Muumini anatakiwa kusoma vitabu vya al-Albaaniy

Swali: Watu wamechanganyikiwa wanaposoma au kusikia Hadiyth na kama ni Swahiyh au dhaifu. Inasemekana kwamba kitabu ”Swahiyh-ul-Jaamiy´ as-Swaghiyr wa Ziyaadatuh” kinabainisha Hadiyth Swahiyh kutokamana na dhaifu. Unasemaje?

Jibu: Ndio, vitabu vya al-Albaaniy – Allaah amuwafikishe – ni vizuri na vyenye faida. Shaykh Muhammad Naaswir-ud-Diyn al-Albaaniy ni mmoja katika ambao wameweka muda wao wote katika jambo hili. Ameweka bidii kubwa ya kufikia Hadiyth Swahiyh na kuzizindua. Vitabu vyake ni vyenye faida na vyenye kunufaisha. Hata hivyo hakulindwa na makosa. Anaweza kufanya baadhi ya makosa ambapo akaona kuwa ni Swahiyh ilihali ni dhaifu na kinyume chake. Hata hivyo haya yanamtokea mara chache. Mwanafunzi anatakiwa kujitahidi kupambanua kati ya Swahiyh na dhaifu kwa mujibu wa yale yaliyobainishwa na wanazuoni.

Ni vizuri kufaidika na vitabu vya Shaykh Naaswir-ud-Diyn al-Albaaniy. Muumini wa kiume na muumini wa kike wanatakiwa kufaidika navyo na vitabu mfano wake kama vile “as-Swahiyh” ya al-Bukhaariy, “as-Swahiyh” ya Muslim na “Riyaadh-us-Swaalihiyn”. Wanazuoni wameandika vitabu na tungo juu ya Hadiyth dhaifu kukiwemo “Sharh al-Jaamiy´ as-Swaghiyr” na “Kashf-ul-Khifaa´”. Muumini anatakiwa kuvisoma ili anufaike na maneno ya wanazuoni.

Swali: Unasemaje juu ya yale aliyoyadhoofisha Shaykh al-Albaaniy?

Jibu: Kwa ujumla yale aliyoyadhoofisha ni dhaifu na yale aliyoyasahihisha ni Swahiyh, kwa sababu ni mwenye kutilia umuhimu mkubwa maudhui haya na ana uzowefu juu ya mlango huu. Kwa ujumla yale aliyoyadhoofisha na kuyasahihisha ni mazuri na ya sawa.

  • Mhusika: Imaam ´Abdul-´Aziyz bin ´Abdillaah bin Baaz
  • Mfasiri: Firqatunnajia.com
  • Marejeo: http://www.binbaz.org.sa/mat/10533
  • Imechapishwa: 27/06/2021