32. Dhana zisizowezekana juu ya Mtume na Maswahabah

Shaykh-ul-Islaam Ibn Taymiyyah amesema:

Ni jambo la muhali kabisa kwamba aliwafunza kila kitu chenye kuwanufaisha katika dini, kukiwemo mambo ya kina, akaacha kuwafunza yale watayoyatamka kwa ndimi zao na wakayaamini ndani ya nyoyo zao juu ya Mola wao na Mwabudiwa Wao, Mola wa walimwengu.

MAELEZO

Ni jambo lisilowezekana kabisa ikawa Mtume (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam) amewafunza ummah wake kila kitu kinachowanufaisha katika dini na dunia yao, kama ambavyo Maswahabah wenyewe walilikiri hilo, akaacha kuzungumzia Tawhiyd na ´Aqiydah ambavyo ndio asili na msingi na ndio jambo ambalo Mitume wote wametumwa kulibainisha na kulilingania. Hapa wanaraddiwa wale ambao wanasema kuwa Aayah na Hadiyth zinazozungumzia majina na sifa za Allaah hazitakiwi kufahamika kwa udhahiri wake, bali zina maana nyingine ambayo haikubainishwa na Mtume (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam). Mtunzi wa kitabu (Rahimahu Allaah) anawaambia kuwa ni jambo lisilowezekana Mtume (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam) eti hakubainisha jambo hilo, na haiwezekani pia ikawa Maswahabah walilinyamazia na wakaacha kuwafikishia watu ubainifu huu. Maneno ya wapinzani ima ikawa kwamba Mtume (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam) alificha haki na akaacha kubainisha, jambo ambalo ni kufuru kwa sababu nadharia hiyo ni kumtuhumu Mtume (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam), au alibainisha haki lakini Maswahabah wakaificha. Nadharia hiyo ni tuhuma dhidi ya Maswahabah. Kwa msemo mwingine haiwezekani Mtume (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam) akaacha kubainisha haki ya Allaah ya kuabudiwa pekee, majina na sifa Zake ambayo watu wote wanatakiwa kuyatambua, kuyatamka na kuyaamini. Hii maana yake ni kwamba ´Aqiydah sahihi ni lazima kutamkwa na kuitambua kidhahiri. Mtume (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam) amewabainishia yote mawili; amewabainishia wanayopasa kuyaamini na vilevile amebainisha yanayotakiwa kusemwa na ndimi zao katika kumsifu Allaah na kutambua haki ya Allaah ya kuabudiwa pekee.

Watu hawa ambao wanamtuhumu Mtume (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam) na wanawatuhumu Maswahabah wako na kinyume chao hii leo wanaosema kuwa Tawhiyd jambo lake ni jepesi na kwamba waislamu wote wanaijua pasi na kuwa na haja ya kubainishiwa na kuisoma. Wanachukulia wepesi jambo la ´Aqiydah na wanawakemea wale ambao wanatilia mkazo jambo la ´Aqiydah, kuwafunza nayo watu na kuwabainishia nayo. Wanawarushia tuhuma za uwongo, kufarikisha watu na nyenginezo nyingi.

  • Mhusika: Imaam Swaalih bin Fawzaan al-Fawzaan
  • Mfasiri: Firqatunnajia.com
  • Marejeo: at-Ta´liyqaat at-Tawdhwiyhiyyah ´alaa Muqaddimat-il-Fatwaaa al-Hamawiyyah, uk. 63-64
  • Imechapishwa: 04/08/2024