Himdi zote ni Zake Allaah. Tunamhimidi Yeye, tunamtaka msaada na tunamuomba msamaha. Tunajikinga Kwake kutokana na shari ya nafsi zetu na matendo yetu maovu. Anayeongozwa na Allaah hakuna yeyote wa kumpoteza, na Anayepotezwa na Allaah hakuna yeyote wa kumuongoza.

Ninashuhudia ya kwamba hakuna mola mwenye kuabudiwa kwa haki isipokuwa Allaah Mmoja asiyekuwa na mshirika na ninashuhudia ya kwamba Muhammad ni mja Wake na ni Mtume Wake. Amma ba´d: Hakika Allaah (Tabaaraka wa Ta´ala) Ametuumba katika uhai huu kutokana na hekima kubwa – ambayo Anaipenda na Kuiridhia – nayo ni kumuabudu Yeye Mmoja asiyekuwa na mshirika. Allaah (Ta´ala) Amesema:

وَمَا خَلَقْتُ الْجِنَّ وَالْإِنسَ إِلَّا لِيَعْبُدُونِ

“Sikuumba majini na watu isipokuwa waniabudu.” (adh-Dhaariyaat 51:56)

Hivyo Allaah Akawatofautisha wanaadamu kutokana na viumbe wengine wote kwa kuwaneemesha akili, ambayo kwa akili hiyo wanaweza kumtambua Mola Wake. Kadhalika wanaweza kutofautisha kati ya yale yanayowanufaisha na yanayowadhuru. Kutokana na Rahmah za Allaah (Subhaanahu wa Ta´ala) kwa waja Wake hakuwaacha kuweza kutambua kati ya kheri na shari kwa kutegemea akili peke yake, bali Amewatumia Mtume na Akawateremshia Vitabu. Ndani yake mna maamrisho yote ambayo Allaah Ameamrisha, makatazo pamoja na hukumu Zake zote ambazo wanahitajia wanaadamu katika kufikia mafanikio duniani na Aakhirah.

Baada ya kutuma Mitume, hapakubaki hoja au udhuru wowote kwa yule aliyepotea au kupinda na Njia ya Allaah. Bali mtu sampuli hii anakuwa ni mwenye kustahiki kuadhibiwa. Allaah (Ta´ala) Amesema:

رُّسُلًا مُّبَشِّرِينَ وَمُنذِرِينَ لِئَلَّا يَكُونَ لِلنَّاسِ عَلَى اللَّـهِ حُجَّةٌ بَعْدَ الرُّسُلِ

“Mitume ni wabashiriaji na waonyaji ili pasikuweko kutoka kwa watu hoja yoyote juu ya Allaah baada ya kuletwa Mitume hao.” (an-Nisaa´ 04:165)

Allaah Amemalizia na kukamilisha ujumbe kwa Mtume wetu Muhammad (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam). Yeye ndiye Nabii wa mwisho na mbora wao na ameteremshiwa Kitabu bora. Hivyo Shari´ah yake ikawa ni kamilifu na nzuri zaidi katika Shari´ah. Hakufa kwa ajili ya kukutana na marafiki walioko juu kati ya Malaika, isipokuwa baada ya Allaah kukamilisha Dini na kutimiza neema. Haya Ameyasema Allaah (Ta´ala) katika Aayah iliyoteremshwa karibu kabla ya kufa kwake (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam), jambo ambalo lilikuwa siku ´Arafah katika Hajj ya kuaga:

الْيَوْمَ أَكْمَلْتُ لَكُمْ دِينَكُمْ وَأَتْمَمْتُ عَلَيْكُمْ نِعْمَتِي وَرَضِيتُ لَكُمُ الْإِسْلَامَ دِينًا

 “Leo nimekukamilishieni dini yenu na nimekutimizieni neema Yangu na nimekuridhieni Uislamu uwe dini yenu.” (al-Maaidah 05:04)

Hivyo hapakubaki nafasi kwa yeyote, pasina kujali ni nani, kuzusha katika Dini chochote au kuzidisha au kupunguza ndani yake. Kitu cha kwanza ambacho Mtume wa Allaah (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam) alichoanza kulingania ni Tawhiyd, ambayo ni ”nashuhudia ya kwamba hapana mola mwenye haki ya kuabudiwa isipokuwa Allaah na Muhammad ni Mtume wa Allaah”. Alibaki Makkah baada ya kutumwa miaka kumi na tatu akilingania katika neno hili ambalo ndio msingi wa dini na hakulingania katika kitu kingine. Kadhalika walilingania Mitume wengine katika neno hili na wakaanza kuwalingania watu wao kwa kusema:

اعْبُدُوا اللَّـهَ مَا لَكُم مِّنْ إِلَـٰهٍ غَيْرُهُ

“Enyi watu wangu! Mwabuduni Allaah, kwani hamna mwabudiwa wa haki mwingine asiyekuwa Yeye.” (al-A´araaf 07:59)

Kwa hivyo Tawhiyd ndio kitu muhimu sana ambacho Mitume walikuja nacho, lengo lao pamoja, nguzo ya msingi katika mambo yote waliyolingania, kitu ambacho walikuwa wamejengea juu yake na sababu ya wao kutumwa. Dalili ya hilo zinapatikana katika Aayah nyingi. Baadhi yake ni Kauli ya Allaah (Ta´ala):

وَلَقَدْ بَعَثْنَا فِي كُلِّ أُمَّةٍ رَّسُولًا أَنِ اعْبُدُوا اللَّـهَ وَاجْتَنِبُوا الطَّاغُوتَ ۖ فَمِنْهُم مَّنْ هَدَى اللَّـهُ وَمِنْهُم مَّنْ حَقَّتْ عَلَيْهِ الضَّلَالَةُ

“Hakika Tulituma katika kila ummah Mtume kwamba: “Mwabuduni Allaah na jiepusheni na Twaaghuut [waungu batili]. Basi miongoni mwao wako ambao Allaah amewaongoza na miongoni mwao wako ambao umethibiti kwake upotevu.” (an-Nahl 16:36)

لَقَدْ أَرْسَلْنَا نُوحًا إِلَىٰ قَوْمِهِ فَقَالَ يَا قَوْمِ اعْبُدُوا اللَّـهَ مَا لَكُم مِّنْ إِلَـٰهٍ غَيْرُهُ إِنِّي أَخَافُ عَلَيْكُمْ عَذَابَ يَوْمٍ عَظِيمٍ

“Hakika Tulimpeleka Nuuh kwa watu wake akasema: “Enyi watu wangu! Mwabuduni Allaah, kwani hakika nyinyi hamna mwabudiwa wa haki mwengine asiyekuwa Yeye. Hakika mimi nakucheleeni adhabu Siku kubwa mno.” (al-A´raaf 07:59)

وَإِلَىٰ عَادٍ أَخَاهُمْ هُودًا ۗ قَالَ يَا قَوْمِ اعْبُدُوا اللَّـهَ مَا لَكُم مِّنْ إِلَـٰهٍ غَيْرُهُ ۚ أَفَلَا تَتَّقُونَ

”Na kwa [watu wa] ‘Aad [Tuliwapelekea] kaka yao Huud. Akasema: ”Enyi watu wangu! Mwabuduni Allaah, kwani hakika nyinyi hamna mwabudiwa wa haki mwengine asiyekuwa Yeye. Je, basi hamtokuwa na taqwa?” (al-A´raaf 07:65)

وَإِلَىٰ ثَمُودَ أَخَاهُمْ صَالِحًا ۗ قَالَ يَا قَوْمِ اعْبُدُوا اللَّـهَ مَا لَكُم مِّنْ إِلَـٰهٍ غَيْرُهُ

”Na kwa [watu wa] Thamuud [Tuliwapelekea) kaka yao Swaalih. Akasema: ”Enyi watu wangu! Mwabuduni Allaah, kwani hakika nyinyi hamna mwabudiwa wa haki mwengine asiyekuwa Yeye.” (Huud 11:61)

وَإِلَىٰ مَدْيَنَ أَخَاهُمْ شُعَيْبًا ۗ قَالَ يَا قَوْمِ اعْبُدُوا اللَّـهَ مَا لَكُم مِّنْ إِلَـٰهٍ غَيْرُهُ

“Na kwa [watu wa] Madyan [Tuliwapelekea] kaka yao Shu’ayb.  Akasema: “Enyi watu wangu! Mwabuduni Allaah, kwani hakika nyinyi hamna mwabudiwa wa haki  mwengine asiyekuwa Yeye.” (Huud 11:84)

Na Aayah zengine nyingi ambazo zinaonyesha kuwa Tawhiyd ndio kitu cha kwanza ambacho Mitume walikuwa wakiwalingania watu wao, kwa sababu Tawhiyd ndio nguzo msingi wa Uislamu na ndio Dini ya Mitume na Manabii wote. Wakati ambapo msingi unakuwa thabiti, basi mtu anajengea juu yake mambo ya ´ibaadah na hukumu. Hii haina maana kwamba yule anayelingania katika Uislamu apuuze matawi mengine ya Uislamu, lakini katika mambo ambayo imeafikiwa juu yake ni kuwa matendo hayasihi wala hayakubaliwi muda wa kuwa ´Aqiydah ya mwenye matendo hayo si sahihi. Kama jinsi kwa mfano si sawa kwetu kujenga nyumba kabla ya kejenga msingi imara ambao itasimama juu yake. Vinginevyo nyumba itaporomoka na kuanguka. Hili linatiliwa nguvu khaswa kwa vile shirki – ambayo ni kinyume cha Tawhiyd – ndio dhambi na jarima kubwa kuliko dhambi zengine zote. Kwa ajili hiyo Allaah (Ta´ala) Ameeleza kwamba Hatomsamehe yule ambaye atakufa juu ya shirki. Allaah (Ta´ala) Amesema:

إِنَّ اللَّـهَ لَا يَغْفِرُ أَن يُشْرَكَ بِهِ وَيَغْفِرُ مَا دُونَ ذَٰلِكَ لِمَن يَشَاءُ

“Hakika Allaah hasamehi kushirikishwa lakini anasamehe yaliyo chini ya hayo kwa amtakae.” (an-Nisaa´ 04:48)

Kila dhambi ambayo imefanywa na mtu na wakati huohuo ikawa ni chini ya shirki na kufuru, kuna matarajio kwa Allaah Akamsamehe mtu huyu na dhambi yake na hivyo Akamuingiza Peponi maadamu amesalimika na shirki. Ama yule anayekufa katika shirki – hata kama atakuwa anadai Uislamu – kwa hakika mafikio yake ni Motoni – Allaah Atukinge nao.

Kwa ajili hiyo ni jambo la kilazima kwetu kuzinduka juu ya jambo hili kubwa, ili tuweze kuwalingania watu katika Tawhiyd, kuwatahadharisha na shirki na kulifanya hilo kuwa kichwa cha mambo tunayolingania kwayo.

Wakati Mtume wa Allaah (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam) alipomtuma Mu´aadh kwenda Yemen ili kuwalingania watu katika Uislamu, alimfunza ni vipi ataanza ulinganizi wake. Alimfunza kuanza na kitu ambacho ni muhimu zaidi na kuendelea mbele. Ibn ´Abbaas (Radhiya Allaahu ´anhumaa) amesema:

“Wakati Mtume wa Allaah (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam) alipomtuma Mu´aadh kwenda Yemen, alimwambia: “Hakika wewe unawaendea watu katika watu wa Kitabu. Hivyo basi, jambo la kwanza ambalo utawalingania kwalo iwe “Hapana mungu mwenye kuabudiwa kwa haki isipokuwa Allaah” – katika upokezi mwingine “… wampwekeshe Allaah”. Wakikutii katika hilo, wafunze ya kwamba Allaah Amefaradhisha juu yao Swalah tano kwa siku. Wakikutii katika hilo, wafunze ya kwamba Allaah Amefaradhisha juu yao Zakaah ambayo itachukuliwa kutoka kwa matajiri wao na kupewa mafukara wao. Wakikutii katika hilo, tahadhari na zile mali  zao nono na iogope du´aa ya mdhulumiwaji; kwani hakika hakuna baina yake na baina ya Allaah kizuizi.”[1]

Kinacholengwa katika Hadiyth hii, ni kwamba (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam) amemwelekeza Mu´aadh namna atavyolingania [watu katika Uislamu] na kwamba aanze kwa Tawhiyd kabla ya kila kitu. Baada ya wao kuingia katika Tawhiyd, ndipo atawalingania katika Shari´ah zingine, kwa kuanza kwa Swalah ambayo ndio kichwa cha ´ibaadah. Kwa ajili hiyo inatakiwa kwa kila yule anayelingania katika Uislamu amfanye Mtume wa Allaah (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam) kuwa ndio kiigizo chake chema.

Enyi ndugu! Litapojulikana hili, basi ni lazima kutambua ya kwamba kuna Da´wah angamizi ambazo zimesimama kati ya Waislamu na zinaitikisa na kuidhuru ´Aqiydah ndani ya nyoyo za Waislamu wengi. Wameichafua ´Aqiydah safi ya Kiislamu na imekuwa kwa kiasi kikubwa na kufikia kiasi cha khatari iliokuwa kubwa, wanawafarikisha Waislamu kuwa makundimakundi na mapotemapote. Maneno yake Mtume (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam) yamesadikika juu yao pale aliposema:

“Tanabahini! Hakika wale waliokuwa kabla yenu katika watu wa Kitabu waligawanyika makundi sabini na mbili. Hakika dini hii itagawanyika makundi sabini na tatu. Makundi sabini na mbili yataingia Motoni na limoja ndilo litaingia Peponi; nalo ni al-Jamaa´ah.”[2]

Hapana shaka kila pote katika mapote haya linadai kuwa lenyewe ndio kundi lililookoka, liko katika usawa na kwamba ndilo linalomfuata Mtume (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam) pasi na mengine. Pamoja na kwamba njia ya haki ni moja pekee na ndio inayoelekeza katika uokozi. Njia nyenginezo zote ni njia za upotevu zinazopelekea katika maangamivu. Ibn Mas´uud (Radhiya Allaahu ´anh) amesema:

“Mtume wa Allaah (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam) alipiga msitari kwa mkono wake na akasema: “Hii ndio njia ya Allaah ilionyooka.” Kisha akapiga misitari mingine kuliani na kushotoni na akasema: “Hizi ni njia zengine; hakuna njia yoyote katika hizo isipokuwa kuna Shaytwaan anayewaita watu kwayo.” Kisha akasoma:

وَأَنَّ هَـٰذَا صِرَاطِي مُسْتَقِيمًا فَاتَّبِعُوهُ ۖ وَلَا تَتَّبِعُوا السُّبُلَ فَتَفَرَّقَ بِكُمْ عَن سَبِيلِهِ ۚ ذَٰلِكُمْ وَصَّاكُم بِهِ لَعَلَّكُمْ تَتَّقُونَ

“Kwamba hii ni njia Yangu iliyonyooka, hivyo basi ifuateni na wala msifuate njia za vichochoro nyinginezo zitakufarikisheni na njia Yake. Hivyo ndivyo alivyokuusieni kwayo mpate kumcha.”[3]

Njia ya haki ni mtu kushikamana barabara na Kitabu cha Allaah na Sunnah za Mtume wa Allaah (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam) na kutoenda kinyume navyo kama ilivyothibiti katika Hadiyth:

“Nimewaachia mambo mawili ambayo mkishikamana nayo hamtopotea baada yake: Kitabu cha Allaah na Sunnah zangu. Havitofarikiana mpaka virudi kwangu katika hodhi.”[4]

Mtume (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam) ametubashiria kuhusu daima kubaki kikundi katika Ummah wangu juu ya haki mpaka siku ya Qiyaamah. Jaabir bin ´Abdillaah (Radhiya Allaahu ´anh) amesema:

“Nimemsikia Mtume wa Allaah (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam) akisema: “Hakutoacha katika Ummah wangu kuendelea kuwepo kikundi kikipambana juu ya haki mpaka siku ya Qiyaamah.”[5]

Ndugu wapendwa! Huu ni utangulizi wa maudhui ambayo nataka kuyaingia kwa jina la: “Uhakika wa Suufiyyah katika mwanga wa Qur-aan na Sunnah”. Hilo ni kwa sababu Suufiyyah baada ya karne ya tatu Hijrah mpaka hivi leo, wameathiri maisha ya Waislamu wengi. Wamefikisha kilele chake katika miaka ya karne za mwisho na wameathiri sana ´Aqiydah za Waislamu wengi na wamezigeuza kutoka nje ya njia yake sahihi ambayo Qur-aan Tukufu na Sunnah safi imekuja navyo. Hichi ndio kipengele khatari sana katika vipengele vya Suufiyyah, kwa sababu fikira za ki-Suufiy zimechanganyika na kuwategemea mawalii na Mashaykh na kupetuka mpaka katika kuwatakasa wafu, kama jinsi imechanganyika na nadharia ya kwamba Allaah amekita kwenye kila kitu na kwamba kila kitu kilichopo ni Allaah, tukiongezea juu ya hayo vile vipengele vyengine vya Kiislamu ambavyo Suufiyyah wameviharibu. Watu wake wanawategemea watu wengine, ilihali wale waongo wanadai kwamba wanamtegemea Allaah, na wanatendea kazi utawa. Hali kadhalika wameharibu roho ya Jihaad ya kupambana katika njia ya Allaah kwa kitu ambacho wanadai kuwa ni Jihaad kubwa zaidi, nayo ni mtu kupigana Jihaad na nafsi yake mwenyewe. Wanafanya hivo kwa kutegemea Hadiyth isemayo:

“Tumetoka katika Jihaad ndogo na kuiendea Jihaad kubwa zaidi; Jihaad ya kupigana na nafsi.”

Hadiyth hii ni batili, jambo ambalo limepelekea katika miaka ya hivi karibuni kuzipa fursa nchi za wakoloni kushambulia nchi nyingi za Waislamu – na bado Suufiyyah ni wenye kuendelea kukithiri kwa wingi katika miji ya Waislamu.

[1] al-Bukhaariy na Muslim.

[2] Ahmad na Abu Daawuud. al-Haafidhw ameifanya kuwa nzuri.

[3] Swahiyh. Ameipokea Ahmad na an-Nasaa´iy.

[4] Swahiyh al-Haakim.

[5] Muslim.

  • Mhusika: Shaykh Muhammad bin Rabiy´ bin Haadiy al-Madkhaliy
  • Mfasiri: Firqatunnajia.com
  • Marejeo: Haqiyqat-us-Suufiyyah
  • Imechapishwa: 10/12/2019