18. Kutokea chini kwenda juu kwa sababu ya Uislamu

Hapo kabla watu walikuwa wakiishi ndani ya upotofu wa wazi, kwa sababu ya kile kipindi kirefu kilichopita kati yake (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam) na wale Mitume wengine waliotangulia. Wakati alipotumwa Mtume huyu (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam) ndipo ikaenea elimu yenye manufaa ambapo watu wakatoka katika viza na wakaingia ndani ya nuru. Kukapatikana wanazuoni. Kukapatikana kati ya watu elimu yenye manufaa. Kama hali ilivyo hii leo. Tuko na Qur-aan, Sunnah na maneno ya wanazuoni. Hii ni nuru kutoka kwa Allaah ilioko mikononi mwa watu. Hoja imesimama hii leo. Mtume (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam) amesema:

”Nimekuacheni katika njia ya wazi; usiku wake ni kama mchana wake. Hakuna atakayepinda kuiacha isipokuwa mwangamivu.”[1]

”Mimi nimekuachieni yale ambayo endapo mtashikana nayo hamtopotea kamwe, Kitabu cha Allaah na Sunnah zangu.”[2]

“Nakuusieni kumcha Allaah (´Azza wa Jall) na kusikiliza na kutii hata kama atatawaliwa juu yenu na mja. Hakika yule atakayeishi muda mrefu katika nyinyi basi atakuja kuona tofauti nyingi. Hivyo basi, lazimianeni na Sunnah zangu na Sunnah za makhaliyfah wangu waongofu na wenye kuongoza. Ziumeni kwa magego yenu. Ninakutahadharisheni na mambo yaliyozuliwa, kwani hakika kila Bid´ah ni upotevu.”[3]

Mtume (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam) ni sayari ambayo Allaah ameangaza kwayo ulimwengu baada ya viza na kipindi hicho watu walikuwa katika upotofu  wa wazi. Allaah (Subhaanahu wa Ta´ala) amesema:

هُوَ الَّذِي بَعَثَ فِي الْأُمِّيِّينَ رَسُولًا مِّنْهُمْ يَتْلُو عَلَيْهِمْ آيَاتِهِ وَيُزَكِّيهِمْ وَيُعَلِّمُهُمُ الْكِتَابَ وَالْحِكْمَةَ وَإِن كَانُوا مِن قَبْلُ لَفِي ضَلَالٍ مُّبِينٍ

“Yeye ndiye aliyempeleka Mtume kwa wasiojua kusoma wala kuandika anayetokamana na wao; anawasomea Aayah Zake na anawatakasa na anawafunza Kitabu na hekima na japo walikuwa hapo kabla katika upotofu wa wazi.”[4]

Wasiokuwa wasomi wanakusudiwa waarabu, kwa sababu hawakuwa na Kitabu kabla ya Qur-aan hii tukufu iliyovishinda na kuvihukumu Vitabu vyengine vyote vya kiungu:

لَّا يَأْتِيهِ الْبَاطِلُ مِن بَيْنِ يَدَيْهِ وَلَا مِنْ خَلْفِهِ تَنزِيلٌ مِّنْ حَكِيمٍ حَمِيد

“Haiingiliwi na batili mbele na nyuma yake – ni Uteremsho kutoka kwa Mwenye hekima, Mwenye kuhimidiwa.”[5]

Kimetumwa kwa watu wasiokuwa wasomi ambao hawasomi wala hawaandiki na wala hawana Kitabu kilichoteremshwa:

وَمَا آتَيْنَاهُم مِّن كُتُبٍ يَدْرُسُونَهَا ۖ وَمَا أَرْسَلْنَا إِلَيْهِمْ قَبْلَكَ مِن نَّذِيرٍ

”Na wala hatukuwapa kitabu chochote wakisomacho na wala hatukuwapelekea kabla yako mwonyaji yeyote.”[6]

لِتُنذِرَ قَوْمًا مَّا أَتَاهُم مِّن نَّذِيرٍ مِّن قَبْلِكَ لَعَلَّهُمْ يَتَذَكَّرُونَ

”… ili uwaonye watu ambao hawakufikiwa na mwonyaji yeyote kabla yako ili wapate kukumbuka.”[7]

Bi maana waarabu. Baada ya ujinga wakawa wasomi na wakaanza kuwafunza watu wote. Baada ya umasikini wakawa matajiri. Baada ya shirki na ukafiri wakawa wepwekeshaji. Baada ya kutwezwa ardhini wakawa mabwana wa ulimwengu ambao waliifungua miji na wakawaongoza watu. Kwa kitu gani? Kwa elimu yenye manufaa na matendo mema na mirathi ya Mtume (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam). Vinginevyo kabla ya hapo walikuwa ni watu wanyonge kabisa. Ni wapi imetoka elimu hii yenye kufurika ambayo mpaka hii leo inaendelea kufurika? Imetoka ndani ya Qur-aan na Sunnah ambavyo Mtume (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam) ametumilizwa navyo.

[1] Ahmad (4/126), Ibn Maajah (43) na al-Haakim (1/95).

[2] Maalik (1594) na al-Haakim (1/171).

[3] Abu Daawuud (4607), at-Tirmidhiy (2676) na Ibn Maajah (34). Swahiyh kwa mujibu wa al-Albaaniy katika ”al-Irwaa’” (2455).

[4] 62:2

[5] 41:42

[6] 34:44

[7] 28:46

  • Mhusika: Imaam Swaalih bin Fawzaan al-Fawzaan
  • Mfasiri: Firqatunnajia.com
  • Marejeo: at-Ta´liyqaat at-Tawdhwiyhiyyah ´alaa Muqaddimat-il-Fatwaaa al-Hamawiyyah, uk. 43-45
  • Imechapishwa: 28/07/2024