2590- Ibn ´Abbaas (Radhiya Allaahu ´anhumaa) amesema:

”Nilimjia Mtume wa Allaah (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam) ilihali anaswali mwishoni mwa usiku. Nikasimama nyuma yake ambapo akanishika kwa mkono wake na akaniweka kwenye msitri mmoja sawasawa naye. Pindi Mtume wa Allaah  (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam) alipoanza kuswali tena nikarudi nyuma. Wakat Mtume wa Allaah (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam) alipomaliza kuswali akanambia: ”Ni kwa nini ulirudi nyuma?” Nikasema: ”Ee Mtume wa Allaah! Hivi kweli inamstahikia yeyote kuswali msitari mmoja sawa na wewe ilihali wewe umetunukiwa kuwa Mtume wa Allaah?” Akapendezwa na maneno yangu ambapo akaniombea kwa Allaah anizidishie elimu na ufahamu wangu.”

Ameipokea al-Haakim (3/534) na Ahmad (1/330) na matamshi ni yake. al-Haakim amesema:

”Ni Swahiyh juu ya masharti ya al-Bukhaariy na Muslim.”

adh-Dhahabiy ameafikiana naye, usawa ni kama alivosema.

Ndani yake kuna faida muhimu ambayo huenda isipatikane katika vitabu vyengine vya Fiqh (bali katika baadhi yake vipo vinavyoikhalifu); Sunnah wakati mtu anaposwali na imamu asimame upande wake wa kuume na kwenye msitari mmoja sawasawa naye. Asisimame mbele yake wala nyuma yake. Haya ni kinyume na yale yanayosemwa na baadhi ya madhehebu kwamba yule mwenye kuongozwa anatakiwa kusogea nyuma kidogo ya imamu kwa njia ya kwamba vidole vya miguuni mwake viwe kwenye msitari mmoja sawasawa na kisigino cha imamu au mfano wake. Haya kama unavoona yanapingana na Hadiyth hii ambayo ni Swahiyh ambayo imetendewa kazi na baadhi ya Salaf. Naafiy´ amesema:

“Siku moja nilisimama nyuma ya ´Abdullaah bin ´Umar alipokuwa anaswali na nyuma yangu hapakuwa mtu mwengine zaidi yangu. Akaashiria kwa mkono wake kwamba nisimame msitari mmoja sawasawa naye.”[1]

´Ubaydullaah bin ´Abdillaah bin ´Utbah amesema:

“Niliingia nyumbani kwa ´Umar bin al-Khattwaab ambapo nikamkuta alikuwa anaswali swalah ya sunnah. Nikasimama nyuma yake ambapo akanivuta karibu mpaka akaniweka msitari mmoja sawasawa naye upande wa kuliani mwake. Wakati Yarfa´ alipokuja nikasogea kwa nyuma ambapo tukasimama safu moja nyuma yake.”[2]

Wakati (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam) alipokuwa katika hali ya kukata roho aliingia msikitini na akaketi kwenye msitari mmoja sawasawa na Abu Bakr as-Swiddiyq ambaye alikuwa anawaongoza watu katika swalah upande wa kushoto kwake[3]. Hadiyth hii ni Swahiyh.

[1] al-Muwattwa’ (1/154).

[2] al-Muwattwa’ (1/169-170). Sanadi zake ni Swahiyh.

[3] Mukhtaswar al-Bukhaariy (366).

  • Mhusika: Imaam Muhammad Naaswir-ud-Diyn al-Albaaniy
  • Mfasiri: Firqatunnajia.com
  • Marejeo: Silsilat-ul-Ahaadiyth as-Swahiyhah (6/1/174-176)
  • Imechapishwa: 25/04/2019