Namna hii mnatakiwa kulingania katika Uislamu

Nimefikiwa na khabari kwamba baadhi yenu mmekemea Bid´ah zinazopatikana makaburi jambo ambalo limesababisha kutokea kwa matatizo. Mambo yakiwa ni hivo kweli basi natarajia kuwa mtalingania kwa Allaah kwa mujibu wa mfumo wa Mitume (Swalla Allaahu ´alayhim wa sallam). Kwa msemo mwingine muanze kulingania katika Tawhiyd na kumtakasia Allaah nia kwa aina zote za ´ibaadah, na khaswakhaswa du´aa. Kwa sababu watu wengi wamepondoka katika suala hili. Utawaona ni wenye kuwaomba mawalii, wakiwataka uokozi na msaada wakati wa shida na mfano wa hayo. Ilihali Allaah anasema:

وَمَنْ أَضَلُّ مِمَّن يَدْعُو مِن دُونِ اللَّـهِ مَن لَّا يَسْتَجِيبُ لَهُ إِلَىٰ يَوْمِ الْقِيَامَةِ وَهُمْ عَن دُعَائِهِمْ غَافِلُونَ وَإِذَا حُشِرَ النَّاسُ كَانُوا لَهُمْ أَعْدَاءً وَكَانُوا بِعِبَادَتِهِمْ كَافِرِينَ

“Ni nani aliyepotea zaidi kuliko yule anayemwomba badala ya Allaah, ambao hatowaitikia mpaka siku ya Qiyaamah nao hawatambui maombi yao. Na pale watakapokusanywa watu, [waungu wao wa batili] watakuwa ni maadui wao na watakuwa wenye kuzikanusha ‘ibaadah zao.” (al-Ahqaaf 46:05-06)

Allaah amesema kuwa wale wenye kumuomba mwingine asiyekuwa Yeye ni wapotevu na akabainisha kuwa wale wenye kuombwa watakuwa ni maadui wa wale waliokuwa wakiwaomba na kwamba watakuwa ni wenye kukanusha ´ibaadah zao siku ya Qiyaamah. Amesema (Ta´ala) hali ya kuwazungumzisha wale wenye kumuomba asiyekuwa Yeye:

وَالَّذِينَ تَدْعُونَ مِن دُونِهِ مَا يَمْلِكُونَ مِن قِطْمِيرٍ إِن تَدْعُوهُمْ لَا يَسْمَعُوا دُعَاءَكُمْ وَلَوْ سَمِعُوا مَا اسْتَجَابُوا لَكُمْ ۖ وَيَوْمَ الْقِيَامَةِ يَكْفُرُونَ بِشِرْكِكُمْ ۚ وَلَا يُنَبِّئُكَ مِثْلُ خَبِيرٍ

“Na wale mnaowaomba badala Yake hawamiliki japo kijiwavu cha kokwa ya tende. Mkiwaomba, hawasikii maombi yenu, na hata wakisikia, hawatakuitikieni na siku ya Qiyaamah watakanusha ushirikina wenu – na wala hakuna atakayekujulisha vilivyo kama Mwenye khabari ya kila kitu].” (Faatwir 35:13-14)

Hapa Allaah amebainisha yafuatayo:

1- Wale wenye kuombwa badala ya Allaah ni mafukara, kwa njia ya kwamba hawamiliki hata kijiwavu cha kokwa ya tende.

2- Amebainisha kwamba hawasikii maombi ya wale wenye kuwaomba.

3- Kukikadiriwa kuwa wanawasikia basi hawawezi kuwaitikia wale wenye kuwaomba. Hayo ni kwa sababu si waweza na ni mafakiri ambao hawawezi kuwaitikia.

4- Siku ya Qiyaamah watakanusha shirki hii ya khatari. Allaah anasema:

فَادْعُوا اللَّـهَ مُخْلِصِينَ لَهُ الدِّينَ وَلَوْ كَرِهَ الْكَافِرُونَ

“Basi muombeni Allaah hali ya kuwa ni wenye kumtakasia dini japokuwa wanachukia makafiri.” (Ghaafir 40:14)

Haijuzu kuchinja kwa ajili ya mwingine asiyekuwa Allaah ambaye amesema:

فَصَلِّ لِرَبِّكَ وَانْحَرْ

”Basi swali kwa ajili ya Mola wako na [pia ukichinja] na chinja [kwa ajili Yake]!” (at-Takaathuur 108:02)

Amebainisha kwamba swalah na kichinjwa hafanyiwi mwingine asiyekuwa Allaah na kwamba mwenye kuyafanya hayo akamfanyia mwingine asiyekuwa Allaah ni shirki kubwa. Mtume (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam) amesema:

“Allaah amemlaani mwenye kumchinjia asiyekuwa Allaah.”[1]

Nadhiri ni ´ibaadah ambayo hatakiwi kufanyiwa mwingine isipokuwa Allaah pekee:

يُوفُونَ بِالنَّذْرِ وَيَخَافُونَ يَوْمًا كَانَ شَرُّهُ مُسْتَطِيرًا

“Wanatimiza nadhiri na wanaiogopa siku ambayo shari yake ni yenye kuenea.” (al-Insaan 76:07)

Hivo ndivo walivyolingania Mitume watukufu wote (Swalla Allaahu ´alayhim wa sallam).

وَمَا أَرْسَلْنَا مِن قَبْلِكَ مِن رَّسُولٍ إِلَّا نُوحِي إِلَيْهِ أَنَّهُ لَا إِلَـٰهَ إِلَّا أَنَا فَاعْبُدُونِ

“Hatukutuma kabla yako Mtume yeyote isipokuwa Tulimfunulia Wahy ya kwamba: “Hakika hapana mwabudiwa wa haki isipokuwa Mimi; hivyo basi niabuduni.” (al-Anbiyaa´ 21:25)

وَلَقَدْ بَعَثْنَا فِي كُلِّ أُمَّةٍ رَّسُولًا أَنِ اعْبُدُوا اللَّـهَ وَاجْتَنِبُوا الطَّاغُوتَ

”Hakika Tulituma katika kila ummah Mtume kwamba: “Mwabuduni Allaah na jiepusheni na Twaaghuut [waungu batili].” (Ibraahiym 16:36)

 Hivyo basi shikamaneni na mfumo wa Mitume na wabainishieni watu maana ya shahaadah, kwamba maana yake ni kwamba hapana mwabudiwa wa haki isipokuwa Allaah. Ahl-ul-Bid´ah na wanafasalfa wameifasiri kimakosa na wanasema kwamba maana yake ni kuwa hakuna muumbaji wala mwenye kuruzuku isipokuwa Allaah pekee. Tafsiri hii ni ya kimakosa na imewatumbukiza watu wengi katika shirki.

Baada ya hapo linganieni katika Tawhiyd-ul-Asmaa´ was-Swifaat na Tawhiyd-ur-Rubuubiyyah na chukueni msaada kutoka katika vitabu vya Shaykh-ul-Islaam Ibn Taymiyyah na Ibn-ul-Qayyim. Kabla ya hapo mnatakiwa kuifahamu Qur-aan na Sunnah kisawasawa na chukueni msaada kutoka katika tafsiri za Salafiyyah ya Ibn Jariyr, Ibn Kathiyr, al-Baghawiy na ya as-Sa´diy. Kuweni wenye hekima mnapolingania kwa Allaah kama alivosema:

ادْعُ إِلَىٰ سَبِيلِ رَبِّكَ بِالْحِكْمَةِ وَالْمَوْعِظَةِ الْحَسَنَةِ ۖ وَجَادِلْهُم بِالَّتِي هِيَ أَحْسَنُ

“Lingania katika njia ya Mola wako kwa hekima na mawaidha mazuri na jadiliana nao kwa ambayo ni mazuri zaidi.” (Ibraahiym 16:125)

Baada ya haya mnatakiwa kuwabainishia watu Bid´ah za kwenye makaburi na mengineyo ambayo yanapatikana kwa watu. Wale waliokinaika na mfumo wa Mitume mtawaona ni wenye kuitikia kwa urahisi.

[1] Muslim (1978).

  • Mhusika: ´Allaamah Rabiy´ bin Haadiy al-Madkhaliy
  • Mfasiri: Firqatunnajia.com
  • Marejeo: https://www.sahab.net/forums/index.php?app=forums&module=forums&controller=topic&id=158682
  • Imechapishwa: 31/03/2019