Mlango unaozungumzia kuanza kwa funga ya mchana na mwisho wake

Allaah (Ta´ala) amesema:

أُحِلَّ لَكُمْ لَيْلَةَ الصِّيَامِ الرَّفَثُ إِلَىٰ نِسَائِكُمْ ۚ هُنَّ لِبَاسٌ لَّكُمْ وَأَنتُمْ لِبَاسٌ لَّهُنَّ ۗ عَلِمَ اللَّـهُ أَنَّكُمْ كُنتُمْ تَخْتَانُونَ أَنفُسَكُمْ فَتَابَ عَلَيْكُمْ وَعَفَا عَنكُمْ ۖ فَالْآنَ بَاشِرُوهُنَّ وَابْتَغُوا مَا كَتَبَ اللَّـهُ لَكُمْ ۚ وَكُلُوا وَاشْرَبُوا حَتَّىٰ يَتَبَيَّنَ لَكُمُ الْخَيْطُ الْأَبْيَضُ مِنَ الْخَيْطِ الْأَسْوَدِ مِنَ الْفَجْرِۖ ثُمَّ أَتِمُّوا الصِّيَامَ إِلَى اللَّيْلِ

“Mmehalalishiwa usiku wa swawm kujamiiana na wake zenu; wao ni vazi kwenu na nyinyi ni vazi kwao. Allaah anajua kwamba nyinyi mlikuwa mkizihini nafsi zenu hivyo akapokea tawbah yenu na akakusameheni. Basi sasa changanyikeni nao [waingilieni] na tafuteni Aliyokuandikieni Allaah kwenu. Kuleni na kunyweni mpaka ubainike kwenu weupe wa alfajiri katika weusi wa usiku. Kisha timizeni swawm mpaka usiku.”[1]

Imaam Ibn Kathiyr (Rahimahu Allaah) amesema:

“Hii ni ruhusa ya Allaah kwa waislamu na kuondoshewa ile hali iliokuweko mwanzoni mwa Uislamu. Hali ilikuwa pindi anapofungua mmoja wao, basi ni halali kwake kula, kunywa na kufanya jimaa hadi wakati wa swalah ya ´ishaa au akilala tu ijapo ni kabla ya hapo. Pindipo tu atalala au akaswali ´ishaa, basi kula chakula, kunywa na kufanya jimaa kunakuwa ni haramu kwake mpaka usiku wa kufuata. Wakapata kutokana na hali hiyo uzito mkubwa. Ndipo kukateremka Aayah hii na wakafurahi furaha kubwa. Kwa vile Allaah amewahalalishia kula, kunywa na kufanya jimaa wakati wowote wa usiku mfungaji atataka mpaka pale kutapobainika mwanga wa asubuhi kutokamana na giza la usiku.”[2]

Hivyo kukabainika kutokana na Aayah tukufu muda uliopangwa wa funga ya mchana mwanzo na mwisho wake. Muda wake ni kuanzia pale ambapo kutapochomoza alfajiri ya pili na mwisho wake ni mpaka kuzame kwa jua.

[1] 02:187

[2] Tazama ”Tafsiyr Ibn Kathiyr” (01/288-290).

  • Mhusika: Imaam Swaalih bin Fawzaan al-Fawzaan
  • Mfasiri: Firqatunnajia.com
  • Marejeo: al-Mulakhasw al-Fiqh (01/378-379)
  • Imechapishwa: 30/03/2021