04. Sababu ya sisi kuthibitisha sifa hizi

[6] Allaah ni Mmoja asiyefanana na chochote. Hatuzifananishi sifa Zake za sifa za viumbe na wala hatuzifanyii namna sifa Zake. Allaah yuko kinyume kabisa na vile ambavyo akili ya mtu inavofikiria.

Yuko hai kwa uhai, ni mjuzi kwa ujuzi, ni muweza kwa uwezo, ni misikivu kwa usikizi, ni muoni kwa uoni, ni mwenye kuzungumza kwa maneno, mwenye kutaka kwa utashi, mwenye kuamrisha kwa amri, mwenye kukataza kwa makatazo.

Tunathibitisha kwamba amemuumba Aadam kwa mkono Wake kutokana na maneno Yake (Ta´ala):

مَا مَنَعَكَ أَن تَسْجُدَ لِمَا خَلَقْتُ بِيَدَيَّ

”Kipi kilichokuzuia usimsujudie Niliyemuumba kwa mikono Yangu?”[1]

بَلْ يَدَاهُ مَبْسُوطَتَانِ

”Bali mikono Yake imefumbuliwa.”[2]

Kwamba ana mkono wa kuume, kutokana na maneno Yake (Subhaanah):

وَالسَّمَاوَاتُ مَطْوِيَّاتٌ بِيَمِينِهِ

”Mbingu zitakunjwa mkononi mwake mwa kuume.”[3]

Kwamba ana uso kutokana na maneno Yake:

كُلُّ شَيْءٍ هَالِكٌ إِلَّا وَجْهَهُ

“Kila kitu ni chenye kuhiliki isipokuwa uso Wake.”[4]

وَيَبْقَىٰ وَجْهُ رَبِّكَ ذُو الْجَلَالِ وَالْإِكْرَامِ

”Utabakia uso wa Mola Wako wenye utukufu na ukarimu.”[5]

Kwamba ana unyayo kutokana na maneno ya Mtume (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam):

”Mpaka pale Mola wako ataweka unyayo Wake juu yake ambapo utasema: ”Tosha, tosha.”[6]

Bi maana juu ya Moto. Ameipokea Ahmad, al-Bukhaariy, Muslim, Abu ´Iysaa at-Tirmidhiy na wengineo.

Kila usiku Anashuka katika mbingu ya chini ya dunia kutokana na maneno ya Mtume wa Allaah (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam):

“Mola wetu anashuka katika mbingu ya chini ya dunia pale kunapobaki theluthi ya mwisho ya usiku.”

Tamko hili ni la al-Bukhaariy. Hadiyth hii imepokelewa na Ahmad, Maalik, al-Bukhaariy, Muslim, Abu ´Iysaa at-Tirmidhiy, Abu Daawuud, Ibn Khuzaymah, ad-Daaraqutwniyna maimamu wengine wa Kiislamu.

Anamcheka mja Wake muumini kutokana na maneno ya Mtume wa Allaah (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam):

”Allaah (Ta´ala) anawacheka watu wawili. Mmoja amemuua mwengine na wote wawili wanaingia Peponi.” Wakasema: “Vipi?” Akasema: “Mmoja amepigana katika njia ya Allaah (´Azza wa Jall) ambapo akauawa shahidi. Kisha Allaah akamsamehe yule muuaji ambaye aliingia katika Uislamu. Halafu akapigana katika njia ya Allaah (´Azza wa Jall) ambapo akauawa shahidi.”[7]

Ameipokea al-Bukhaariy na wengineo.

[1] 38:75

[2] 05:64

[3] 39:67

[4] 28:88

[5] 55:27

[6] al-Bukhaariy (4848) na Muslim (2846)

[7]al-Bukhaariy (2826) na Muslim (1890).

  • Mhusika: Imaam Abul-Husayn Muhammad bin Abiy Ya´laa al-Hanbaliy
  • Mfasiri: Firqatunnajia.com
  • Marejeo: Kitaab-ul-I´tiqaad, uk. 25-26
  • Imechapishwa: 20/02/2019