05. Makusudio ya elimu ambayo ni lazima kwa Ummah kuisoma

Kabla ya kuingia katia masuala haya tunapaswa kujua kwamba makusudio ya elimu ambayo ni lazima kwa Ummah kujifunza nayo, ima uwajibu kwa kila mmoja kwa dhati yake au uwajibu wenye kutosheleza, ni elimu ya dini aliyokuja nayo Mtume (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam).

Kuhusu elimu ya kidunia kama elimu ya sayansi, viwanda, hesabu, mazoezi na uhandisi ni elimu ambazo zimeruhusiwa kuzisoma. Wakati fulani zinaweza kuwa lazima pindi Ummah watapozihitajia. Ni lazima kwa anayeweza. Lakini hata hivyo sio elimu iliyokusudiwa ndani ya Qur-aan na Sunnah na ambayo Allaah amewasifia wenye nayo na akawatapa na ambayo Mtume (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam) amesema juu yake:

“Wanachuoni ndio warithi wa Mitume.”[1]

Makusudio ni elimu ya dini.

Ama elimu ya kidunia asiyeijua hapati dhambi na mwenye kuisoma ameruhusiwa. Akiwanufaisha Ummah basi anapewa thawabu kwayo. Mtu akifa ilihali hajui elimu hii hatoadhibiwa siku ya Qiyaamah. Lakini mwenye kufa na yeye hajui elimu ya kidini na khaswa elimu ya kilazima basi ataulizwa siku ya Qiyaamah ni kwa nini hakujifunza na kwa nini hakuuliza. Atakayesema kuwa Mola wake ni Allaah, dini yake ni Uislamu na Mtume wake ni Muhammad (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam) pindi atapolazwa ndani ya kaburi atasalimika. Ataulizwa ni wapi amejifunza mambo hayo ambapo atajibu kuwa alisoma na kujifunza Kitabu cha Allaah.

Kuhusu yule ambaye aliyapuuza hayo atapoulizwa ndani ya kaburi lake atasema kuwa hajui na kwamba aliwasikia watu wakisema kitu na yeye akakisema. Huyu atajaziwa moto ndani ya kaburi lake, atabanwa mpaka zikutane mbavu zake na kaburi lake litakuwa ni shimo miongoni mwa mashimo ya Motoni. Kwa sababu hajui na wala hakusoma. Ataambiwa:

“Hukujua na wala hukusoma.”[2]

Hakusoma na wala hawakufuata wanachuoni. Alikuwa mpotevu katika maisha yake. Huyu ndiye atakula khasara.

[1] al-Bukhaariy hali ya kuiwekea taaliki (67), Abu Daawuud (3641), Ibn Maajah (223) na at-Tirmidhiy (2682).

[2] al-Bukhaariy (1338), Muslim (2870) na Abu Daawuud (4753).

  • Mhusika: Imaam Swaalih bin Fawzaan al-Fawzaan
  • Mfasiri: Firqatunnajia.com
  • Marejeo: Sharh Thalaathat-il-Usuwl, uk. 19-20
  • Imechapishwa: 19/11/2020