Ni lazima mtu awe ndani ya swalah katika du´aa ya siku ya ijumaa?

Swali: Mtume (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam) amesema katika Hadiyth kuhusu saa ya kujibiwa du´aa siku ya ijumaa:

“… naye akiwa amesimama akiswali.”

Je, hii ina maana kwamba mtu akitaka kuomba du´aa ni lazima awe ndani ya swalah?

Jibu: Hapana, si lazima. Kuhusu saa ya ijumaa, wanazuoni wametofautiana kuhusu wakati wake kwa maoni mengi. Haafidhw Ibn Hajar (Rahimahu Allaah) amesema:

”Wanazuoni wametofautiana kuhusu saa hiyo kwa maoni arobaini. Lakini maoni yenye nguvu zaidi ni mawili:

1 – Ni kuanzia wakati Khatwiyb anapoingia siku ya ijumaa hadi swalah inapomalizika. Hivyo mtu huomba du´aa katika vipindi vya unyamazo wa imamu, baina ya Khutbah mbili, katika Sujuud na ndani ya swalah.

2 – Ni saa ya mwisho ya siku ya ijumaa baada ya ´Aswr.

Zimekuja Hadiyth kuhusu jambo hili.

Maneno yake (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam):

“… naye akiwa amesimama akiswali.”

haimaanishi kuwa ni lazima awe anaswali, kwa sababu anayengojea swalah anahesabiwa kuwa yuko katika hukumu ya mwenye kuswali.

  • Muhusika: ´Allaamah ´Abdul-´Aziyz bin ´Abdillaah ar-Raajihiy
  • Tarjama: Firqatunnajia.com
  • Marejeo: Fataawaa Mutanawwi´ah (24)
  • Imechapishwa: 18/09/2026