23. Allaah kuzungumza na waja siku ya Qiyaamah na kuamini Hodhi

Imaam Ahmad bin Hanbal (Rahimahu Allaah) amesema:

“Inatakiwa kuamini kuwa Allaah atawazungumzisha waja siku ya Qiyaamah, hakuna baina yao na baina Yake mkalimani. Hili linatakiwa kuaminiwa na kusadikishwa. Inatakiwa kuamini Hodhi na kwamba Mtume wa Allaah (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam) ana hodhi ambayo Ummah wake siku ya Qiyaamah wataijia. Upana wake ni kama urefu wake na ni sawa na masafa ya safari ya mwezi. Vikombe vyake ni sawa na idadi ya nyota mbinguni, kama yalivyopokelewa mapokezi Swahiyh kupitia njia nyingi.”

MAELEZO

Hayo yanafahamishwa na Hadiyth Swahiyh ikiwa ni pamoja na:

“Hakuna yeyote kati yenu isipokuwa Allaah atamzungumzisha siku ya Qiyaamah na kutakuwa hakuna mkalimani kati yao.”[1]

Kuhusiana na hodhi ya Mtume (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam), ni yale yaliyopokelewa ikiwa ni pamoja vilevile na al-Bukhaariy kutoka kwa Maswahabah wengi, akiwemo Abu Hurayrah na Asmaa´ bint Abiy Bakr (Radhiya Allaahu ´anhum), yanayofahamisha ya kwamba Mtume (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam) ana hodhi itakayoendewa na waumini kinyume na watenda madhambi katika Ummah wake. Miongoni mwa dalili hizo ni maneno ya Mtume (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam):

“Watanijia mimi watu. Pale nitapotaka kuwashika tahamaki atajitokeza mtu kati yangu mimi na wao na atasema: “Njooni!” Nitasema: “Kwenda wapi?” Atasema: “Ninaapa kwa Allaah! Kwenda Motoni!” Niseme: “Hakika hawa ni katika Maswahabah zangu”, aambiwe: “Hakika wewe hujui yale waliyozusha baada yako.”[2]

Kuna Hadiyth nyingi zenye maana kama hii.

[1] al-Bukhaariy (6539) na Muslim (1016).

[2] al-Bukhaariy (6576) na Muslim (2297).

  • Mhusika: ´Allaamah Ahmad bin Yahyaa an-Najmiy
  • Mfasiri: Firqatunnajia.com
  • Marejeo: Itmaam-ul-Minnah, uk. 114-115
  • Imechapishwa: 22/04/2019