14. Mtume anamsikia ndani ya kaburi lake anayemswalia?

Swali: Mtu akija kwenye kaburi la Mtume (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam) kwa ajili ya kumswalia na kumtakia amani anamsikia na kumuona? Je, ´Aqiydah hii ni ya kishirikina?

Jibu: Kilichowekwa katika Shari´ah kwa muislamu pindi anapotembelea msikiti wa Mtume (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam) basi aanze kuswali ndani ya msikiti wake (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam). Akiweza kufanya hivo katika Rawdhwah tukufu ndio bora zaidi. Kisha aelekee katika kaburi la Mtume (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam) na asimame mbele yake kwa adabu na kwa sauti ya chini halafu amsalimie Mtume (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam), marafiki zake wawili (Radhiya Allaahu ´anhumaa). Abu Daawuud amepokea kwa cheni ya wapokezi ilio nzuri kupitia kwa Abu Hurayrah (Radhiya Allaahu ´anh) ya kwamba Mtume (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam) amesema:

“Hakuna yeyote anayenitolea salamu isipokuwa Allaah hunirudishia roho yangu mpaka nikaweza kumuitikia salamu.”[1]

Baadhi ya wanazuoni wamejengea hoja kwa Hadiyth hii juu ya kwamba yeye (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam) anasikia salamu ya muislamu wakati anaporudishiwa roho yake. Wanazuoni wengine wakasema kuwa Hadiyth hii haisemi wazi jambo hilo na kwamba hilo sio maalum kwa yule anayemtolea salamu karibu na kaburi lake. Bali udhahiri wa Hadiyth imekusanya waislamu wote kwa jumla.

Imethibiti kutoka kwake (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam) kwamba amesema:

“Hakika miongoni mwa siku zenu bora ni siku ya ijumaa. Hivyo basi niswalieni kwa wingi. Kwani hakika ya swalah zenu ni zenye kuonyeshwa kwangu.” Wakasema: “Ee Mtume wa Allaah! Ni vipi utaonyeshwa swalah zetu ili umekwishateketea?” Akasema: “Allaah ameuharamishia udongo kula miili ya Mitume.”[2]

Ameipokea Abu Daawuud, an-Nasaa´iy na Ibn Maajah kwa cheni ya wapokezi nzuri.

Yametangulia maneno yake (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam) aliposema:

“Hakika Allaah anao Malaika wanaozunguka ambao wanafikisha salamu kutoka kwa Ummah wangu.”[3]

Hadiyth hii na nyenginezo zilizopokelewa zikiwa na maana kama hiyo zinajulisha ya kwamba yeye (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam) zinamfikia swalah na amani za wanaomswalia na kumtakia amani. Ndani yake hakuna kwamba anasikia. Kwa hivyo haifai kusema kwamba anasikia mambo hayo isipokuwa kwa dalili Swahiyh na ya wazi itayotegemewa. Hakika jambo hili na mengine mfano wake ni kwa mujibu wa dalili na hivyo maoni hayana nafasi. Allaah (Subhaanah) amesema:

فَإِن تَنَازَعْتُمْ فِي شَيْءٍ فَرُدُّوهُ إِلَى اللَّـهِ وَالرَّسُولِ إِن كُنتُمْ تُؤْمِنُونَ بِاللَّـهِ وَالْيَوْمِ الْآخِرِ ۚ ذَٰلِكَ خَيْرٌ وَأَحْسَنُ تَأْوِيلًا

”Mkizozana juu ya jambo, basi lirudisheni kwa Allaah na Mtume mkiwa mnamuamini Allaah na siku ya Mwisho. Hivyo ni bora na matokeo mazuri kabisa.”[4]

Tumelirudisha jambo hili katika Qur-aan tukufu na Sunnah Swahiyh na hatukupata yanayofahamisha juu ya kwamba swalah na amani za wanaomswalia zinamfikia (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam). Kilichopo katika Sunnah ni dalili juu ya kwamba yanamfikia. Katika baadhi yake zimesema wazi ya kwamba zinawafikia Malaika.

Ama kusema kwamba (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam) anawaona waislamu ni jambo lisilokuwa na msingi. Aidha hakuna ndani ya Aayah na Hadiyth yanayofahamisha jambo hilo. Ni kama ambavo (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam) hazijui hali za walimwengu na yale yanayozuka kutoka kwao. Kwa sababu maiti yamekwishakatika mafungamano yake na watu wa ulimwenguni na utambuzi wa hali zao, kama zilivyokwishatangulia dalili juu ya hayo. Yale yanayosimuliwa kuhusu maudhui haya katika simulizi, ndoto na mengineyo yanayosemwa na baadhi ya Suufiyyah juu ya kuhudhuria kwake (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam) kati yao na kuziona hali zao. Vivyo hivyo yale yanayotajwa na baadhi ya wale wanaosherehekea mazazi yake (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam) kuhusu kwamba anahudhuria kati yao, yote hayo hayana usahihi na wala haijuzu kuyategemea. Dalili ni zenye kufupika katika maneno ya Allaah (Subhaanah) na maneno ya Mtume Wake (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam) na maafikiano ya wanazuoni wakaguzi. Kuhusu maoni, ndoto, simulizi na vipimo ni mambo hayana nafasi katika maudhui haya na wala kusitegemewe chochote katika hayo katika kuthibitisha kitu katika yale tuliyotaja.

Swalah na amani zimwendee Mtume wetu Muhammad, kizazi chake na wale watakaomfuata kwa wema mpaka siku ya Malipo.

[1] Ahmad (1434) na Abu Daawuud (2041).

[2] Ahmad (15729), Abu Daawuud (1047), an-Nasaa´iy (1374) na Ibn Maajah (1085).

[3] Ahmad (4198) na an-Nasaa´iy (1282).

[4] 04:59

  • Mhusika: Imaam ´Abdul-´Aziyz bin ´Abdillaah bin Baaz
  • Mfasiri: Firqatunnajia.com
  • Marejeo: at-Tahdhiyr min Fitnat-il-Qubuur, uk. 58-61
  • Imechapishwa: 03/05/2022