3- Kuamini Vitabu: Ni Vitabu ambavo Allaah ameviteremsha juu ya Mitume kwa ajili ya kuwaongoza watu. Tunaamini kuwa ni maneno ya Allaah kikweli na tunaamini vile vilivyotajwa majina na Allaah na vile ambavyo havikutajwa majina na Allaah. Allaah ametutajia Tawraat, Injiyl, Qur-aan tukufu, sahifa za Ibraahiym na Muusa na az-Zabuur. Tunaviamini. Vilevile tunaamini vile ambavo Allaah hakututajia majina katika hivyo.

Imani ya kuamini Vitabu vilivyotangulia inakuwa ni imani kwa njia ya ujumla. Imani ya kuamini Qur-aan inakuwa ni imani kwa njia ya upambanuzi kwa kila kilichomo ndani yake. Kwa sababu hicho ndio Kitabu chetu na kimeteremshwa kwa Mtume wetu Muhammad (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam). Yule mwenye kupinga Aayah au herufi moja miongoni mwa herufi zake anakuwa ni kafiri na mwenye kuritadi nje ya Uislamu.

Vivyo hivyo yule mwenye kuamini sehemu ya Qur-aan na akakufuru sehemu nyingine ni kafiri. Kadhalika yule mwenye kuamini baadhi ya Vitabu na akakufuru baadhi nyingine ni kafiri. Ambaye atasema kuwa yeye anaamini Qur-aan na wala haamini Tawraat na Injiyl ni kafiri. Au akasema kuwa anaamini Tawraat na Injiyl na wala haamini az-Zabuur ambayo imeteremshwa kwa Daawuud (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam) ni kafiri. Amesema (Ta´ala):

وَآتَيْنَا دَاوُودَ زَبُورًا

“Tumempa Daawuud Zabuur.”[1]

Au akapinga sahifa za Ibraahiym ni kafiri. Kwa sababu ni mwenye kumkadhibisha Allaah (´Azza wa Jall) na Mitume Yake. Huyo ni kafiri kwa sababu amekanusha nguzo miongoni mwa nguzo za imani.

4- Kuwaamini Mitume: Inatakiwa kuwaamini Mitume wote kuanzia wa mwanzo wao mpaka wa mwisho wao. Wale ambao Allaah amewataja majina katika wao na wale ambao hawakuwataja majina. Tunatakiwa kuwaamini wote na kwamba ni Mitume wa Allaah kikweli ambao wamekuja kwa ujumbe na wakaufikisha kwa nyumati zao.

Yule mwenye kumkufuru Mtume mmoja peke yake basi amewakufuru Mitume wote. Amesema (Ta´ala):

إِنَّ الَّذِينَ يَكْفُرُونَ بِاللَّـهِ وَرُسُلِهِ وَيُرِيدُونَ أَن يُفَرِّقُوا بَيْنَ اللَّـهِ وَرُسُلِهِ وَيَقُولُونَ نُؤْمِنُ بِبَعْضٍ وَنَكْفُرُ بِبَعْضٍ وَيُرِيدُونَ أَن يَتَّخِذُوا بَيْنَ ذَٰلِكَ سَبِيلًا أُولَـٰئِكَ هُمُ الْكَافِرُونَ حَقًّا ۚ وَأَعْتَدْنَا لِلْكَافِرِينَ عَذَابًا مُّهِينًا وَالَّذِينَ آمَنُوا بِاللَّـهِ وَرُسُلِهِ وَلَمْ يُفَرِّقُوا بَيْنَ أَحَدٍ مِّنْهُمْ أُولَـٰئِكَ سَوْفَ يُؤْتِيهِمْ أُجُورَهُمْ ۗ وَكَانَ اللَّـهُ غَفُورًا رَّحِيمًا

“Hakika wale waliomkufuru Allaah na Mitume Wake na wanataka kufarikisha kati ya Allaah na Mitume Wake na wanasema: “Tunaamini baadhi [ya Mitume] na tunawakanusha wengine” na wanataka kuchukua njia iliyo baina ya hayo – hakika hao ndio makafiri wa kweli na tumewaandalia makafiri adhabu ya kutweza. Na wale waliomwamini Allaah na Mitume Yake na hawakufarikisha yeyote kati yao,basi  hao atawapa ujira wao na Allaah daima ni Mwenye kusamehe, Mwenye kurehemu.”[2]

Kumkufuru Nabii au Mtume mmoja ni kuwakufuru wote. Kwa ajili hiyo amesema:

كَذَّبَتْ قَوْمُ لُوطٍ الْمُرْسَلِينَ

“Watu wa Luutw waliwakadhibisha Mitume.”[3]

Pamoja na kwamba walimkufuru Nuuh peke yake. Kumkadhibisha kwao Nuuh peke yake wanazingatiwa wamewakufuru Mitume wengine.

Vivyo hivyo wale wenye kumkufuru ´Iysaa na Muhammad, kama wanavofanya mayahudi, au wakamkufuru Muhammad, kama wanavofanya manaswara, basi wanazingatiwa kuwa wamewakufuru wote. Ni lazima kuwaamini Mitume wote (Swalla Allaahu ´alayhim wa sallam) ambao Allaah ametutajia majina yao na wale ambao hakututajia majina yao. Allaah ametutajia baadhi yao kama ilivyotajwa katika Suurah “al-An´aam”:

وَتِلْكَ حُجَّتُنَا آتَيْنَاهَا إِبْرَاهِيمَ عَلَىٰ قَوْمِهِ ۚ نَرْفَعُ دَرَجَاتٍ مَّن نَّشَاءُ ۗ إِنَّ رَبَّكَ حَكِيمٌ عَلِيمٌ وَوَهَبْنَا لَهُ إِسْحَاقَ وَيَعْقُوبَ ۚ كُلًّا هَدَيْنَا ۚ وَنُوحًا هَدَيْنَا مِن قَبْلُ ۖ وَمِن ذُرِّيَّتِهِ دَاوُودَ وَسُلَيْمَانَ وَأَيُّوبَ وَيُوسُفَ وَمُوسَىٰ وَهَارُونَ ۚ وَكَذَٰلِكَ نَجْزِي الْمُحْسِنِينَ وَزَكَرِيَّا وَيَحْيَىٰ وَعِيسَىٰ وَإِلْيَاسَ ۖ كُلٌّ مِّنَ الصَّالِحِينَ وَإِسْمَاعِيلَ وَالْيَسَعَ وَيُونُسَ وَلُوطًا ۚ وَكُلًّا فَضَّلْنَا عَلَى الْعَالَمِينَ

“Na hiyo ndio hoja Yetu tuliyompa Ibraahiym juu ya watu wake.  Tunampandisha cheo tumtakaye. Hakika Mola wako ni Mwenye hekima, Mjuzi wa kila kiut. Na Tukamtunukia Ishaaq na Ya’quub – wote tuliwaongoza – na Nuuh tulimwongoza kabla na katika kizazi chake Daawuud na Sulaymaan na Ayyuub na Yuusuf na Musaa na Haaruun; na hivyo ndivyo tunavowalipa wenye kufanya ihsaan, na Zakariyyaa na Yahyaa na ‘Iysaa na Ilyaas – wote ni miongoni mwa waja wema, na Ismaa’iyl na al-Yasaa´ na Yuunus na Luutw – na wote tuliwafadhilisha juu ya walimwengu.”[4]

Katika Aayah hizi  na nyenginezo wametajwa baadhi yao. Kwa hivyo tunaamini wale ambao Allaah ametutajia majina katika wao na wale ambao hakututajia majina yao.

[1] 04:163

[2] 04:150-152

[3] 26:160

[4] 06:83-86

  • Mhusika: Imaam Swaalih bin Fawzaan al-Fawzaan
  • Mfasiri: Firqatunnajia.com
  • Marejeo: Sharh Thalaathat-il-Usuwl, uk. 213-215
  • Imechapishwa: 25/01/2021