87. ´Aqiydah inayopelekea kumkana mungu

Imaam adh-Dhahabiy (Rahimahu Allaah) amesema:

”Katika mambo yanayofahamisha kuwa Muumba (Tabaarak wa Ta´ala) yuko juu ya kila kitu, juu ya ´Arshi Yake tukufu, na hakukita mahali popote, ni maneno Yake (Ta´ala)… ”[1]

Yatafakari maneno haya! Kwani ndani yake kuna haki, ambayo kutokana na ujinga, kumewafanya watu wengi mosi kupinga yale yanayofahamishwa na dalili nyingi ndani ya Qur-aan na Sunnah kuhusu ujuu Wake (Ta´ala) juu ya ´Arshi Yake, pili kuwatukana Salafiyyuun wanaoyaamini. Wanadai kuwa Salafiyyuun wamemfanya Allaah (´Azza wa Jall) kuwa na mahali juu ya ´Arshi – ametakasika Allaah kutokana na yale wanayoyasema madhalimu kutakasika kukubwa! Huyu hapa mtunzi wa kitabu – ambaye ni mmoja katika maimamu wao wakubwa, ambaye anatamka wazi kutakasika kwa Allaah (Ta´ala) kutokana na kuingia ndani ya maeneo yote. Hakuna kingine kinachowafanya watu hawa wengi kufahamu kwao kimakosa ya kwamba kuamini uwepo wa Allaah (´Azza wa Jall) juu ya viumbe Wake kunampelekea eti amekita ndani ya viumbe Wake. Wanasema eti kuwa hilo ni batili –  na kila kinachopelekea katika batili basi nacho ni batili. Hata hivyo hawajui, au wamejifanya ni wajinga, ya kwamba mahali ni jambo la kuwepo na kwamba hakuna kitu kilichozuka kilichopo juu ya ´Arshi. Kwa msemo mwingine ni kwamba kule juu hakuna sehemu kabisa. Kwa hiyo Allaah (Tabaarak wa Ta´ala) yuko juu ya ´Arshi Yake na si sehemu maalum. Miongoni mwa mambo yanayoshangaza ni kwamba watu hawa ambao hawaamini uwepo wa Allaah (´Azza wa Jall) juu ya ´Arshi Yake kwa sababu eti ya kukimbia kuamini sehemu, matokeo yake wametumbukia ndani ya jambo baya zaidi, nalo ni kuamini kuwa Allaah yuko sehemu kikweli. Wanasema kuwa Allaah yuko kila mahali au ndani ya kila kilichopo – Allaah ametakasika kukubwa kutokana na hayo!

Ajabu zaidi kuliko hayo ni kwamba baadhi walizindukana jinsi ´Aqiydah hiyo inamfananisha Allaah (´Azza wa Jall) na viumbe waliyokita kwenye maeneo. Wakataka kumtakasa kutokana na ufahamu huo, matokeo yake wakatumbukia katika jambo baya zaidi, nalo ni makanusho yanayopelekea kutokuwepo Kwake (Ta´ala) kabisa. Hivyo wakasema kuwa Allaah hayuko juu, chini, kuliani, kushotoni, mbele, nyuma, si ndani ya ulimwengu, nje ya ulimwengu, hakushikana na ulimwengu wala hakutengana nao. Haya nimeyasikia mara nyingi yakisemwa kutoka juu ya mimbari za ijumaa kutoka kwa baadhi ya wahubiri ambao watu wanawadhania vyema. Dini hii imekuwa na ugeni wa namna gani! Wanazuoni wamekuwa wajinga namna gani, sembuse wasiokuwa wasomi! Naapa kwa Allaah! Mtu ambaye ni mfaswaha zaidi angeliambiwa aelezee kitu ambacho hakipo, asingeliweza kueleza vyema zaidi kuliko maelezo ya watu hawa juu ya mungu wao. Kama alivosema mmoja katika wale maimamu wa wale waliotangulia, pengine ni Imaam Ibn-ul-Qayyim (Rahimahu Allaah), kwamba mfananishaji anaabudu sanamu na mkanushaji anaabudu kisichokuwepo. Yote haya ni kutokana na kupinda kutokana na Sunnah, Salaf na maimamu wa Hadiyth – Tunamuomba Allaah (Ta´ala) atukusanye nao chini ya bendera ya Muhammad (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam)!

[1] al-´Uluww lil-´Aliy al-Ghaffaar, uk. 106.

  • Mhusika: Imaam Shams-ud-Diyn Muhammad bin Ahmad adh-Dhahabiy
  • Mfasiri: Firqatunnajia.com
  • Marejeo: Mukhtasar-ul-´Uluww, uk. 122-123
  • Imechapishwa: 03/07/2024
  • taaliki: Imaam Muhammad Naaswir-ud-Diyn al-Albaaniy