Swali: Ni wepi ambao wanaruhusiwa kuacha kufunga Ramadhaan?

Jibu: Ambao wanaruhusiwa kuacha kufunga Ramadhaan ni wale wenye udhuru wa Kishari´ah. Nao ni hawa wafuatao:

1- Msafiri ambaye inajuzu kwake kufupisha swalah ambaye safari yake ni kilomita 80 na zaidi.

2- Mgonjwa ambaye endapo atafunga atakumbwa na ugumu, atasababisha maradhi kumzidi au yakachelewa kupona. Huyu anaruhusiwa kula.

3- Mwenye hedhi na damu ya uzazi. Haijuzu kwao kufunga ilihali wako na hedhi na nifasi. Ni haramu kwao kufunga. Vivyo hivyo mjamzito na mwenye kunyonyesha wakichelea juu ya nafsi zao au wakichelea juu ya watoto wao. Katika hali hii inajuzu kwao kuacha kufunga. Hali kadhalika mgonjwa ambaye hayatarajiwi kupona maradhi yake. Kadhalika mtumzima sana. Wote hawa ni miongoni mwa watu wenye udhuru ambao wameruhusiwa na Shari´ah kula.

Miongoni mwa hawa wako ambao wameamrishwa kulipa, kama mfano wa msafiri, mgonjwa ambaye maradhi yake yanatarajiwa kupona, mwenye hedhi, damu ya uzazi, mwenye mimba na mnyonyeshaji. Wote hawa ni wajibu kwao kulipa. Amesema (Ta´ala):

“Watimize idadi katika siku nyinginezo.”[1]

Kuhusu wale ambao hawawezi kulipa, kushindwa ambako ni kwa kuendelea, kama mfano wa mtumzima sana na mtu aliye na maradhi yasiyotarajiwa kupona, hawa sio lazima kulipa. Badala yake wanatakiwa kulisha maskini kwa kila siku moja waliokula. Amesema (Ta´ala):

“Na kwa wale wanaoiweza lakini kwa tabu watoe fidia kulisha masikini.”[2]

[1] 02:183

[2] 02:184

  • Mhusika: Imaam Swaalih bin Fawzaam al-Fawzaan
  • Mfasiri: Firqatunnajia.com
  • Marejeo: http://www.alfawzan.af.org.sa/node/14891
  • Imechapishwa: 30/05/2017