Swali: Naomba nasaha na maelekezo ambayo yataninasua kuniondosha kutoka katika tatizo hili. Wakati ninapooga josho la janaba basi naweza kukaa bafuni kwa muda mredu inaweza kufika saa moja mpaka mbili, jambo ambalo limenitia uzito. Haya ni kwa sababu ya kusugua kwangu kwa wingi. Ni zipi sehemu ambazo mtu anatakiwa kuzisugua zaidi na ambazo hazifikiwi na maji?

Jibu: Hapana shaka kwamba mtu huyu ambaye ameuliza swali hili amesibiwa na [ugonjwa wa] wasiwasi. Namuomba Allaah amwondoshee. Kwa sababu uogaji ni mwepesi. Pitisha mkono wako juu ya mwili wako pasi na kusugua na inatosha kufanya hivo. Bali mtu akiingia ndani ya bwawa kwa nia ya kuondosha hadathi kisha akatoka ndani yake hadathi yake inaondoka. Hakuna kinachomlazimu isipokuwa kusukutua na kupandisha maji puani. Hapa inahusiana na janaba. Ama wudhuu´ ni lazima mtu apangilie na aanze kuosha uso kwanza, kisha mikono miwili, kisha afute kichwa halafu aoshe miguu miwili.

Nasaha zangu kwa ndugu huyu apuuzie jambo hili. Kwanza aanze kutawadha wudhuu´ wa kawaida wa swalah. Kisha ajimwagie maji kichwani mwake mpaka yamshuke. Halafu aoshe mwili wake uliobaki. Ahakikishe maji yameingia ndani ya makapwa. Kadhalika ahakikishe maji yameingia ndani ya mapaja mawili na sehemu zengine kuko wazi. Akipitisha mkono wake juu ya mwili wake basi amefanya linalompasa.

  • Mhusika: Imaam Muhammad bin Swaalih bin ´Uthaymiyn
  • Mfasiri: Firqatunnajia.com
  • Marejeo: al-Liqaa’ ash-Shahriy (50) http://binothaimeen.net/content/1150
  • Imechapishwa: 24/06/2019