Swali: Mimi nina kaka na ndugu ambao kwa masikitiko makubwa hawaswali na wala hawasimamishi mipaka ya Allaah. Je, ni lazima juu yangu kuwakata? Kila ninapowaamrisha mema au kuwakataza maovu, wanafanya mzaha na maskhara na mimi na wanasema “je wewe unataka kuwafanya watu wote kuwa wema?” Wao wamekataa kukaa na mimi na wamenikata, lipi la wajibu kwangu kufanya juu yao?

Jibu: Ni juu yako kuwahama na kuwakata. Maadamu hawakubali nasaha na hawaswali, inatakikana kwako kuwahama na kuwakata mpaka hapo Allaah Atapowaongoza. Hili ndilo la wajibu, bali hii ndio Sunnah iliyosisitizwa. Baadhi ya wanachuoni wanaona hivi, uwajibu wa kuwahama na kuwakata kutokana na upotofu wao na kuzuia njia za kheri. Lakini ukiwasiliana nao baadhi ya nyakati kwa kutaraji pengine Allaah Akawaongoza, kwa kuwalingania na kuwapa nasaha, hakuna neno. Na ikiwa wataendelea, hakuna neno kwako kuwakata na kujiweka kwako mbali nao kikamilifu. Mtume (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam) aliwakata Maswahabah watatu wakati walipoacha kwenda kupigana vita pamoja naye bila ya udhuru. Muhimu ni kuwa, watu hawa inatakikana kuwahama. Kwa uchache, kuwahama kunakuwa ni Sunnah iliyosisitizwa mpaka hapo Allaah Atapowaongoza na kuwarudisha katika usawa.

  • Mhusika: Imaam ´Abdul-´Aziyz bin ´Abdillaah bin Baaz
  • Mfasiri: Firqatunnajia.com
  • Marejeo: Fataawaa Nuur ´alaad-Darb (770)
  • Imechapishwa: 15/03/2018