Swali: Sisi tuko na Mashaykh wa Suufiyyah ambao wanatilia umuhimu wa kutengeneza makuba na makaburi. Watu wanaamini juu yao wema na baraka. Ikiwa jambo hili halikuwekwa katika Shari´ah basi ni zipi nasaha zako kwao na wao ni wenye kuigwa kwa mtazamo wa kundi kubwa la watu. Tupe faida Allaah akubariki?

Jibu: Nasaha kwa wanazuoni wa Suufiyyah na wengineo ni wachukue yale yenye kufahamishwa na Qur-aan na Sunnah na wawafunze watu mambo hayo. Wajihadhari kuwafuata waliokuwa kabla yao katika yanayokwenda kinyume na hayo. Dini sio kwa kuwafuata kichwa mchunga Mashaykh wala wengineo. Hakika si venginevyo dini ni yale yanayochukuliwa kutoka ndani ya Qur-aan na Sunnah na yale waliyoafikiana wanazuoni katika Maswahabah (Radhiya Allaahu ´anhum) na wale waliowafuata kwa wema. Namna hii ndivo inavyochukuliwa dini na si kwa kuwafuata kibubusa hawa na wale.

Sunnah Swahiyh kutoka kwa Mtume wa Allaah (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam) imefahamisha ya kwamba haijuzu kuyajengea makaburi, kuijengea misikiti, makuba wala jengo lolote juu yake. Yote hayo ni haramu kwa andiko la Mtume (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam). al-Bukhaariy na Muslim wamepokea kupitia kwa ´Aaishah (Radhiya Allaahu ´anhaa) ambaye ameeleza kwamba Mtume wa Allaah (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam) amesema:

”Allaah awalaani mayahudi na manaswara. Wameyafanya makaburi ya Mitume wao kuwa ni mahali pa kuswalia.”

Amesema (Radhiya Allaahu ´anhaa):

“Anatahadharisha waliyoyafanya.”[1]

al-Bukhaariy na Muslim wamepokea kupitia kwa Umm Salamah na Umm Habiybah (Radhiya Allaahu ´anhumaa) ya kwamba walimtajia Mtume (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam) kanisa waliloliona Habashah na namna yalivyokuwa na mapicha. Akasema (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam):

“Hao ndio wale ambao wanapofiwa na mtu mwema, basi hujenga juu ya kaburi lake msikiti na huchora ndani yake picha hiyo. Hao ndio viumbe waovu kabisa mbele ya Allaah.”[2]

Akaeleza (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam) ya kwamba wale wanaojenga misikiti juu ya makaburi ndio viumbe waovu kabisa. Vivyo hivyo wale wenye kuyaweka mapicha kwa sababu zinaita katika shirki. Kwa sababu wajinga wakiona misikiti na makuba juu yake basi watamtukuza yule aliyemo ndani, wakamtaka uokozi, wakamwekea nadhiri na wakamwomba badala ya Allaah na wakaomba kutoka kwao msaada. Yote haya ndio shirki kubwa.

Muslim amepokea katika “as-Swahiyh” yake kupitia kwa Jundub bin ´Abdillaah (Radhiya Allaahu ´anh) ambaye amesimulia kwamba amemsikia Mtume (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam) kabla ya kufa kwake kwa siku tano akisema:

“Hakika Allaah amenifanya kuwa kipenzi Wake wa karibu kama alivyomfanya Ibraahiym kuwa kipenzi Wake wa karibu. Na lau ningemchukua yeyote katika Ummah wangu kuwa kipenzi wangu wa karibu, basi ningelimfanya Abu Bakr kuwa kipenzi  wangu wa karibu. Tanabahini! Hakika wale waliokuwa kabla yenu walikuwa wakiyafanya makaburi ya Mitume wao kuwa mahali pa kuswalia. Tanabahini! Msiyafanye makaburi kuwa mahali pa kuswalia. Hakika mimi nawakatazeni na hilo.”[3]

Namna hii ndivo alivoipokea Muslim katika “as-Swahiyh” yake.

Hayo yakafahamisha ubora wa as-Swiddiyq (Radhiya Allaahu ´anh), kwamba ndio Swahabah bora na mbora wao na kwamba kama ingelifaa kwa Mtume (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam) kumfanya mtu awe kipenzi mwandani basi angelimfanya yeye (Radhiya Allaahu ´anh) kuwa kipenzi mwandani. Lakini Allaah (Jalla wa ´Alaa) amemkataza kutokamana na hilo ili yatakasike zaidi mapenzi yake kwa Mola Wake (Subhaanahu wa Ta´ala). Kwani mapenzi ya ndani kabisa (الخلة) yako juu zaidi ya mapenzi ya kawaida.

Vilevile katika Hadiyth kuna dalili juu ya kuharamika kujenga juu ya makaburi, kujenga misikiti juu yake na kumsema vibaya yule mwenye kufanya hivo kwa njia tatu:

1 – Kusimangwa yule mwenye kufanya hivo.

2 – Maneno yake (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam):

“Msiyafanye makaburi kuwa mahali pa kuswalia.”

3 – Maneno yake (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam):

“Hakika mimi nawakatazeni na hilo.”

Kwa hiyo akakataza kuyajengea makaburi kwa njia hizi tatu. Amesema (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam):

“Hakika wale waliokuwa kabla yenu walikuwa wakiyafanya makaburi ya Mitume wao kuwa mahali pa kuswalia.”

Kisha akasema:

“Tanabahini! Msiyafanye makaburi kuwa mahali pa kuswalia.”

Bi maana msiwaige.

“Hakika mimi nawakatazeni na hilo.”

Haya matahadharisho ya wazi ya kujenga juu ya makaburi na kuyafanya kuwa ni mahali pa kuswalia. Sababu na hekima ya hilo ni yale yaliyosemwa na wanazuoni ya kwamba ni njia inayopelekea katika shirki kubwa, kuabudiwa kwa waliyomo ndani ya makaburi, kuwatekelezea maombi, nadhiri, kuombwa uokozi wa haraka, kuwachinjia na kuomba msaada kutoka kwao. Hali ndivo ilivyo hivi sasa katika nchi nyingi huko Suudan kwao na muulizaji, Misri, Shaam na ´Iraaq.

Katika nchi nyingi utaona anakuja mtu wa kawaida mjinga ambaye anasimama mbele ya kaburi la mtu ambaye alikuwa anamjua na anamuomba msaada na uokozi. Hayo yanatokea katika kaburi la al-Badawiy, al-Husayn, bibi Nafiysah, Zaynab na wengineo huko Misri, kama inavotokea huko kwenu Suudan ambapo katika makaburi mengi, kama inavotokea katika nchi nyenginezo, kama inavotokea katika baadhi ya mahujaji wajinga kwenye kaburi la Mtume (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam) Madiynah, katika makaburi ya watu wa al-Baqiy´, katika kaburi la Khadiyjah Makkah na makaburi mengine. Mambo haya hutokea kwa wajinga. Wanahitaji kufunzwa, kubainishiwa na wanazuoni kuwatilia umuhimu.

Kwa hiyo ni lazima kwa wanazuoni wa Shari´ah wote – ni mamoja wale wanaonasibishiwa Taswawwuf na wengineo – kumcha Allaah, wawanasihi waja wa Allaah, wawafunze dini yao, kuwatahadharisha kuyajengea makaburi, kujenga misikiti juu ya makaburi au makuba na aina nyenginezo za majengo. Aidha wawatahadharishe kuwaomba wafu na kuwataka msaada wafu. Du´aa ni ´ibaadah ya Allaah pekee. Kwa sababu Allaah (Subhaanah) amesema:

فَلَا تَدْعُوا مَعَ اللَّـهِ أَحَدًا

“Hivyo basi msiombe yeyote pamoja na Allaah.”[4]

وَلَا تَدْعُ مِن دُونِ اللَّـهِ مَا لَا يَنفَعُكَ وَلَا يَضُرُّكَ ۖ فَإِن فَعَلْتَ فَإِنَّكَ إِذًا مِّنَ الظَّالِمِينَ

“Wala usiombe badala ya Allaah asiyekufaa [ukimwabudu] na wala asiyekudhuru [usipomwabudu]. Na ukifanya hivyo, basi hakika utakuwa miongoni mwa madhalimu.”[5]

Bi maana miongoni mwa washirikina.

Vilevile amesema (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam):

“Du´aa ndio ´ibaadah.”[6]

Mtume (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam) amesema:

“Unapoomba basi mwombe Allaah na upotaka msaada basi mtake msaada Allaah.”[7]

Maiti yamekatika matendo yake kutoka kwa watu. Kwa hiyo ni mwenye haja ya kuombewa du´aa, kuombewa msamaha na kuombewa rehema na si yeye kuombwa badala ya Allaah. Mtume (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam) amesema:

“Anapofariki mwanadamu basi matendo yake hukatika isipokuwa mambo matatu; swadaqah yenye kuendelea, elimu ambayo watu wananufaika nayo au mtoto mwema mwenye kumuombea du´aa.”[8]

Ni vipi basi ataombwa badala ya Allaah? Vivyo hivyo masanamu, miti, mawe, jua, mwezi na nyota vyote haviombwi badala ya Allaah na wala haviombwi uokozi. Hali kadhalika waliyomo ndani ya makaburi – ijapo watakuwa ni Mitume na waja wema – Malaika na majini hawaombwi pamoja na Allaah. Allaah (Subhaanah) amesema:

وَلَا يَحْسَبَنَّ الَّذِينَ يَبْخَلُونَ بِمَا آتَاهُمُ اللَّـهُ مِن فَضْلِهِ هُوَ خَيْرًا لَّهُم ۖبَلْ هُوَ شَرٌّ لَّهُمْ ۖ سَيُطَوَّقُونَ مَا بَخِلُوا بِهِ يَوْمَ الْقِيَامَةِ ۗ وَلِلَّـهِ مِيرَاثُ السَّمَاوَاتِ وَالْأَرْضِ ۗ وَاللَّـهُ بِمَا تَعْمَلُونَ خَبِيرٌ

“Wala wasidhani kabisa wale wanaofanya ubakhili kwa yale Aliyowapa Allaah katika fadhila Zake kwamba hayo ni kheri kwao, bali ni shari kwao. Watafungwa kongwa yale waliyoyafanyia ubakhili Siku ya Qiyaamah. Na ni Wake Allaah Pekee urithi wa mbingu na ardhi. Na Allaah ni Mwenye khabari za ndani kwa yale myafanyayo.”

Amefanya kule kuwafanya Malaika na Mitume kuwa waungu kwa njia ya kuwaomba na kuwataka uokozi ni ukafiri. Isitoshe Allaah (Subhaanahu wa Ta´ala) haamrishi mambo hayo. Hadiyth ya Jaabir iliopokelewa na Muslim amesema (Radhiya Allaahu ´anh):

“Mtume wa Allaah (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam) amekataza kulitia chokaa kaburi, kukaa juu yake na kujenga juu yake.”[9]

Hayo ni kwa sababu ni njia inayopelekea katika shirki. Kujenga juu yake, kuyatia chokaa, kuyavisha mavazi na kuyajengea jengo yote haya ni njia inayopelekea kuyaadhimisha, kuchupa mpaka kwayo na kuwaomba wenye nayo. Kuhusu kukaa juu yake ni kuyatweza, jambo ambalo halijuzu. Kwa hiyo mtu asiketi juu yake. Ni yenye kuheshimiwa na hayatwezwi. Mtu asiketi, asikojoe, asinye juu yake, asiyaegemee na wala asiyakanyage. Mambo haya yamekatazwa kwa sababu ya kumuheshimiwa muislamu. Yote haya yamekatazwa. Muislamu aliyekufa hatwezwi na wala haombwi badala ya Allaah. Hakuchupwi mpaka juu yake ambapo akaombwa badala ya Allaah kama ambavo hadharauliwi ambapo akakanyagwa, akatupiwa taka, akakojolewa na uchafu. Si haya ya mwanzo wala haya ya mwisho. Shari´ah imekuja ikiwa na ukatikati; imekuja ikiwa ni yenye kuyaheshimu makaburi, kuwaombea wenye nayo msamaha na rehema na kuwatembelea kwa ajili ya kuwaombea du´aa, msamaha na sambamba na hayo imekuja ikiwa ni yenye kukataza kuwakera kwa kuwatupia uchafu, taka, kuwakojolea, kuyakalia na mengineyo.

Miongoni mwa mambo hayo ni yale yaliyokuja katika Hadiyth Swahiyh ambapo Mtume (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam) amesema:

“Msikae juu ya makaburi  na wala msiswali kuyaelekea.”

Haijuzu kuyafanya makaburi kuwa Qiblah na wala kuketi juu yake. Kwa hiyo Shari´ah kamilifu na tukufu ikawa imekusanya kati ya mambo mawili:

1 – Kuharamisha kuchupa mpaka kwa watu waliyomo ndani ya makaburi na kuwaomba badala ya Allaah, kuwataka uokozi, kuwawekea nadhiri na mfano wa matendo kama hayo. Matendo yote haya ni shirki kubwa.

2 – Kuwakera, kuwadharau, kukaa juu ya makaburi yao, kuyakanyaga, kuyaegemea au kuweka taka juu yake. Yote haya yamekatazwa.

Kwa haya muumini na yule anayetafuta haki anapata kutambua kuwa Shari´ah imekuja kwa ukati na kati; si kwa kushirikisha, kukera wala kudharau. Mtume na mtu mwengine mwema anaombewa du´aa, anaombewa msamaha na anatolewa salamu wakati wa kumtembelea. Kuhusu kumwomba badala ya Allaah haifai. Kwa hiyo haitakiwi kusema ´Ee bwana nisaidie haraka haraka´, ninusuru, mponyeshe mgonjwa wangu au nasumbuliwa na jambo fulani. Mambo haya anaombwa Allaah. Vilevile hadharauliwi kwa njia ya kwamba kukawekwa taka juu ya kaburi lake, likakanyagwa au likawekwa taka. Si haya ya mwanzo wala haya ya mwisho.

Kuhusu aliye hai hapana neno kusaidizana naye kwa sababu yuko na matendo katika yale yanayofaa katika zile sababu ambazo ni zenye kuhisiwa. Amesema (Ta´ala):

فَاسْتَغَاثَهُ الَّذِي مِن شِيعَتِهِ عَلَى الَّذِي مِنْ عَدُوِّهِ

“Akamsaidia yule ambaye katika kundi lake dhidi ya yule ambaye ni katika adui wake.”[10]

Katika kisa cha Muusa. Hakika Muusa ambaye alikuwa anaombwa msaada alikuwa hai. Yule mwana israaiyl alitaka msaada dhidi ya ambaye ni audi yake ambaye ni Qubtwiy. Vivyo hivyo mtu pamoja na ndugu zake na jamaa zake ambapo wanasaidizana katika mashamba yao, kukarabatika nyumba zao, kutengeneza nyumba zao na mambo mengine katika mahitaji yao. Husaidiana katika zile sababu zenye kuhisiwa na zenye kuwezekana. Katika hali hii hapana vibaya. Kadhalika kupitia njia ya simu, njia ya uandishi na njia ya faksi. Yote haya ni katika kusaidizana kwenye kuhisiwa katika mambo yanayowezekana. Lakini katika yanayohusiana na ´ibaadah haifai. Haifai kumwambia aliye hai au ambaye ameshakufa kwamba akuponyee mgonjwa wako au akurudishie kisichoko mbele yako kwa kuamini kwamba yuko na siri katika jambo hilo. Wala haitakikani kumwambia akunusuru dhidi ya maadui wetu kutokana na siri yake. Lakini kuomba nusura kutoka kwa aliye hai na muweza aliyeko mbele yako kutokana na zile sababu zenye kuhisiwa kama vile silaha na mkopo ni sawa. Vivyo hivyo hapana vibaya akamwendea daktari akamuomba amtibu. Lakini kumwambia amponye kwa sababu anaamini kuwa yuko na siri, kama inavotambulika kwa Suufiyyah na wengineo, ni ukafiri. Kwa sababu mtu hawezi kuendesha ulimwengu. Anaweza kufanya hivo katika yale mambo yenye kuhisiwa. Daktari anaendesha yale mambo yenye kuhisiwa kama vile dawa.

Vivyo hivyo mtu ambaye ni muweza na aliye hai anaendesha katika zile sababu zenye kuhisiwa, anaweza kukusaidia kwa mkono wake, anasimama nawe, anakukopa pesa, msaada wa ujenzi, anakupa spea za gari yako au akakusaidia kukufanyia uombezi mbele ya wawezao kukusaidia. Yote haya ni mambo yenye kuhisiwa na yasiyokuwa na neno. Wala hayaingii katika kuwaabudu wafu, kuwataka msaada wafu na mfano wa hayo.

Walinganizi wengi wa shirki hubabaisha kwa mambo haya. Mambo haya yako wazi na hayamchanganyi isipokuwa yule ambaye ni mjinga kabisa wa watu. Kushirikiana na waliohai ni kitu kinachofaa kwa sharti zake zinazotambulika. Kuwaomba, kuwataka uokozi na kuwawekea nadhiri wafu ni mambo yaliyokatazwa na yanayotambulika kwa wanazuoni na kwamba ni shirki kubwa kwa maafikiano ya wanazuoni. Hayana mzozo kati ya Maswahabah na wanazuoni waliokuja baada yao, waumini na watambuzi. Vivyo hivyo kujenga juu ya makaburi na kujenga misikiti juu ya makaburi na majengo ni maovu yanayotambulika kwa wanazuoni. Shari´ah imekuja kuyakataza. Kwa hiyo haifai mambo haya yakawachanganya wanazuoni.

Kwa hiyo ni lazima kwa wanazuoni kwa mara nyingine tena kumcha Allaah popote walipo, wawanasihi waja wa Allaah, wawafunze Shari´ah ya Allaah na wasimpake mafuta yeyote yule katika mambo hayo. Bali wanapaswa kumfunza kiongozi, mdogo na mkubwa. Vilevile watahadharishe yale aliyoharamisha Allaah na wawaelekeze katika yale aliyoyawekea Allaah Shari´ah. Haya ndio yanayowapasa wanazuoni popote watapokuwepo kupitia njia ya mazungumzo ya mdomo, njia ya uandishi, njia ya utunzi, njia ya Khutbah ya ijumaa, njia ya simu, njia ya faksi na nyenginezo za kisasa. Mtu anatakiwa kuzitumia katika kufikisha ulinganizi wa Allaah na kuwanasihi waja wa Allaah.

[1] al-Bukhaariy (436) na Muslim (529).

[2] al-Bukhaariy (427) na Muslim (528).

[3] Muslim (532).

[4] 72:18

[5] 10:106

[6] Ahmad (17919), Abu Daawuud (1479), at-Tirmidhiy (2969) na Ibn Maajah (3828).

[7] Ahmad (2758) na at-Tirmidhiy (2516).

[8] Muslim (1631).

[9] Muslim (970).

[10] 28:15

  • Mhusika: Imaam ´Abdul-´Aziyz bin ´Abdillaah bin Baaz
  • Mfasiri: Firqatunnajia.com
  • Marejeo: at-Tahdhiyr min Fitnat-il-Qubuur, uk. 4-14
  • Imechapishwa: 06/04/2022