Ni lini inalipwa swalah iliyompita mtu?

Swali: Ni wakati gani wa mwisho mtu anaweza kulipa swalah za vile vipindi vitano ambazo mtu hakuziswali?

Jibu: Mtu akiacha moja katika zile swalah tano kwa sababu ya udhuru miongoni mwa nyudhuru, kama vile kusahau, kupitiwa na usingizi na mfano wa nyudhuru kama hizo, basi atailipa wakati atakapoondokewa na udhuru huo. Mtume (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam) amesema:

“Atayechukuliwa na usinigizi akapitwa na swalah au akaisahau basi aiswali atapokumbuka. Haina kafara isipokuwa kufanya hivo.”

Wakati (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam) yeye na Maswahabah zake walipopitikiwa na usingizi kwenye swalah ya Fajr walipokuwa safarini na hawakuamka isipokuwa baada ya jua kuchomoza, waliilipa. Mtume (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam) aliikidhi kwa sifa yake. Aliamrisha kuadhiniwe, kisha akaswali Rak´ah mbili kama anavyoiswali kila siku. Hiyo ina maana kwamba aliiswali kwa sauti ya juu.

Ama ikiwa mtu ameacha swalah kwa makusudi pasi na udhuru wa Kishari´ah, hapa ndipo wanachuoni wametofautiana. Wapo baadhi ya wanachuoni wenye – nao ndio wengi wenye kuona hivo – kwamba ni lazima kuilipa kama ilivyo lazima kwa yule mwenye udhuru. Kujengea juu ya maoni haya mtu akiacha swalah moja wapo mpaka ukatoka wakati wake kwa makusudi, basi ni lazima kuilipa. Baadhi ya wanachuoni wengine wakasema kuwa mwenye kuacha swalah kwa makusudi pasi na udhuru wa Kishari´ah basi hakumfai kitu kuilipa hata kama ataiswali mara elfumoja. Kwa sababu huko ni kuvuka mipaka ya Allaah. Jengine ni kwa sababu Mtume wa Allaah (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam) amesema:

“Mwenye kufanya kitendo kisichofikiana na amri yetu atarudishiwa mwenyewe.”

Kitendo hichi – yaani cha kuchelewesha swalah mpaka ukatoka wakati wake – hakiafikiana na amri ya Allaah wala Mtume Wake (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam). Hivyo kinakuwa ni chenye kurudishwa na si chenye kufaa. Kujengea juu ya maoni haya – ambayo pia ndio chaguo la Shaykh-ul-Islaam Ibn Taymiyyah – ni lazima kwa mtu huyu kuyatengeneza matendo yake, kutubu kwa Allaah tawbah ya kweli, kukithirisha kuomba msamaha na matendo mengine mema atayosamehewa kwayo. Naona kuwa maoni haya ndio yenye nguvu kuliko maoni ya wale wanaosema kuwa ni lazima kuikidhi.

  • Mhusika: Imaam Muhammad bin Swaalih bin ´Uthaymiyn
  • Mfasiri: Firqatunnajia.com
  • Marejeo: Nuur ´alaad-Darb (10) http://binothaimeen.net/content/6732
  • Imechapishwa: 17/11/2020