30. Ngazi ya pili ya makadirio – matakwa ya Allaah yenye kutekelezeka na uwezo Wake wenye kuenea

Shaykh-ul-Islaam Ibn Taymiyyah (Rahimahu Allaah) amesema:

”2 – Ngazi ya pili ni yale matakwa ya Allaah yenye kutekelezeka na uwezo Wake wenye kuenea. Ni kuamini ya kwamba yale yote ambayo Allaah ametaka yatokee, yametokea, na yale ambayo hakutaka yatokee, hayakutokea, na kwamba hakuna chochote kinachotikisika wala kutulia mbinguni wala ardhini isipokuwa ni kwa utashi wa Allaah (Subhaanah), na kwamba hakuna chochote kinachokuwepo katika ufalme Wake isipokuwa yale anayoyataka na kwamba Yeye (Subhaanahu wa Ta´ala) juu ya kila jambo ni muweza katika vilivyopo na visivoykuwepo. Licha ya hivo, amewaamrisha waja kumtii na kumtii Mtume Wake na akawakataza kumuasi. Hakika (Subhaanah) anawapenda wenye kumcha, wafanyao wema na waadilifu. Anawaridhia wale wenye kuamini na wakatenda matendo mema. Hawapendi makafiri. Hawaridhii watenda madhambi. Haamrishi machafu. Hayuko radhi juu ya waja Wake kukufuru. Hapendi ufisadi. Waja ni wenye kutenda kikweli. Allaah ndiye ameumba matendo yao. Mja ni muumini na kafiri, mwema na muovu, mswaliji na mfungaji. Waja wanao uwezo juu ya matendo yao. Wanayo matakwa. Allaah ndiye kawaumba, uwezo na matakwa yao. Kama alivosema (Ta´ala):

لِمَن شَاءَ مِنكُمْ أَن يَسْتَقِيمَ وَمَا تَشَاءُونَ إِلَّا أَن يَشَاءَ اللَّـهُ رَبُّ الْعَالَمِينَ

“Kwa yule Atakaye miongoni mwenu anyooke. Na hamtotaka isipokuwa atake Allaah, Mola wa walimwengu.”[1]

Ngazi hii ya makadirio inakanushwa na wengi katika Qadariyyah, ambao Mtume (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam) amewaita kuwa ”waabudia moto wa ummah huu”. Lipo kundi lingine ambalo limechupa mipaka katika kuthibitisha kiasi cha kwamba wakafikia kumkanushia mja uwezo na utashi wake. Halafu wanadai kuwa matendo na hukumu za Allaah hazina hekima wala manufaa.”[2]

Hawa wa mwisho wamekusudiwa Ashaa´irah, kwa sababu wao ndio wamechupa mipaka na kukanusha hekima ya Allaah, jambo ambalo amelipambanua Ibn-ul-Qayyim (Rahimahu Allaah) katika ”Shifaa’-ul-´Aliyl fiyl-Qadhwaa’ wal-Qadar wal-Hikmah wat-Ta´liyl”. Rejea, kwa sababu ni muhimu sana.

[1] 81:28-29

[2] Majmuu´-ul-Fataawaa (1/148-150) kwa baadhi ya uandishi mpya.

  • Mhusika: Imaam Muhammad Naaswir-ud-Diyn al-Albaaniy
  • Mfasiri: Firqatunnajia.com
  • Marejeo: al-´Aqiydah at-Twahaawiyyah – Sharh wa Ta´liyq, uk. 44-45
  • Imechapishwa: 25/09/2024