1- Ibn Mas´uud amesema:

“Shikamaneni na elimu kabla haijanyakuliwa. Inanyakuliwa pindi wanachuoni wanapofariki. Mtawaona watu wanaosema kuwa wanalingania katika Kitabu cha Allaah ilihali wao wenyewe wamekipuuza. Shikamaneni na elimu. Hakika mmoja wenu hajui ni lini ataihitajia au ni lini itahitajika katika uwepo wake. Shikamaneni na elimu, tahadharini na Bid´ah na shikamaneni na ile dini ya kwanza.”

2- Ibn Mas´uud amesema:

“Elimu sio kuwa na mapokezi mengi. Elimu ni kuwa na uchaji Allaah.”

3- Maalik amesema:

“Elimu sio kuwa na mapokezi mengi. Elimu ni kuwa na uchaji Allaah.”

4- Ni wajibu kwa aliye na busara kujiepusha na vitu vyote vya kidunia vinavyoweza kuichafua elimu yake. Kadhalika anatakiwa kuitendea kazi elimu kadri na uwezo wake hata kama itakuwa moja ya ishirini ya Hadiyth. Katika hali hii anakuwa kama ambaye katoa zakaah ya elimu. Yule asiyeweza kutendea kazi elimu asishindwe vilevile kuihifadhi.

5- Wahb bin Munabbih amesema:

“Allaah kamwe haitoi akili ya mtu ambaye anatafuta elimu kwa ajili ya haki na Sunnah.”

6- al-Mu´tmair bin Sulaymaan amesema:

“Baba yangu aliniandikia barua pindi nilipokuwa Kuufah. Kwenye barua hiyo kulikuwa kumeandikwa: “Nunua karatasi na uandike elimu. Mali itaisha na elimu itabaki.”

7- Kusafiri sana na kuiacha familia na mji kwa ajili ya kutafuta elimu pasi na kuitendea kazi wala kuihifadhi sio katika sifa za wenye busara. Kitu bora mtu anaweza kufanya katika hali hii ni kuwa na mwelekeo mzuri na hima yenye nguvu pamoja na kujiepusha na maasi.

8- Wakiy´ amesema:

“Acha kutendea maasi ili uweze kuhifadhi.”

9- Mwenye busara hafanyi bidii kwa kitu kisicholeta manufaa duniani na Aakhirah. Akiifikia elimu basi asiifanyie ubakhili wa kufundisha. Baraka ya kwanza ya elimu ni kufundisha. Sikumwona yeyote anayeifanyia ubakhili elimu yake isipokuwa vilevile hakukunufaishwa kwa elimu yake. Kama ambavyo hakuna manufaa yoyote kwa maji yaliyo chini ya ardhi mpaka pale yatapoanza kuchomoza kadhalika hakuna manufaa yoyote kwa elimu mpaka pale itapoenezwa na kufundishwa.

10- Abuud-Dardaa´ amesema:

“Mtu ima ni mwanachuoni au mwenye kujifunza. Hakuna kheri mbali na hao wawili.”

  • Mhusika: Imaam Muhammad bin Hibbaan al-Bustiy
  • Mfasiri: Firqatunnajia.com
  • Marejeo: Rawdhat-ul-´Uqalaa’ wa Nuzhat-ul-Fudhwalaa’, uk. 37-41
  • Imechapishwa: 12/11/2016