Mtoto anang´ang´ania kufunga ilihali swawm inamdhuru

Swali: Nina mtoto wa kiume ambaye bado angaliki mdogo anaendelea kung´ang´ania kufunga Ramadhaan pamoja na kuwa kufunga huko kunamdhuru kwa sababu ya udogo wa umri wake na ubaya wa afya yake. Je, nitumie ukali ili aweze kula?

Jibu: Akiwa bado ni mdogo ambaye hajabaleghe sio lazima kwake kufunga. Lakini ikiwa anaweza bila ya uzito anatakiwa aamrishwe. Maswahabah (Radhiya Allaahu ´anhum) walikuwa wakiwafungisha watoto wao. Ilikuwa inafikia mpaka mtoto analia wanampa kitu anacheza nacho. Lakini ikithibiti kuwa kitu hichi kinamdhuru anatakiwa kukatazwa. Ikiwa Allaah (Subhaanahu wa Ta´ala) ametukataza kuwapa watoto wadogo mali zao kwa kuchelea zisije kuwaharibu, basi wana haki zaidi ya kukatazwa na mambo yenye kuwadhuru miili yao. Lakini hata hivyo wanatakiwa kukatazwa kwa njia isiyokuwa ya ukali. Mtu anatakiwa kujiepusha na mwenendo huu pindi anapotangamana na watoto wakati wa kuwalea.

  • Mhusika: Imaam Muhammad bin Swaalih bin ´Uthaymiyn
  • Mfasiri: Firqatunnajia.com
  • Marejeo: Majmuu´-ul-Fataawaa (19/83)
  • Imechapishwa: 28/05/2017