia samaki wao juu juu siku yao ya Sabt, na siku isiyokuwa ya Sabt hawakuwajia.”[1]

Allaah alituwekea uongozi mbele yetu, lakini hatukuuchukua. Ndipo Allaah akatugeuza; baadhi yetu tunaishi nchikavu na baadhi yetu wengine tunaishi baharini. Wale ambao wako katika bahari sisi ndio nondo. Ama wale walio nchikavu ndio panya mijusi na panya za kukimbia.” Kiongozi wa waumini akatugeukia na kusema: “Mmesikia alivosema?” Tukasema: “Ndio.” Akasema: “Ninaapa kwa Yule ambaye alimtuma Muhammad kwa utume mtapata hedhi kama wanavopata hedhi wanawake wenu.”[2]

Yule ambaye imepokelewa kutoka kwa mmoja wao wanakusudiwa maimamu wao.

Huu ni  uongo mkubwa kabisa. Uongo wa kwanza:

“Msiseme juu ya wasii wenu isipokuwa tu kheri.”

´Aliy (Radhiya Allaahu ´anh) kamwe asingejisifu na kudai kwamba yeye ndiye wasii wa Mtume wa Allaah (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam).

Isitoshe jengine ni kwamba anatumia mienendo ya wachawi pale ambapo anatema mate baharini kwa kuashiria makarama. Baada ya hapo nondo wanasema kuwa wao ni kutoka katika ule mji wa wana wa israaiyl ambao Allaah aliwageuza na kuwafanya kuwa nyani na nguruwe.

Katika uongo mkubwa kabisa ni kule kusema kwamba hawakugeuzwa isipokuwa ni kwa sababu ya kupinga uongozi wa ´Aliy. Sababu ya kugeuzwa kumebainishwa; ni kule kukataa kukomeka na matendo waliyokatazwa. Amesema (Ta´ala):

وَلَقَدْ عَلِمْتُمُ الَّذِينَ اعْتَدَوْا مِنكُمْ فِي السَّبْتِ فَقُلْنَا لَهُمْ كُونُوا قِرَدَةً خَاسِئِينَ

“Hakika mlikwishawajua  wale miongoni mwenu waliovuka mipaka ya Sabt tukawaambia: “Kuweni manyani waliotwezwa!”[3]

[1] 07:163

[2] Tafsiyr al-´Ayyaashiy (2/35).

[3] 02:65

  • Mhusika: ´Allaamah Rabiy´ bin Haadiy al-Madkhaliy
  • Mfasiri: Firqatunnajia.com
  • Marejeo: al-Intiswaar li Kitaab-il-´Aziyz al-Jabbaar, uk. 205-206
  • Imechapishwa: 12/09/2018