Ibn Baaz Kuhusu Allaah Alimuumba Aadam Kwa Sura Yake

Swali: Allaah amemuumba Aadam kwa sura Yake. Je, hii ina maana kwamba sifa zote alizonazo Aadam ndizo alizonazo Allaah?

Jibu: Haya yamethibiti kutoka kwa Mtume (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam) katika “as-Swahiyh” ya al-Bukhaariy na ya Muslim aliposema (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam):

“Allaah alimuumba Aadam kwa sura Yake.”

Katika upokezi wa Ahmad na kundi la Ahl-ul-Hadiyth wengine imekuja:

“Allaah alimuumba Aadam kwa sura ya ar-Rahmaan.”

Dhamira katika Hadiyth ya kwanza inarudi kwa Allaah. Wanachuoni kama mfano wa Ahmad, Ishaaq bin Raahuuyah na maimamu wengine wa Salaf wamesema:

“Ni wajibu kuipitisha kama ilivyokuja kwa njia inayolingana na Allaah. Mtu anatakiwa kufanya hivo pasi na kushabihisha, kufananisha wala kukanusha.”

Hilo halipelekei ya kwamba sura Yake (Subhanaah) ni kama mfano wa sura ya Aadam kama ambavyo vilevile haipelekei kule kumthibitishia Allaah uso, mkono, vidole, unyayo, mguu, kughadhibika na sifa Zake nyenginezo ni kama mfano wa sifa za wanaadamu. Yeye (Subhaanah) anasifika kwa yale aliyojielezea Mwenyewe au kwa yale aliyoelezewa na Mtume Wake (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam) kwa njia inayolingana Naye pasi na kufanana na viumbe Wake kwenye chochote katika hayo. Amesema (´Azza wa Jall):

لَيْسَ كَمِثْلِهِ شَيْءٌ ۖ وَهُوَ السَّمِيعُ الْبَصِيرُ

“Hakuna chochote kinachofanana Naye – Naye ni Mwenye kusikia, Mwenye kuona.” (42:11)

Ni lazima kwetu kuipitisha kama ilivyotajwa kwa njia aliyoikusudia Mtume (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam). Tunatakiwa kufanya hivo pasi na kuifanyia namna wala kuipigia mfano.

Maana yake – na Allaah ndiye mjuzi zaidi – ni kwamba alimuumba Aadam kwa sura Yake akiwa ni mwenye uso, mwenye kusikia, mwenye kuona, anasikia, anaongea, anaona na anafanya mengineyo. Hilo halipelekei ya kwamba uso wa Aadam ni kama uso wa Allaah, kusikia kwa Aadam ni kama kusikia kwa Allaah, kuona kwa Aadam ni kama kuona kwa Allaah na kadhalika. Vivyo hivyo haipelekei ya kwamba sura ya Aadam ni kama sura ya Allaah. Hii ndio kanuni ya kijumla juu ya mlango huu kwa mujibu wa Ahl-us-Sunnah wal-Jamaa´ah. Nayo ni kuzipitisha Aayah na Hadiyth zinazozungumzia sifa za Allaah kwa udhahiri wake pasi na kuzipotosha, kuzifanyia namna, kuzifanyia mfano wala kuzikanusha. Kinyume chake wanamthibitishia Allaah majina Yake bila ya kuzifanyia mfano na wakati huo huo wanamtakasa kushabihiana na viumbe Wake bila ya kukanusha. Hivi ni tofauti na wanavyofanya Ahl-ul-Bid´ah katika Mu´attwilah na Mushabbihah. Usikizi, uoni na ujuzi wa viumbe sio kama ujuzi wa Allaah. Mambo ni namna hii hata kama ile aina ya ujuzi, usikizi na uoni ni wenye kuafikiana. Lakini yale aliyopwekeka nayo Allaah hayafanani na yeyote katika viumbe Wake. Hakuna kitu mfano Wake. Kwa kuwa sifa Zake ni sifa kamilifu na haziingiliwi na kasoro aina yoyote ile. Inapokuja katika sifa za viumbe zinaingiliwa na mapungufu na kuondoka kama katika ujuzi, usikizi, uoni na mengineyo.

  • Mhusika: Imaam ´Abdul-´Aziyz bin ´Abdillaah bin Baaz
  • Mfasiri: Firqatunnajia.com
  • Marejeo: https://www.binbaz.org.sa/fatawa/286
  • Imechapishwa: 28/01/2017