Katika kumuamini Allaah inatakiwa vilevile kuamini majina Yake mazuri na sifa Zake kuu zilizothibiti katika Qur-aan na Sunnah. Mtu anatakiwa afanye hivo bila ya kupotosha, kukanusha, kuziwekea namna na kuzifananisha. Bali ni wajibu kuyapitisha kama yalivyokuja bila ya kuyafanyia namna pamoja na kuamini ile maana tukufu iliyofahamishwa nayo ambayo ni sifa ya Allaah (Subhaanahu wa Ta´ala). Ni wajibu kumsifu nazo kwa njia inayolingana Naye. Inatakiwa kufanya hivo pasi na kumshabihisha na viumbe Wake kwenye chochote katika hayo. Amesema (Ta´ala):

لَيْسَ كَمِثْلِهِ شَيْءٌ ۖ وَهُوَ السَّمِيعُ الْبَصِيرُ

“Hakuna chochote kinachofanana Naye – Naye ni Mwenye kusikia, Mwenye kuona.” (42:11)

فَلَا تَضْرِبُوا لِلَّـهِ الْأَمْثَالَ ۚ إِنَّ اللَّـهَ يَعْلَمُ وَأَنتُمْ لَا تَعْلَمُونَ

“Basi msimpigie Allaah mifano. Hakika Allaah anajua nanyi hamjui.” (16:74)

Hii ndio ´Aqiydah ya Ahl-us-Sunnah wal-Jamaa´ah kuanzia kwa Maswahabah wa Mtume wa Allaah (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam) na wale waliowafuata kwa wema. Nayo ndio iliyonukuliwa na Imaam Abul-Hasan al-Ash´ariy (Rahimahu Allaah) katika kitabu “al-Maqaalaat ´an Aswhaab-il-Hadiyth wa Ahl-is-Sunnah”. Imenukuliwa vilevile na wanachuoni na watu wa imani wengine.

al-Awzaa´iy (Rahimahu Allaah) amesema: “az-Zuhriy na Mak-huul waliulizwa kuhusu Aayah za sifa za Allaah ambapo wakasema:

“Zipitishe kama zilivyokuja.”

al-Waliyd bin Muslim (Rahimahu Allaah) amesema: “Maalik, al-Awzaa´iy, al-Layth bin Sa´d na Suufyaan ath-Thawriy waliulizwa kuhusu Aayah zinazozungumzia sifa za Allaah ambapo wote wakasema:

“Zipitishe kama zilivyokuja pasi na kuzifanyia namna.”

al-Awzaa´iy (Rahimahu Allaah) amesema:

“Tulikuwa tukisema, na wanafunzi wa Maswahabah wamejaa, ya kwamba Allaah (Subhaanah) amelingana juu ya ´Arshi” na tukiamini vilevile sifa zilizothibiti katika Sunnah.””

Pindi Rabiy´ah bin Abiy ´Abdir-Rahmaan, ambaye ni mwalimu wa Maalik (Rahimahumaa Allaah), alipoulizwa kuhusu kulingana alisema:

“Kulingana kunajulikana. Namna haitambuliki. Ujumbe ni wenye kutoka kwa Allaah. Ni juu ya Mtume kufikisha kuliko wazi. Ni juu yetu kusadikisha.”

Wakati Imaam Maalik (Rahimahu Allaah) alipoulizwa kuhusu hilo alisema:

“Kulingana kunajulikana. Namna haijulikani. Kuamini hilo ni wajibu. Kuulizia hilo ni Bid´ah.” Baada ya hapo alimwambia yule muulizaji:

“Mimi sikuoni wewe isipokuwa ni mtu muovu.”

Halafu akaamrisha atolewe nje.

Maana kama hii imepokelewa kutoka kwa mama wa waumini Umm Salamah (Radhiya Allaahu ´anhaa).

Imaam Abu ´Abdir-Rahmaan bin al-Mubaarak (Rahimahu Allaah) amesema:

“Tunamtambua Mola wetu (Subhaanah) ya kwamba yuko juu ya mbingu, juu ya ´Arshi na ametengana na viumbe Wake.”

Maneno ya maimamu kuhusiana na mada hii ni mengi sana. Hatuwezi kuyanukuu yote katika muhadhara huu. Anayetaka kusoma mengi katika hayo basi arejee yale yaliyoandikwa na wanachuoni wa Sunnah katika mlango huu. Mfano wa kitabu “as-Sunnah” cha ´Abdullaah bin Imaam Ahmad, “Kitaab-ut-Tawhiyd” cha Imaam mtukufu Muhammad bin Khuzaymah, “as-Sunnah” cha Abul-Qaasim al-Laalakaa´iy at-Twabariy, “as-Sunah” cha Abu Bakr bin Abiy ´Aaswim, “al-Hamawiyyah” cha Shaykh-ul-Islaam Ibn Taymiyyah ambacho ni jibu kubwa na lililo na faida nyingi. Ndani yake ameweka wazi (Rahimahu Allaah) ´Aqiydah ya Ahl-us-Sunnah na humo vilevile amenukuu maneno yao mengi na dalili za Kishari´ah na za kiakili juu ya usahihi wa yale wanayoamini Ahl-us-Sunnah na ubatilifu wa yale waliyosema wapinzani wao. Vilevile inahusiana na kitabu chake kwa jina “at-Tadmuriyyah” ambapo ndani yake amekipanua na amebainisha ´Aqiydah ya Ahl-us-Sunnah wal-Jamaa´ah kwa kutumia dalili za kinakili na za kiakili na wakati huo huo kuwaraddi wenye kwenda kinyume. Ameidhihirisha haki na kuiponda batili. Hilo linatambulika na kila mwanachuoni mwenye kuvisoma kwa nia njema hali ya kuwa ni mwenye kukusudia kuijua haki. Kila yule mwenye kwenda kinyume na Ahl-us-Sunnah katika yale wanayoitakidi katika mlango wa majina na sifa za Allaah ni lazima atumbukie katika kuzikhalifu dalili za kinukuu na za kiakili pamoja vilevile na kujigonga kwa wazi katika yale yote atayoyathibitisha na kuyakanusha.

Kuhusu Ahl-us-Sunnah wal-Jamaa´ah wanamthibitishia Allaah (Subhaanahu wa Ta´ala) yale aliyojithibitishia Mwenyewe katika Qur-aan au yale aliyothibitishiwa na Mtume Wake Muhammad (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam) katika Sunnah Swahiyh. Uthibitishaji huu unafanyika bila ya ufananishaji na vilevile anatakaswa (Subhaanah) kushabihiana na viumbe Wake ambapo inakuwa ni utakasaji ulio mbali na ukanushaji. Kwa ajili hiyo wakafuzu kwa usalama kutokamana na kujigonga na wakazifanyia kazi dalili zote. Huu ndio mwenendo wa Allaah. Ambaye anashikamana na haki aliyomtuma nayo Mtume Wake, akatumia juhudi yake katika hilo na akamtakasia nia Allaah katika kuitafuta humuwafikisha katika haki na humfanya hoja yake ikashinda. Amesema (Ta´ala):

بَلْ نَقْذِفُ بِالْحَقِّ عَلَى الْبَاطِلِ فَيَدْمَغُهُ فَإِذَا هُوَ زَاهِقٌ

“Bali Tunavurumisha haki dhidi ya batili inaivunja; tahamaki [batili] inatoweka.” (21:18)

وَلَا يَأْتُونَكَ بِمَثَلٍ إِلَّا جِئْنَاكَ بِالْحَقِّ وَأَحْسَنَ تَفْسِيرًا

“Wala hawakujii kwa mfano wowote isipokuwa Tunakuletea haki na tafsiri nzuri kabisa.” (25:33)

Haafidhw Ibn Kathiyr (Rahimahu Allaah) amesema maneno mazuri katika Tafsiyr yake inayojulikana kuhusiana na maneno ya Allaah:

إِنَّ رَبَّكُمُ اللَّـهُ الَّذِي خَلَقَ السَّمَاوَاتِ وَالْأَرْضَ فِي سِتَّةِ أَيَّامٍ ثُمَّ اسْتَوَىٰ عَلَى الْعَرْشِ

“Hakika Mola wenu ni Allaah ambaye ameumba mbingu na ardhi katika siku sita kisha akalingana juu ya ´Arshi.” (07:54)

Niyatanukuu hapa kutokana na ukubwa wa faida yake. Amesema (Rahimahu Allaah) yafuatayo:

“Watu hapa wana maoni mengi sana. Hapa sio mahala pa kuyajadili. Mahala hapa tutasimulia ´Aqiydah ya Sala; Maalik, al-Awzaa´iy, ath-Thawriy, al-Layth bin Sa´d, ash-Shaafi´iy, Ahmad, Ishaaq bin Raahuuyah na maimamu wengine wa waislamu wa kale na waliokuja baadaye. Nayo ni kuyapitisha kama yalivyokuja pasi na kuyafanyia namna, kuyashabihisha, wala kuyakanusha. Inavyoonekana kitu kinachokuja kwa haraka kwenye akili ya wale wenye kuzifananisha sifa za Allaah na za viumbe Wake ni kumkanushia nayo Allaah. Hakika Allaah hafanani na chochote katika viumbe Wake. Hakuna kitu kinachofanana Naye – Naye ni Mwenye kusikia, Mwenye kuona. Mambo yalivyo ni kama walivyosema maimamu, ambapo mmoja wao ni Na´iym bin Hammaad al-Khuzaa´iy, ambaye ni mwalimu wa al-Bukhaariy, aliyesema:

“Mwenye kumshabihisha Allaah na viumbe Wake anakufuru. Anayemkanushia Allaah yale aliyojisifia Mwenyewe anakufuru. Hakuna katika yale Allaah aliyojithibitishia Mwenyewe na Mtume Wake ushabihishaji.”

Atayemthibitishia Allaah (Ta´ala) yale yaliyothibiti katika Aayah zilizo wazi na maelezo Swahiyh kwa njia inayolingana na utukufu wa Allaah na wakati huohuo akamkanushia Allaah (Ta´ala) mapungufu, basi amefuata njia ya uongofu.”

  • Mhusika: Imaam ´Abdul-´Aziyz bin ´Abdillaah bin Baaz
  • Mfasiri: Firqatunnajia.com
  • Marejeo: al-´Aqiydah as-Swahiyhah wa maa yudhwaadduhaa, uk. 05-07
  • Imechapishwa: 30/05/2023