Mwanafunzi aanze kuhifadhi au kuelewa kwanza?

Swali: Kuna mwanafunzi ambaye ana dhamira ya kusoma kwelikweli na anataka mwongozo na nuru. Je, unampendekeza kuhifadhi kwanza au kuelewa? Ni mutuni zipi unazopendekeza ahifadhi?

Jibu: Mimi nampendekeza ahifadhi kwanza yule ambaye bado ni mdogo. Kwa sababu mdogo anatofautiana na mkubwa inapokuja katika kuhifadhi kwa mambo mawili:

1- Uharaka wa kuhifadhi.

2- Kutosahau.

Kwa ajili hiyo kuna mithali ambayo ni maarufu isemayo:

“Elimu utotoni ni kama kuchonga kwenye jiwe.”

Jengine ni kwamba akili ya mtoto haiwezi kubeba kufafanuliwa maana na kumtilia uzito kwa sababu bado ni mdogo. Hili ni mosi.

Pili: Kitu cha kwanza na ambacho ni bora zaidi kinachotakiwa kuhifadhiwa ni Kitabu cha Allaah (´Azza wa Jall). Hili ndio jambo la kwanza. Kwa sababu ukihifadhi Qur-aan ndio msingi katika kuthibitisha hukumu na dalili. Ukikihifadhi na unaweza kukisoma katika hali zote – midhali huna janaba – unaweza kukisoma na huku watembea, ndani ya gari, unaweza kukisoma ukiwa juu ya kitanda chako na katika nyakati zengine midhali huna janaba au sehemu ambazo hazistahiki Qur-aan kusomwa nafasi hiyo.

Kisha baada ya hapo yale yaliyosihi kutoka kwa Mtume (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam) na khaswa khaswa vile vitabu vilivyokhusisha hilo kama “´Umdat-ul-Ahkaam”. Yaliyomo ndani yametolewa katika “as-Swahiyh” mbili. Halafu yale waliyoandika wanachuoni katika Fiqh. Bora katika yale tunayoona sisi ni “Zaad-ul-Mustaqniy´ fiy Ikhtiswaar-il-Muqniy´”. Mwalimu wetu Shaykh ´Abdur-Rahmaan bin Sa´diy (Rahimahu Allaah) alikuwa akitupendezea nacho na akisema kwamba ni katika vitabu vilivyokusanya na vifupi. Jengine ni kwa kuwa wanachuoni wamekifafanua kwa wingi, kuweka maelezo ya chini, taaliki na mengineyo.

  • Mhusika: Imaam Muhammad bin Swaalih bin ´Uthaymiyn
  • Mfasiri: Firqatunnajia.com
  • Marejeo: al-Liqaa’ ash-Shahriy (38) http://binothaimeen.net/content/856
  • Imechapishwa: 19/06/2018