Swali: Sisi tunaishi na watu ambao wanatumbukia katika mambo ambayo yanamkasirisha Allaah na Mtume wake. Kama kama ambao wanachukulia wepesi jambo la swalah, wananyoa ndevu zao, wanaume wanaovaa mavazi marefu yenye kuvuka kongo mbili za miguu na maasi mengine ya waziwazi. Tunatakiwa kuwa na msimamo gani kwao?

Jibu: Ambaye anachukulia wepesi jambo la swalah ni mbaya zaidi kuliko ambaye ananyoa ndevu zake. Kunyoa ndevu ni maasi na ni haramu. Hapana shaka juu ya hilo. Lakini kuchukulia wepesi jambo la swalah ni khatari zaidi. Huyu akiendelea kuchukulia wepesi jambo la swalah basi usitangamane naye na wala usikae naye baada ya kumnasihi. Jitenge naye mbali.

Kuhusu ambaye ananyoa ndevu zake mbainishie Hadiyth zilizopokelewa juu ya jambo hili na mnasihi. Pengine Allaah akamwongoza. Asipokubali jitenge naye mbali. Kwa sababu ukitangamana naye ni kama kwamba umeridhia yale anayofanya.

Mtume (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam) ameeleza kuhusu wana wa israaiyl ya kwamba mmoja wao alikuwa akikutana na ndugu yake katika maasi ambapo anamnasihi, kisha anakutana naye kwa mara ya pili akamnasihi, kisha anakutana naye kwa mara ya tatu akamnyamazia na wala hilo halimzuii kula pamoja naye, kukaa naye na kunywa naye. Allaah alipoona hali hiyo akazikutanisha nyoyo zao na akawalaani kupitia ulimi wa Mitume wao. Amesema (Ta´ala):

لُعِنَ الَّذِينَ كَفَرُوا مِن بَنِي إِسْرَائِيلَ عَلَىٰ لِسَانِ دَاوُودَ وَعِيسَى ابْنِ مَرْيَمَ ۚ ذَٰلِكَ بِمَا عَصَوا وَّكَانُوا يَعْتَدُونَ كَانُوا لَا يَتَنَاهَوْنَ عَن مُّنكَرٍ فَعَلُوهُ

“Wamelaaniwa wale waliokufuru katika wana wa israaiyl kwa ulimi wa Daawuud na ‘Iysaa mwana wa Maryam. Hivyo ni kwa sababu ya kuasi kwao na walikuwa wakivuka mipaka. Walikuwa hawakatazani maovu waliyofanya.” (05:77-78)

Mtenda maasi akiendelea juu ya maasi yake na asipokee nasaha kutoka kwako, basi usiikae naye. Bali jitenge naye mbali. Usiikae naye isipokuwa wakati wa dharurah na wakati huohuo uchukie yale anayofanya. Ama kukiwa hakuna dharurah yoyote jiepushe naye mbali.

  • Mhusika: Imaam Swaalih bin Fawzaan al-Fawzaan
  • Mfasiri: Firqatunnajia.com
  • Marejeo: Sharh Nawaaqidh-il-Islaam https://ajurry.com/safrawy/chorohat-elakida/chorohat-nawakid-elislam/charh-salah-fawzan/04.mp3
  • Imechapishwa: 01/12/2018