Abu Muhammad ´Abdullaah bin Abiy Zayd al-Qayrawaaniy (Rahimahu Allaah) amesema:

Waja wamewekewa Malaika ambao wanayaandika matendo yao.

MAELEZO

Ahl-us-Sunnah wal-Jamaa´ah wanaamini watukufu wanaoandika ambao ni wale Malaika waliopewa kazi ya kulinda na kuandika matendo ya wanadamu, mazuri na maovu.

Allaah amewaumba Malaika kwa nuru na wanazo mbawa. Allaah (Subhaanahu wa Ta´ala) amesema:

الْحَمْدُ لِلَّـهِ فَاطِرِ السَّمَاوَاتِ وَالْأَرْضِ جَاعِلِ الْمَلَائِكَةِ رُسُلًا أُولِي أَجْنِحَةٍ مَّثْنَىٰ وَثُلَاثَ وَرُبَاعَ ۚ يَزِيدُ فِي الْخَلْقِ مَا يَشَاءُ ۚ إِنَّ اللَّـهَ عَلَىٰ كُلِّ شَيْءٍ قَدِيرٌ

“Himdi zote njema anastahiki Allaah, Mwanzilishi wa mbingu na ardhi, Mwenye kuwafanya Malaika kuwa wajumbe wenye mbawa mbilimbili na tatutatu na nnenne. Huzidisha katika uumbaji atakavyo. Hakika Allaah ni Muweza juu ya kila jambo.”[1]

Kutokana na uwezo Allaah wanaruka, wanapanda juu na wanashuka chini. Allaah amewawezesha kufanya hivo. Sisi hatuwaoni kwa umbile lao, lakini wanaweza kuja kwa umbile la kibinadamu. Kwa sababu sisi hatuwezi kuwaona kwa umbile lao na kwa ajili hiyo ndio maana wanakuja kwa umbile la kimtu ili tusiogope juu ya kuwaona. Kama ambavo Jibriyl alikuwa akimjia Mtume (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam) mbele ya Maswahabah zake katika umbile la Dihyah al-Kalbiy (Radhiya Allaahu ´anh)[2].

Kuwaamini Malaika ni moja katika zile nguzo sita za imani. Imetajwa katika Hadiyth ya Jibriyl (´alayhis-Salaam) pale alipomuuliza Mtume (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam) kuhusu imani ambapo akajibu:

“Imani ni kumwamini Allaah, Malaika Wake, Vitabu Vyake, Mitume Yake, siku ya Mwisho na kuamini Qadar, nzuri yake na shari yake.”[3]

[1] 35:1

[2] al-Bukhaariy (3634).

[3] Muslim (8).

  • Mhusika: Imaam Swaalih bin Fawzaan al-Fawzaan
  • Mfasiri: Firqatunnajia.com
  • Marejeo: Bayaan-ul-Ma´aaniy fiy Sharh Muqaddimati Ibn Abiy Zayd al-Qayrawaaniy, uk. 79
  • Imechapishwa: 30/08/2021