Wako ambao wanawapa udhuru na wanasema kwamba hawa wanaoabudu makaburi ni wajinga. Wanasema kwamba wanapewa udhuru kwa ujinga. Mara nyingi tunasikia maneno haya au tunayasoma katika vitabu vyao. Wanakiri kwamba kitendo hichi hakijuzu lakini kwamba watu hawa ni wajinga.

Tunawajibu kwa kuwaambia: Vipi watakuwa ni wajinga na wao wanasoma Qur-aan na ndani yake kuna makatazo juu ya shirki na kuweka mkati na kati asiyekuwa (´Azza wa Jall)? Yule ambaye kafikiwa na Qur-aan naye ni mwarabu anayefahamu maana yake, hoja imekwishamsimamia. Amesema (Jalla wa ´Alaa):

وَأُوحِيَ إِلَيَّ هَـٰذَا الْقُرْآنُ لِأُنذِرَكُم بِهِ وَمَن بَلَغَ

”Nimefunuliwa hii Qur-aan ili nikuonyeni kwayo na kila itayomfikia.” (al-An´aam 06:19)

Kwa kifupi ni kwamba hawana hoja yoyote. Hoja yao ni batilifu mbele ya Mola wao. Tunamuomba Allaah awaongoze katika usawa, washikamane na haki, waache ukaidi, kufuata kichwa mchunga na badala yake warudi katika Kitabu cha Mola wao na Sunnah za Mtume wao Muhammad (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam). Lengo ni wao wahakikishe Uislamu wao, wairekebishe dini yao na wawe katika Ummah wa Muhammad (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam) na wasiwe miongoni mwa jumla ya wa washirikina na wafuasi wa Abu Jahl na Abu Lahab.Yule ambaye kafikiwa na Qur-aan naye ni mwarabu, basi hoja imemsimamia. Akiwa sio mwarabu basi ni lazima atarjumiwe maana yake mpaka aifahamu. Wawa watu wanaoyaabudu makaburi wanaishi katika miji ya waarabu nao ni waarabu wenye ufaswaha. Pengine baadhi yao wakawa wamehifadhi kitabu cha “Siwabayh”, wanaitambua lugha ya kiarabu na balagha. Lakini pamoja na haya yote wanaabudu kaburi. Hivi kweli mtu huyu ni mwenye kupewa udhuru? Mara nyingi utayakuta makaburi na makuba haya katika miji ya waarabu ambao Qur-aan imeteremka kwa lugha yao. Vipi mtathubutu kusema kwamba watu hawa ni wajinga? Ujinga utaendelea mpaka lini? Baada ya kutumwa Mtume (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam) na kuteremshwa Qur-aan ujinga umeondoka na kumekuja elimu na hoja.  Mtu huyu apewe udhuru ilihali anaishi katika mji wa waislamu, amehifadhi Qur-aan, anasoma na kusikiliza Qur-aan na anasikia maneno ya wanachuoni khaswa khaswa baada ya kuja hivi vyombo vya mawasiliano ambavyo vinawanukulia watu maneno ya wanachuoni na Qur-aan inasomwa asubuhi na jioni kwa sauti inayosikiwa na ambaye yuko mashariki na magharibi. Vipi mtu anaweza kweli kuthubutu kwamba watu hawa hawajafikiwa na hoja na kwamba ni wajinga? Pamoja na kuwa wengi wao wana vyeti vya juu inapokuja katika lugha ya kiarabu, elimu za dini, elimu za visomo, Fiqh na misingi?

Shani ya mambo ni kwamba hili ni jambo kubwa na la khatari. Nyinyi mnasoma, mnasikia na wako miongoni mwao ambao wamesafiri na wakaona ajabu ya maajabu katika matendo ya watu hawa, shirki zao na mizimu yao na wala hawakubali nasaha zozote. Hawamsikii yule anayewaita katika haki isipokuwa wachache anaowachagua Allaah. Hili ni jambo la khatari. Haijuzu kwa mwanafunzi wala mwanachuoni kunyamazia jambo hili. Bali ni lazima kwake kuwabainishia watu, kuwawekea watu wazi na kulingania kwa Allaah. Ni wajibu pia kwa mtawala wa waislamu kuwapiga vita watu hawa mpaka dini iwe kwa ajili ya Allaah pekee.

  • Mhusika: Imaam Swaalih bin Fawzaan al-Fawzaan
  • Mfasiri: Firqatunnajia.com
  • Marejeo: Sharh Nawaaqidh-il-Islaam, uk. 53-54
  • Imechapishwa: 06/08/2018