Abu Dharr (Radhiya Allaahu ´anh) amesema:

”Mtume (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam) hakufa na kumwacha ndege anayepiga kwa mbawa zake mbinguni isipokuwa ametufunza kitu juu yake.”[1]

´Umar bin al-Khattwaab (Radhiya Allaahu ´anh) amesema:

“Mtume wa Allaah (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam) alituhadithia kila kitu kuanza kwa uumbaji mpaka pale ambapo watu wa Peponi watakapoingia kwenye makazi yao na watu wa Motoni watakapoingia kwenye makazi yao. Aliyahifadhi hayo mwenye kuyahifadhi na aliyasahau mwenye kuyasahau.”[2]

MAELEZO

Abu Dharr (Radhiya Allaahu ´anh) anashuhudia kuwa Mtume (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam) amewabainishia watu mambo yote wanayoyahitaji katika dini yao, mpaka ndege wanaoruka angani; amewabainishia walio halali kuliwa na walio haramu kuliwa.

´Umar bin al-Khattwaab (Radhiya Allaahu ´anh) pia ameshuhudia mfano wake na akasema:

“Mtume wa Allaah (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam) alituhadithia kila kitu kuanza kwa uumbaji mpaka pale ambapo watu wa Peponi watakapoingia kwenye makazi yao na watu wa Motoni watakapoingia kwenye makazi yao. Aliyahifadhi hayo mwenye kuyahifadhi na aliyasahau mwenye kuyasahau.”

Hii ni Khutbah yake ndefu ambapo Mtume (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam) siku nzima alikhutubia. Inapofika wakati wa swalah, anashuka kutoka kwenye mimbari, anaswali kisha anapanda tena na kuwabainishia kila kitu. Hiki kilikuwa kisimamo chake (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam) kimoja tu. Aliwabainishia kuanzia mwanzo wa uumbaji mpaka pale ambapo watu wa Peponi watakapoingia Peponi na watu wa Motoni watakapoingia Motoni, elimu ambayo Allaah alimfunza. Hapa tu ilikuwa kwenye kikao kimoja ambapo akawabainishia (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam) kila wanachokihitaji. Alifanya nini wakati wa maisha yake yote? Maisha yake mazima ilikuwa kubainisha na kuweka wazi kimaneno na kivitendo. Kama alivosema ´Umar (Radhiya Allaahu ´anh):

“Aliyahifadhi hayo mwenye kuyahifadhi na aliyasahau mwenye kuyasahau.”

Kwa maana nyingine ni kwamba si kila mtu anayejua kinachobainishwa. Wanayajua baadhi ya wanazuoni na kuna wengi wasioyajua. Ujinga sio hoja kuwa Mtume (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam) hakubainisha. Mtume (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam) amebainisha, lakini watu wengi hawayajui. Hilo linatokana na upungufu wao, na si katika ubainifu wake Mtume (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam).

[1] Ahmad (5/153), al-Bazzaar (3897) na at-Twabaraaniy (1647).

[2] al-Bukhaariy (3192) na Muslim (2891).

  • Mhusika: Imaam Swaalih bin Fawzaan al-Fawzaan
  • Mfasiri: Firqatunnajia.com
  • Marejeo: at-Ta´liyqaat at-Tawdhwiyhiyyah ´alaa Muqaddimat-il-Fatwaaa al-Hamawiyyah, uk. 61-62
  • Imechapishwa: 04/08/2024