Ndugu wapendwa! Jipambeni kwa adabu za funga na jiepusheni na zile sababu za kuadhibiwa na kupatilizwa. Jipambeni kwa sifa za Salaf watukufu. Kwani hakika mwisho wa Ummah huu hautofaulu isipokuwa kwa yale yaliyowafanya wa mwisho wao kufaulu katika matendo mema na kujiepusha na madhambi. Ibn Rajab (Rahimahu Allaah) amesema:

“Kuna ngazi mbili za wafungaji; ngazi ya kwanza ni wale walioacha chakula chao, kinywaji chao na matamanio yao kwa ajili ya Allaah (Ta´ala) ambapo anataraji zawadi ya hayo Peponi. Hakika huyu amefanya biashara pamoja na Allaah na amefanya vyema; Allaah hapotezi ujira wa aliyefanya vyema matendo yake. Wala hakati tamaa pamoja Naye kwa anayeyafanya. Bali anampa faida iliokuwa kubwa zaidi. Mtume wa Allaah (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam) amesema kumwambia bwana mmoja:

“Hakika hutoacha chochote kwa ajili ya kumuogopa Allaah isipokuwa Allaah atakupa bora kuliko hicho.”

Ameipokea Imaam Ahmad[1].

 Mfungaji huyu Allaah atampa Peponi atakacho katika vyakula, vinywaji na wanawake. Allaah (Ta´ala) amesema:

كُلُوا وَاشْرَبُوا هَنِيئًا بِمَا أَسْلَفْتُمْ فِي الْأَيَّامِ الْخَالِيَةِ

“Kuleni na kunyweni kwa furaha kwa yale mliyoyatanguliza katika siku nyingi zilopita.”[2]

Mujaahid na wengineo wamesema:

“Imeteremka juu ya wafungaji.”

Hadiyth ya ´Abdur-Rahmaan bin Samurah ambapo alimuona Mtume (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam) usingizini mwake akasema:

“Nilimuona bwana mmoja katika Ummah wangu akitoa ulimi nje na kuhema kwa ajili ya kiu na kila anapokaribia hodhi anazuiwa na kufukuzwa. Ikamjia funga ya Ramadhaan ambapo akampa maji na kuondosha kiu.”

Ameipokea at-Twabaraaniy.

[1] Swahiyh.

[2] 69:24

  • Mhusika: Imaam Muhammad bin Swaalih bin ´Uthaymiyn
  • Mfasiri: Firqatunnajia.com
  • Marejeo: Majaalis Shahr Ramadhwaan, uk. 79-80
  • Imechapishwa: 29/04/2021