Mwanamke mwenye hedhi kusoma vitabu vya dini

Swali: Inajuzu kwangu kwa mfano kusoma vitabu kama “Fiqh-us-Sunnah” au vitabu vyengine vya dini wakati niko na hedhi?

Jibu: Inajuzu kwa mwanamke mwenye hedhi kumdhukuru Allaah, kusema “Subhaan Allaah”, kusema “Laa ilaaha illa Allaah”, kusema “Allaahu Akbar” na asome vitabu vya dini atakavyo. Ni mamoja vitabu hivi ni vya tafsiri ya Qur-aan, Hadiyth za Mtume (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam), vya Fiqh au vyenginevyo. Hakuna neno juu yake kwa kufanya hivo.

Kuhusu kusoma Qur-aan akiwa na hedhi ni jambo ambalo wanachuoni wametofautiana. Lakini maoni tunayoona kuwa yana nguvu ni kwamba si haramu kwake kusoma Qur-aan akihitajia kufanya hivo. Kwa mfano ni mwalimu wa kike na anahitajia kusoma Qur-aan mbele ya wanafunzi wa kike kwa ajili ya mafunzo, akawa ni mwanafunzi wa kike na anahitajia kusoma Qur-aan kwa ajili ya mitihani au mfano wa hayo, katika hali hizi hakuna neno. Kwa sababu, kama alivyosema Shaykh-ul-Islaam Ibn Taymiyyah (Rahimahu Allaah):

“Hakuna Sunnah Swahiyh ya wazi kabisa inayomkataza mwenye hedhi kusoma Qur-aan.”

Msingi ni kutakasika kwa dhimmah na kujuzu kwa jambo hilo. Hili ni tatizo. Lau jambo hilo lingelikuwa ni haramu basi Sunnah ingelisema kwa ubainifu na kwa wazi kiasi cha kwamba isifichikane kwa yeyote. Kutokana na haya tunasema kwa kufuata lililo salama zaidi… kwa sababu mwanamke akihitajia kusoma Qur-aan na yeye yuko na hedhi hakuna neno kufanya hivo. Asipohitajia basi inamtosha kwake kusema “Subhaan Allaah”, kusema “Allaahu Akbar”, kusema “Laa ilaaha illa Allaah” na asome vitabu vya dini kama ilivyo katika swali hili.

  • Mhusika: Imaam Muhammad bin Swaalih bin ´Uthaymiyn
  • Mfasiri: Firqatunnajia.com
  • Marejeo: Nuur ´alaad-Darb (14) http://binothaimeen.net/content/6782
  • Imechapishwa: 12/02/2021