Kullaabiyyah na Ashaa´irah wamethibitisha kuwa Allaah ataonekana Aakhirah na wakakanusha kuonekana katika upande fulani na kwamba ni kwa juu. Wamefanya hivo kwa kutaka kukusanya kati ya I´tiqaad ya kukanusha kuwa Allaah yuko na mwili na kuthibitisha kuonekana kwa kitu ambacho kina mwili kuona kitu kisichokuwa na mwili. Wametaka kuthibitisha kuonekana kwa kuwa ni kitu wasichoweza kukikanusha kutokana na maandiko yaliyothibiti juu yake, lakini wakati huo huo wametaka kuafikiana na Mu´tazilah katika kupinga upande na uwepo juu. Wao hawataki kutofautiana na Mu´tazilah, bi maana katika kukanusha uwepo juu wa Allaah. Kwa sababu wote wawili wanakanusha kuwa Allaah hana mwili na sehemu haiwi isipokuwa kwa vitu vilivyo na viwiliwili. Midhali Allaah hana mwili basi hawezi kuwa na mahala. Ashaa´irah wakataka kuwa pamoja na Ahl-us-Sunnah katika kuthibitisha kuonekana kwa Allaah Aakhirah na wakati huo huo kuwa pamoja na Mu´tazilah katika kukanusha kuonekana kwa upande fulani na kwamba ni kwa juu. Lakini hata hivyo wakashindwa kufanya hivo…

Ahl-us-Sunnah wakajadiliana nao kwa majibu mawili:

Mosi: Kullaabiyyah na Ashaa´irah mmeleta kitu ambacho kidharurah hakiingii akilini kabisa. Kiakili ni kwamba kila chenye kuonekana ni lazima kiwe upande fulani kwa yule mwenye kukitazama na isitoshe kiwe wazi wazi. Ni jambo lisilowezekana kukawa mtazamaji aliyesimama kukiangalia kitu isipokuwa kwa kuwepo upande fulani anapokitazamia. Ama kuwepo chenye kutazamwa pasina kuwepo na upande fulani ni kitu kisichoingia akilini kabisa.

Kwa ajili hii watu wengi wenye busara wamewacheka Kullaabiyyah na Ashaa´irah pale walipothibitisha kuwa Allaah ataonekana Aakhirah na wakati huo huo wakakanusha kuwa hatoonekana kwa upande fulani na kusema kuwa hili ni jambo lisilowezekana na haliingii akilini. Kwa ajili hii mapote yote ya kibinaadamu yamewakaripia Kullaabiyyah na Ashaa´irah na kuwacheka kwa kule kuthibitisha kwao kuonekana na wakati huo huo wakakanusha kuwa itakuwa kwa upande fulani. Ndio maana Mu´tazilah wakawashambulia na kuwaambia “Nyinyi mmejiingiza wenyewe kwenye mtego: vipi mtathibitisha kuonekana kwa Allaah Aakhirah kisha wakati huo huo mpinge kuwa ataonekana upande fulani? Ni moja kati ya mambo mawili; ni lazima mthibitishe kuwa ataonekana upande fulani na upande huo ni kwa juu na hivyo muwe ni maadui zetu kwani mtakuwa mmejiunga pamoja na Mushabbihah au mkanushe kuwa hatoonekana na kwa kufanya hivo mtakuwa wenzetu. Ama kubaki kwenu hali ya kuwa mnayumbayumba; mnathibitisha kuonekana na wakati huo huo mnapinga kuwa upande fulani, hili ni jambo lisiloingia akilini na haliwezekani.”

Pili: Jibu la pili ni kwamba kumethibiti Hadiyth ambazo zimepokelewa kwa mapokezi mengi [Mutawaatir] kutoka kwa Mtume (Swalla Allaahu ´alayhi wa salalm) zilizo wazi ya kwamba waumini watamuona Mola Wao siku ya Qiyaamah akiwa kwa juu. Kumekuja Hadiyth Swahiyh wakati Mtume (Swalla Allaahu ´alayhi wa salalm) alipoulizwa kama tutamuona Mola Wetu siku ya Qiyaamah? Akasema: “Je, mnasongamana katika kuona jua na mwezi?” Wakasema: “Hapana.” Akasema: “Basi na nyinyi mtamuona vivyo hivyo.” Katika Hadiyth ya pili: “Ee Mtume wa Allaah, hivi kweli tutamuona Mola Wetu siku ya Qiyaamah?” Mtume (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam) akasema: “Hivi mnadhurika mnapolitazama jua pasina kuwepo mawingu kati yake?” Wakasema: “Hapana, ee Mtume wa Allaah!” Akasema: “Basi mtamuona vivyo hivyo.” Katika Hadiyth nyingine imekuja: “Mtamuona Mola Wenu kwa macho yenu.”

Hizi ni dalili za wazi kabisa zinazoonesha kuwa sisi tutamuona Mola Wetu kama tunavyoona jua na mwezi. Sisi tunaona jua na mwezi kwa juu kwa macho. Hadiyth ziko wazi juu ya hili.

Makusudio ya Hadiyth sio kumshabihisha Allaah na mwezi au jua – Allaah ametakasika na hilo. Bali makusudio ni muonaji atakavyoona; bi maana sisi tutamuona Mola Wetu siku ya Qiyaamah muonekano wa wazi kabisa usiyotatiza kama jinsi tunavyoona jua na mwezi muonekano wa wazi juu yetu pasina kutatizika. Allaah hana anayefanana naye:

لَيْسَ كَمِثْلِهِ شَيْءٌ ۖ وَهُوَ السَّمِيعُ الْبَصِيرُ

“(Lan) Hakuna chochote kinachofanana Naye – Naye ni Mwenye kusikia, Mwenye kuona.” (42:11)

هَلْ تَعْلَمُ لَهُ سَمِيًّا

“Je, unamjua mwengine mwenye Jina kama Lake?” (19:65)

Haya yamebatilisha madai ya Kullaabiyyah na Ashaa´irah kusema kwamba ni jambo linawezekana kukawepo muonekano bila ya kutazamia kwa upande fulani.

  • Mhusika: ´Allaamah ´Abdul-´Aziyz bin ´Abdillaah ar-Raajhiy
  • Mfasiri: Firqatunnajia.com
  • Marejeo: al-Hidaayah ar-Rabbaaniyyah fiy Sharh al-´Aqiydah at-Twahaawiyyah (01/233-234)
  • Imechapishwa: 28/05/2020